Kutengeneza Nyusi
Question
Nini hukumu ya mwanamke kutengeneza nyusi?
Answer
Sharia tukufu imemuhimiza mwanamke ajipambe na ajirembeshe kwa ajili ya mumewe; imepokelewa kutoka kwa Asmaa bint Yazid Al-Ansariyyah kwamba Mtume (S.A.W) alimwambia alipomuuliza kuhusu vitendo walivyohusishwa navyo wanaume pekee kama jihadi na mengineyo, akamuuliza je mwanamke anashirikiana na mumewe katika hilo? Akamwambia: «Nenda ewe mwanamke, na uwaambie wanawake walioko nyumbani kwako kuwa kufanya wema wa mwanamke mmoja wenu kwa mumewe, na kutafuta radhi zake, na kufuata mambo anayoyapenda, ni sawa na (malipo ya) hayo yote»; yaani: anayejipamba na kujirembesha kwa mumewe ana malipo na thawabu za jihadi, Hija na ibada nyinginezo.
Hivyo, mwanamke kutengeneza nywele za nyusi zilizozidi kiasi cha kawaida kwa ajili ya kujirembesha kwa mumewe ni jambo linalopendekezwa kisharia; imepokelewa kutoka kwa Aisha kwamba alimwambia mwanamke aliyekuwa akiondoa nywele za uso wake ili ajirembeshe kwa mumewe: «Ondoa kero kutoka kwako, na ujitengeneze kwa ajili ya mumeo».
Ama yale yaliyokuja kuhusu uharamu wa An-Nams katika kauli ya Mtume (S.A.W): «Mwenyezi Mungu amewalaani wenye kuchanja na wanaochanjwa, na wanaonyofoa nyusi na wanaonyofolewa, na wanaoweka nafasi kati ya meno kwa ajili ya uzuri wanaobadilisha uumbaji wa Mungu»; kinachokusudiwa ni mwanamke ambaye hajaolewa na anafanya hivyo ili kuwafitini wanaume, na pia yule ambaye haruhusiwi pambo kama mwanamke aliyefiwa na mumewe akiwa katika eda.
Maelezo
Ni katika Sunna kwa Muislamu kusafisha mwili wake na kujali uzuri wa muonekano wake, kutoka kwa Abu Hurairah (R.A) kutoka kwa Mtume (S.A.W) amesema: ((Maumbile ni matano — au matano ni katika Fitra —: Kutahiri, kunyoa nywele za siri, kukata kucha, kunyofoa nywele za kwapani, na kupunguza sharubu)) [1].
Sharia imependekeza mwanamke ajipambe kwa mumewe na ikamwekea malipo makubwa. Kutoka kwa Asmaa bint Yazid Al-Ansariyyah kwamba Mtume (S.A.W) alimwambia: ((... Nenda ewe mwanamke, na uwaambie wanawake walioko nyumbani kwako kuwa kufanya wema[2] wa mwanamke mmoja wenu kwa mumewe, na kutafuta radhi zake, na kufuata mambo anayoyapenda, ni sawa na (malipo ya) hayo yote)) [3]. Yaani: anayejipamba na kujirembesha kwa mumewe ana malipo na thawabu za Jihadi, Hija na ibada nyinginezo.
Ama kuhusiana na kunyofoa na kutengeneza nyusi: kwa mwanamke kuondoa au kunyofoa nywele za nyusi zilizozidi kiasi cha kawaida ambazo zinaweza kumfanya mume amkinai mkewe asipozitengeneza, hilo ni jambo linalojuzu na kupendekezwa kisharia; kutoka kwa Aisha (R.A) : «Mwanamke mmoja alisema: Ewe Mama wa Waumini, hakika katika uso wangu kuna nywele (nyusi), je ninyofoe ili nijirembeshe kwa mume wangu? Aisha (R.A) akasema: Ondoa kero kutoka kwako, na ujitengeneze kwa ajili ya mumeo kama unavyojitengeneza kwa ajili ya kutembelewa...» [4].
Ama kwa mwanamke ambaye hajaolewa, haijuzu kwake kuchukua chochote katika asili ya nywele ya nyusi yake isipokuwa kuondoa zile zilizozidi na zilizojitokeza ovyo pekee, bila kufanya hivyo kwa ajili ya urembo.
Uharamu wa An-Nams[5] ulioelezwa katika Hadithi ya Abdillah Ibn Mas'ud (R.A) ambapo Mtume (S.A.W) amesema: ((Mwenyezi Mungu amewalaani[6] wenye kuchanja na wanaochanjwa, na wanaonyofoa nyusi na wanaonyofolewa, na wanaoweka nafasi kati ya meno kwa ajili ya uzuri wanaobadilisha uumbaji wa Mungu)) (Imepokelewa kutoka kwa Imamu Muslim).
Kinachokusudiwa ni kuwa mwanamke anastahili adhabu katika hali mbili:
Mwanamke ambaye hajaolewa, na anafanya hivyo ili kuwafitini wanaume. Wanachuoni wa Fiqhi walisema: «Kunyofoa nyusi ni kuondoa nywele... na pengine inahusu anapofanya hivyo ili kujipamba kwa ajili ya watu wageni»[7].
Mwanamke ambaye haruhusiwi pambo; kama aliyefiwa na mumewe akiwa katika eda. Wanachuoni wa Fiqhi walisema: «Katazo linahusu mwanamke aliyekatazwa kutumia pambo kama aliyefiwa na mumewe au aliyepotewa na mume, hivyo haipingani na yaliyopokewa kwa Aisha kuhusu ruhusa ya kuondoa nywele za nyusi na uso»[8].
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
Inajuzu kwa mwanamke aliyeolewa kutengeneza nywele za nyusi zilizozidi maadamu ni kwa ridhaa ya mumewe, na inapendekezwa kwake kufanya hivyo ikiwa ni kwa ajili ya kujirembesha kwa mume na kuishi naye vizuri.
Mwanamke ambaye hajaolewa haijuzu kwake kuchukua chochote katika asili ya nywele za nyusi zake isipokuwa kuondoa zile zilizozidi na zilizojitokeza ovyo pekee bila urembo.
[1] Imepokelewa kutoka kwa Al-Bukhari na Musalim.
[2] «Tabayyu'l»: Kujirembesha.
[3] Imepokelewa kutoka kwa Al-Bayhaqi katika “Shu’ab Al-Iman” (11/178).
[4] Imepokelewa kutoka kwa Abd al-Razzaq katika Musannaf wake (3/146).
[5] «An-Nams»: Kuchukua au kunyofoa nywele za nyusi.
[6] «Laana»: Kustahili kufukuzwa katika rehema ya Mwenyezi Mungu.
[7] Hashiyat Ibn Abidin “Radd AlMuhtaar” (6/373)
[8] Hashiyat al-Adawi “Kifayat al-Talib al-Rabbani” (2/459).
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
