Hukumu ya mgonjwa kukataa kumeza da...

Egypt's Dar Al-Ifta

Hukumu ya mgonjwa kukataa kumeza dawa

Question

Baba yangu aliugua, akaenda kwa daktari ambaye alimfanyia uchunguzi na kumuandikia dawa. Baada ya kununua dawa hizo, baba yangu amekataa kuzitumia. Je, ni nini hukumu ya yeye kukataa kutumia dawa? Ikizingatiwa kuwa daktari ametuambia kuwa atapata nafuu akizingatia mpango wa matibabu.

Answer

Ni halali kwa mwanadamu kukimbilia kile kinachopunguza maumivu yake na kurahisisha uzito wa maradhi, na hilo halipingani na kumtegemea kwake Mwenyezi Mungu. Kama vile ambavyo kuchukua sababu za kisharia hakupingani na kumtegemea kwake Mwenyezi Mungu; basi mgonjwa anapaswa kuchukua sababu za kupona ili aishi kwa afya njema. Vilevile, anapaswa kuwa na juhudi ya kutumia dawa kwa kadiri ya uwezo wake na asiziache; ili aweze kutimiza wajibu wake kwa nafsi yake, familia yake, na nchi yake kwa ukamilifu zaidi. Pia ili asipelekee kuongezeka kwa ugonjwa au kuenea kwake na kusambaa katika mwili wake wote, na kugeuka kutoka kuwa ugonjwa wa muda na kuwa ugonjwa wa kudumu.

Maelezo

Imeamuliwa kisharia kwamba kuchukua sababu ni Sunna ya ulimwengu; kwani Mwenyezi Mungu Aliyetukuka ameunganisha sababu na matokeo yake, akajaalia kila kitu kina sababu, na akamuamuru mwanadamu achukue sababu hizo. Na kwa kadiri ya ufanisi wa kuchukua sababu, ndivyo matokeo yanavyokuja. Sababu zenyewe hazina nguvu kwa dhati yake, bali daima zinahitaji amri ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na matakwa Yake. Hivyo, jitihada katika kutafuta sababu kwa viungo vya mwili ni kumtii Mwenyezi Mungu, na kumtegemea kwa moyo ni imani Kwake na kudhania kheri Kwake. Aliyetukuka anasema: {Na litikise kwako shina la mtende, utakuangushia tende mbivu zilizo tayari kuliwa} [Maryam: 25]. Basi hakuna neno kwa mwanadamu kukimbilia kile kinachopunguza maumivu yake na kurahisisha uzito wa maradhi, na hilo halipingani na kumtegemea kwake Mwenyezi Mungu.

Sharia ya Kiislamu imemuamuru mwanadamu kujilinda nafsi yake na afya yake; ikamhimiza mgonjwa wakati ugonjwa unapomshukia ajitibu, na ikajaalia uhusiano kati ya ugonjwa na tiba kuwa ni uhusiano wa sababu na tokeo. Kutoka kwa Usama bin Sharik (R.A.) amesema: “Mabedui walisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Je, tusijitibu? Akasema: "Ndiyo, enyi waja wa Mwenyezi Mungu, jitibuni; kwani Mwenyezi Mungu hakuweka ugonjwa isipokuwa ameuwekea shifaa (ponyo)," au akasema: "dawa, isipokuwa ugonjwa mmoja tu." Wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni upi huo? Akasema: "Uzee"”[1]. Katika hadithi hii kuna uhalali wa kujitibu, uhalali wa kufanyiwa matibabu na madaktari, na kujuzu kwa tiba na matibabu.

Wanazuoni wa Fiqhi wametofautiana kuhusu hukumu ya mgonjwa kutumia dawa katika hali ambayo ugonjwa unatarajiwa kupona, ambapo wafuasi wa madhehebu ya Hanafi na Maliki: Wanaona kuwa kutumia dawa kwa mgonjwa ni halali (Mubaha) na si wajibu, hasa ikiwa kuacha kutumia dawa hakupelekei kuangamia (kifo). Baadhi yao waliona kuwa utabibu si wajibu bali ni halali, na hakuna tofauti kati ya mwanamume na mwanamke.

Wengine: Wanaona kuwa kujitibu ni Sunna kwa sababu ya kitendo cha Mtume (S.A.W.) mwenyewe, kuitafuta kwake tiba, na kuhimiza kwake kuitumia. Wakati huo huo, kumlazimisha mgonjwa kutumia dawa ni chukizo (Makruh).

Baadhi ya Wataalamu wa Fiqhi: Wanaona kuwa ni wajibu kutumia dawa ikiwa dawa hiyo ni yenye manufaa na kuacha kuitumia kutapelekea kuangamia kwa mujibu wa kauli ya daktari mwaminifu; mfano wa kuweka kidonda kwenye جبيرة (mti wa kufungia kiungo kilichovunjika) na mfano wake, ambapo kama isipowekwa inaweza kupelekea kuharibika kwa kiungo kilichoumia.

Wengineo: Wanaona kuwa kuacha kujitibu ni bora zaidi na kukifanya ni jambo linalojuzu; hasa kwa kuwa kuacha ni katika uzuri wa kumtegemea Mwenyezi Mungu. Hata hivyo, kutumia dawa hakupingani na kumtegemea Mwenyezi Mungu kutokana na kitendo cha Mtume (S.A.W.) na amri yake, naye ndiye bwana wa wanaomtegemea Mwenyezi Mungu; kwa mujibu wa habari ya Abu Darda kwamba (S.A.W.) amesema: “Hakika Mwenyezi Mungu ameteremsha ugonjwa na dawa, na akajaalia kwa kila ugonjwa kuna dawa; basi jitibuni, wala msijitibu kwa haramu”.

Inapaswa kwa mgonjwa kuchukua sababu za kupona ili aishi kwa afya njema, hivyo ajitahidi kutumia dawa kwa kadiri ya uwezo wake na asiziache; ili aweze kutimiza wajibu wake kwa nafsi yake, familia yake, na nchi yake kwa ukamilifu zaidi. Hali hiyo inasisitizwa zaidi ikiwa madaktari wanaona kuwa katika kuacha kwake kutumia dawa kuna kuongezeka kwa ugonjwa, kuenea kwake, au kusambaa na kuchanua katika mwili wake wote, na kugeuka kutoka kuwa ugonjwa wa muda na kuwa ugonjwa wa kudumu. Kwa hiyo, msimamo wa kutumia dawa ndio ulio bora zaidi katika zama zetu hizi, hasa baada ya mapinduzi makubwa ya kielimu katika nyanja za tiba na dawa. Hata hivyo, ikiwa itakuwa vigumu kwa mgonjwa kutumia dawa na nafsi yake ikawa inaichukia, akaacha kuitumia na ikawa kuacha huko hakupelekei kuenea kwa maambukizi (kwa wengine), basi hana dhambi kwa kufuata msimamo wa wale waliojuzisha kuacha miongoni mwa wanazuoni wa Fiqhi.

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Inampasa mgonjwa kutumia dawa kama alivyoelekezewa na daktari, hasa ikiwa madaktari wamethibitisha kuwa katika kuacha kwake kutumia dawa kuna kuongezeka kwa ugonjwa na kuenea kwake, au kuchanua na kusambaa katika mwili wake wote, na kugeuka kutoka kuwa ugonjwa wa muda na kuwa ugonjwa wa kudumu. Ikiwa itakuwa vigumu kwake kutumia dawa na nafsi yake ikawa inaichukia, akaacha kuitumia na ikawa kuacha huko hakupelekei kuangamia (kifo) au kuenea kwa maambukizi, basi hatapata dhambi kwa kuacha huko, kwa kufuata msimamo wa wale waliojuzisha kuacha miongoni mwa wanazuoni wa Fiqhi; hasa kwa kuwa yeye ndiye anayewajibika na nafsi yake na ndiye anayebeba matokeo ya maamuzi yake, na haijuzu kumlazimisha jambo lolote bila ridhaa yake.

 

[1] Imetolewa na Imam Al-Tirmidhiy.

Share this:

Related Fatwas