Ndoa ya Misyaar

Egypt's Dar Al-Ifta

Ndoa ya Misyaar

Question

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na rehma na amani zimwendee bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, masahaba wake na wanaomfuata, na baada ya hayo:

Answer

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na rehma na amani zimwendee bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, masahaba wake na wanaomfuata, na baada ya hayo:

Ndoa ni mkataba wa maneno baina ya watu wawili; mwanamume na mwanamke ambao hawana vizuizi vya kisheria, hali yake kama mkataba wowote ambao unasihi kisheria kwa kupatikana sharti na nguzo zake na kutokuwepo vizuizi vyovyote. kadhalika mkataba katika Fiqhi ya Kiislamu kimsingi unaweza kuwa kwa maneno.

Basi kama likifanywa katika upande wa kuanza kutoka kwa aliye na sifa kamili za kutenda, masharti na nguzo zake zikiwa zimekamilika bila vizuizi, basi huzingatiwa kuwa mikataba ni sahihi, inafuata athari zake na hukumu zinazofuatia.

Katika ndoa ya Misyaar, mkataba wa ndoa unafungwa, sharti na nguzo zinatimizwa, ila mwanamke anakubaliana na mumewe ili aiche haki yake ya kulala naye na kumpa matumizi au mojawapo ya mawili hayo.

Na "Misiyar" silo neno la kiajemi –kama anavyosema Sheikh Al Qaradhawiy- lakini ni neno la kawaida katika lahaja za nchi za Ghuba, labda maana yake ni kupita na kutokaa muda mrefu, basi inadhihirika ndoa ya Misiyar ilichukua maana yake kutokana na  maana hiyo. [Fatawa Muasweraha 291/3]. Kwani mwanamume katika ndoa hiyo anamtembelea mke wake katika nyakati mbalimbali, na hakai naye muda mrefu.

Kimsingi aina hiyo ya ndoa ni halali ikiwa mkataba umetimiza sharti na nguzo zake zinazotakikana kisheria, nazo ni: ijaabu (makubaliano ya kuoana), kuwepo kwa walii, mashahidi na kutokuwepo vizuizi vya kisheria kwa wanandoa.

Mkataba huo ukitimizwa sharti na nguzo zake, basi unakuwa na haki zinazoambatana na mkataba wa kindoa kama vile Nasaba, Urithi, Eda, Talaka, kuingiliana, kukaa na matumizi na wajibu na haki nyingine ziambatazo na ndoa, lakini wanandoa wakiafikiana kwamba mke aache haki ya kukaa au kupata matumizi, basi mwanamke akiacha haki yake au baadhi yake inajuzu kisheria kwani yeye ndiye mwenye haki hiyo naye anaweza kuiacha bila ya kuathiri hali ya kusihi mkataba wa ndoa.

Ibn Qudama alisema katika kitabu chake “Al Mugh-niy” alipozungumzia aina za masharti ya ndoa: “Sehemu ya pili: yanayobatilisha sharti na yanayohahikisha mkataba, kama vile ikishurutishwa kutokuwa na mahari kwa mke au kutompa matumizi au mke ashurutishe asiingiliane na mumewe au mumewe atumie kinga ya kuingiliana (kinga za mimba) au mumewe ampe siku zaidi ya mke mwenza au mumewe ashurutishe asimtembelee zaidi ya siku moja kila wiki au amtembelee mchana tu bila ya usiku au mumewe amshurutishe mkewe ampe matumizi au ampe kitu angalau hata kidogo, basi masharti hayo yote ni batili; kwani hayaafikiane na maana inayotakikana na mkataba tena kwa kuwa yanamaanisha kuondosha yaambatanazo na mkataba hata kabla ya kufungika, kwa hiyo haijuzu kama ilivyo haki ya wamiliki wawili, mmoja hana haki ya kumshurutisha mwenzake aiache haki yake kabla ya mauzo.

 Ama mkataba wenyewe, basi unakuwa ni sahihi; kwani masharti yale yanaambatana na vitu vya ziada ambavyo havilazimishwi kuvitaja tena haidhuru kutovitaja kwa hiyo havibatilishi mkataba kama ikishurutishwa mahari ambayo asili yake ni haramu”. [Al Mughniy 72/7]

Suala la kujuzu kwa mwanamke aache baadhi ya haki zake wakati wa kufunga mkataba wa ndoa yake linarejea maneno ya Mwenyezi Mungu: {Na mwanamke akichelea kutupwa na kutojaliwa na mumewe, basi si vibaya kwao wakisikizana kwa suluhu. Na suluhu ni bora. Na nafsi zimewekwa machoni mwake tamaa na choyo. Na mkifanya wema na mkamchamungu basi hakika Mwenyezi Mungu Anazo khabari za yote mnayoyatenda} [AN-NISAA, 128].

Ilisimuliwa kutoka kwa Mama wa Waumini Bi. Aisha R.A. ya kwamba sababu ya kushuka kwa Aya hiyo ni: “Mume anakuwa na mke hali ya kuwa amemchukiza hamtaki anataka kuachana naye, na mkewe amwambie: “nakupa uhuru wa kuniacha”, basi Aya hiyo ilishuka katika suala hilo”. [Sahihi Al Bokhariy 2318]

Na Kutoka kwa Ibn Abass R.A. alisema: “Bi. Sauda aliogopa Mtume s.a.w. amwache akamwambia: usinipe talaka niache niishi nawe na siku yangu mpe Bi. Aisha, basi Mtume S.A.W. akafanya na hiyo Aya ilishuka: (basi si vibaya kwao wakisikizana kwa suluhu. Na suluhu ni bora)”. [Sunan At Tirmiziy 3040]

Ndoa ya Misyaar siyo mpya katika Fiqhi ya Kiislamu lakini jina lake ndilo jipya na aina hiyo ni ya zamani ambayo ilikuwa inajulikana kwa jina la ndoa ya “NAHARIYAT AU LAYLIYAT (ndoa ya kukutana mchana au usiku)”, na mazingatio hapa yanakuwa katika hukumu siyo majina.

Ilitajwa katika kitabu cha Fat-h Al Qadir kilichotungwa na Al Kamal bin Al Hamam Al Hanafiy: “Si vibaya kuwaoa AL NAHARIAT nao ni: kuwaoa wanawake sharti kukutana nao mchana sio usiku”. [Kitabu cha Fat-hu Al Qadeer 249/3]

Imamu Ahmad alisema - kama ilivyotajwa katika kitabu cha Al Mughniy - katika suala la mwanamume ambaye kamwoa mwanamke akamshurutisha akae naye mara moja kila wiki halafu mkewe akarejea na kusema: sikubali ila siku baada ya siku, akasema Imamu Ahmad: Ana haki ya kuachana na ombi lake kwa hiari yake na hiyo inajuzu ama akisema: Sikubali ila baada ya kugawanya masiku, basi ni haki yake anaweza kuiomba muda wowote akitaka. Aidha ilisimuliwa na Al Athram katika suala la mwanamume anayemwoa mwanamke akamshurutisha aende kwake siku maalumu kwamba inajuzu lakini mkewe akifuta maneno yake akirudi kuomba haki yake basi anakuwa na haki ya kuomba, kadhalika alisema katika suala la mwanamume anayemwoa mwanamke sharti ampe matumizi ya derham tano au kumi kila mwezi ya kwamba ndoa hiyo inajuzu kisheria, naye mkewe ana haki ya kufuta maneno yake. Naye Al Maruzi alirejea aliyoyasema Imamu Ahmad katika suala la Al Nahariat na AL Layliyat akasema: Aina hiyo ya ndoa haiafikiani na ndoa ya watu wa Uislamu. Naye Hamad bin Abi Sulaiman na Ibn Shubruma ni miongoni mwa waliochukizwa na  suala la kuwaoa AL NAHARIYAT. Na Al Thauriy alisema: Hapa sharti ni batili. Ingawa Al Hassan na A’twaa walikuwa haoni vibaya katika ndoa ya AL NAHARIYAT, naye Al Hassan alikuwa haoni vibaya kwa mtu amwoe mwanamke sharti aainishe kwake siku maalumu kukutana naye kila mwezi. Hapa uchukizo wa wanaochukizwa na suala hilo unarejea kubatilisha sharti na kujuzu kwa wanaojuzu kunarejea asili ya ndoa, kwa hiyo maoni yao yanaafikiana juu ya usahihi wa ndoa na kubatilisha sharti. [Al Mughniya kwa Ibn Qudamah 72/7 kwa mageuzi madogo]

Maana ya kauli ya Imamu Ahmad: Aina hiyo ya ndoa haiafikiani na ndoa ya watu wa Uislamu; si ndoa kamili, kama unavyosema: Si Muumini asiyependa ya nduguye, kwa anayoyapenda ya nafsi yake. [Kitabu cha Fatawa Muaserah kwa Sheikh Al Qaradhawiy 294/3] Na maana inayotakikana hapa: Si Muumini mwenye imani kamili asiyependa ya nduguye kwa anayoyapenda ya nafsi yake.

Ingawa baadhi ya Maulamaa wameelekea kutojuzu aina hiyo ya ndoa, wakapata dalili kuthibitisha kauli yao, na miongoni mwa dalili hizo ni:

Mkataba katika aina hiyo ya ndoa unakuwa unaambatana na baadhi ya masharti yanayohitalifiana na lengo “maana” la mkataba, kama sharti la mwanamke kuachana na haki yake katika kugawanya siku za wiki na mke mwenza, matumizi n.k., masharti hayo ni mabaya yanaweza kubatilisha mkataba.

Ilitangulia kujadili dalili hizo kutokana na kauli ya Imamu Inb Qudama kuhusu sehemu ya pili ya masharti ya ndoa, ambayo ilitajwa kwamba mkataba unajuzu kisheria lakini unakuwa na sharti baya.

Ndoa kwa aina yake hiyo inahitalifiana na makusudio ya Sheria ya Kiislamu yanayoelekeza kuleta pahala pa kukaa, mapenzi pamoja na ulezi kwa watoto.

Kiufupi: sisi hatusemi kwamba aina hiyo ya ndoa haiafikiani na ndoa sahihi ya Kiislamu inayotakikana, [[Kitabu cha Fatawa Muaserah kwa Sheikh Al Qaradhawiy 295/3]. Bali tunasema kwamba aina hiyo inalifikia lengo kuu la ndoa nalo ni kujizuia na machafu kama ilivyokuja katika Hadithi ya Mtume S.A.W,  “Enyi vijana yeyote anayekuwa na uwezo wa ndoa, basi aoe kwani inamwondolea tamaa na kulinda tupu”. [Imeafikiana nayo, Sahihu Al Bokhariy 4779, na Sahihi Muslim 1400]

Ndoa ya Misyaar kimsingi inategemea hali ya usiri na kufichika na asili ya ndoa katika Sheria ya Kiislamu ni kutangazwa.

Hapa baadhi ya watu walijibu kauli hiyo kwamba suala la usiri silo kitu cha msingi katika aina hiyo ya ndoa, bali aina hiyo inaweza kuwa na aina ya tangazo na rekodi katika masjala ya kiserikali (rasimu) aidha suala la kuficha ndoa baada ya kukamilika masharti na nguzo zake hakuifanyi kuwa ni batili kwa mujibu wa maoni ya wengi wa Maulamaa wa kifiqhi.

Na yaliyonakiliwa na Wamaliki kuhusu suala la kushurutishia hali ya usiri kwa mashahidi ili wafiche habari ya ndoa, basi hayo yanajibiwa kwamba mashahidi wakishurutishwa wawe na usiri wakati wa kufunga mkataba, ama ikitokea bada ya kufunga mkataba basi haidhuru. [Kitabu cha Fatawa Muaserah kwa Sheikh Al Qaradhawiy 300/3- pamoja na As Sharhu Al Kabeer Sheikh Ad Dardier 236/2]

Ndoa hiyo inakuwa na aina nyingi za marufuku za kisheria, kwani baadhi ya wanawake wanaweza kuchukua aina hii ya ndoa kama ni njia ya kufanya machafu wakadai kwamba wameolewa kwa njia ya ndoa ya Misyaar, kwa hiyo inalazimika kukataza aina hiyo ya ndoa ili kujiepusha na mambo ya shaka.

Ingawa kauli hii inajibiwa kwamba inapindukia mipaka katika suala la kujiepusha na mambo ya shaka, kwani aina hiyo ya ndoa inaweza kusaidia katika kuilinda nafsi na mambo machafu.

Ndoa ya aina hiyo inaletea madhara kwa mke wa kwanza; kwani mumewe atatembelea mkewe wa pili kukaa nae na kufanya mapenzi naye bila ya mke wa kwanza kujua, jambo ambalo linapuguzia haki ya mke wa kwanza.

Rai hiyo inajibiwa kwamba, si lazima ndoa hiyo ya Misyaar iwe ya pili, bali inaweza kuwa ya kwanza au ya pili tena mke anaweza kuwa na taarifa nayo.

Tena mume akiwa na mke wa pili lakini analificha suala lake kwa mke wa kwanza, basi haidhuru ikiwa anaangalia kwa uangalifu haki za mke wa kwanza katika kukaa naye na matumizi yake n.k.

Aina hiyo ya ndoa inavunja heshima ya mwanamke, licha ya kuwa haina mwelekeo wa hali ya jambo baadaye kwa talaka akiomba mke haki yake kugawanya siku za wiki au akiomba haki yake ya kupata matumizi, aidha aina hiyo ya ndoa inakuwa kama njia ya kumkandamiza mke kutokana na hali yake ilivyo; kwani yeye akipata mume kwa mujibu wa ndoa ya kawaida hatakubali kwa namna hiyo ya ndoa ya Misyaar.

Rai hiyo inajibiwa kwamba, hakuna uhusiano wa karibu kati ya hali ya kuomba mke haki yake katika kugawanya siku za wiki na mke mwenza au kupata matumizi na kuachika “kutalikiwa”; kwani talaka inaweza kutokea kwa sababu yoyote nyingine mbali na kuomba mke haki yake ya kupata matumizi au kugawanya siku za wiki na mke mwenza.

Mume kwa mujibu wa ndoa hiyo anaweza kumkandamiza mkewe akiona ana mali na utajiri hali ya kuwa mke ana shida naye, basi anaweza kumkandamiza ili apate manufaa yoyote.

Rai hiyo inajibiwa kwamba, kumkandamiza mke kunaweza kutokea hata katika ndoa ya kawaida, bali jambo hilo linatokea mara nyingi, mume anamkandamiza mkewe halafu anamwacha au anampa talaka, na jambo hilo linaambatana zaidi na imani na tabia na halina uhusiano na aina ya ndoa.

Aina hiyo ya ndoa haiafikiani na yaliyotajwa na Mwenyezi Mungu kuhusu mume na haki yake ya kuwa mlinzi wa mkewe; kwani katika aina hiyo ya ndoa hatobeba jukumu la kutoa matumizi wala pahala pa kukaa, naye Mwenyezi Mungu Amefanya mume awe mlinzi wa mkewe kwa mambo mawili;

La kwanza: Amefadhilisha baadhi yao kuliko wengine kwa sababu ya sifa ambazo Mwenyezi Mungu Amewapa ili wawe na uwezo wa kuvumilia na subira.

 La pili: kwa wanazozitoa; mahari na matumizi.

Rai hiyo inajibiwa kwamba kukubali kwa mume suala la mkewe kuacha haki yake ya kupata matumizi hakumaanishi mume aache haki yake ya kuwa mlinzi wa mkewe; hakuna uhusiano baina ya masuala hayo mawili.

Upambanuzi katika tofauti zilizopo kati ya ndoa ya Misyaar na ndoa ya Mutaa’ “ndoa ya muda maalumu”

Ndoa ya mutaa inakuwa kwamba mwanamume anamwambia mwanamke: nakupa kadhaa niingiliane nawe kwa siku moja, mwezi mmoja au mwaka n.k. akiainisha muda kama ilivyotangulia katika mifano au akiuacha bila ya kuainisha yote ni sawa, kama kwamba anasema: nakupa kadhaa niingiliane nawe msimu wa Hija au kwa muda nitakaobaki nchini au mpaka Zaidi arudi hali ya kwamba muda ukiisha talaka inatokea.

Ndoa ya mutaa ni aina mojawapo wa ndoa za kijahiliya, nayo ilikuwa halali mwanzoni mwa Uislamu halafu ikaharamishwa tena ni haramu kwa mujibu wa makubaliano ya pamoja ya Maulamaa kwa ujumla; Imamu abu Hanifa, Maliki, Shafii na Hanbali. [Al Mausu'ah Al Fiqhiyah Al Kuwaitiyah 233-334/41

Baadhi ya wapinzani wa ndoa ya Misyaar waliuelekea mtazamo wa Qiyasi kulinganisha baina ya ndoa ya mutaa na ndoa ya Misyaar ili kupata dalili za kisheria za kuharamisha ndoa ya Misyaar, ingawa kuna tofauti kubwa baina ya aina hizo mbili.

Kwani ndoa ya mutaa inakuwa na muda maulumu unaosawazisha ujira au mahari maalumu tena muda huo mara nyingi unaainishwa kwa mujibu wa ujira au mahari tofauti na ndoa ya Misyaar ambayo haiainishiwi muda maalumu tena inakuwa na sifa ya kudumu na inaendelea mpaka itokee talaka.

Halikadhalika mwanamke hapati talaka katika hali ya ndoa ya mutaa lakini anaachana na mumewe wakati wa kuisha muda walioafikiana, hali ya kuwa anapata talaka yake katika ndoa ya Misyaar ikitokea talaka.

Upambanuzi katika tofauti zilizopo kati ya ndoa ya Misyaar na ndoa ya Muhalalishaji

Baadhi ya wapinzani wa ndoa ya Misyaar walielekea kulinganisha baina ya ndoa ya Misyaar na ndoa ya Muhalalishaji ambayo Mtume S.A.W. aliilaani na akamlaani mwenye kuifanya.

Mtazamo huo unajibiwa kwamba. Lengo la mwanamume hapa ni tofauti; maana katika ndoa ya Misyaar mwanamume anakuwa na haja ya kumwoa mwanamke, lakini katika ndoa ya Muhalalishaji, Muhalalishaji anakusudia tendo lake la kumrudisha mwanamke kwa mume wake wa kwanza; katika hali ya ndoa ya Muhalalishaji maana inayotakikana hasa katika ndoa haipatikani.

Lakini ndoa ya Misyaar, maana inayotakikana na ndoa inakuwepo ambapo mwanamume na mwanamke wanaafikiana wawe pamoja, nayo ni ndoa yenye sifa ya kudumu kama kila Muislamu anayekusudia kumwoa mwanamke Muislamu; asili katika ndoa ni nia ya kudumu katika ndoa. [Fatawa Mo'aswerah kwa Sheikh Al Qaradhawiy 298/3]

Kwa ufupi ni kwamba, Misyaar ni ndoa sahihi na inajuzu kisheria ikiwa na nguzo za ndoa na masharti yake yanayotakiwa kisheria, aidha mwanamke akiacha baadhi ya haki zake za kukaa au kupata matumizi ya nyumbani au mojawapo ya hayo ni jambo ambalo halibatilishi mkataba wa ndoa, ingawa mwanamke ana haki ya kuomba baadaye haki yake ya kukaa na kupata matumizi ya nyumbani wakati wowote akitaka, naye mumewe analazimika kulitekeleza ombi lake.

Tena aina hiyo ya ndoa licha ya kuwa ni sahihi ila ikipatikana khofu ya kuwepo madhara au uovu katika jamii kuenezwa – kama kwamba watu waache ndoa ya iliyozoeleka inayokubalika wakaelekea ndoa ya Misyaar – hapo kiongozi anaweza kuizuia kwa sababu hiyo, na hilo linaingia katika mlango wa siasa ya kisheria kama alivyofanya Omar R.A. alipomwamrisha Huzaifa R.A. amwache mke wake myahudi akisema: “ninachelea kuwa mtawaacha wanawake Waislamu  na kuwaoa wanawake ambao hawakutulia”. Ingawa asili katika ndoa hiyo ni sahihi. [Moswanaf Abdulrazaq 176/7]

Naye Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Zaidi.

Imeandikwa na  Mustafa Abdul Karim Muhammad

6/8/2007

Share this:

Related Fatwas