Makazi ya kujitegemea kwa Wanandoa
Question
Je, ni wajibu kwa mume kumpatia mke wake makazi ya kujitegemea mbali na familia yake (ya mume), kama vile nyumba au mfano wake?
Answer
Uislamu umejaalia uhusiano kati ya wanandoa ujengeke juu ya heshima, kuthaminiana, mapenzi, na huruma; Mwenyezi Mungu anasema: "Na katika ishara Zake ni kuwa amekuumbieni wake kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao, na ameweka kati yenu mapenzi na huruma. Hakika katika hayo bila shaka kuna ishara kwa watu wanaofikiri" [Ar-Rum: 21].
Kuhusu mwanamke kumuomba mumewe ampatie makazi ya kujitegemea, hilo ni jambo linalojuzu kisharia, na ni haki miongoni mwa haki za mke kwa mumewe.
Vilevile, mwanamume anapaswa kuwa karibu na wazazi wake katika uzee wao ikiwa wanahitaji huduma yake, kwani huku ni katika kuwafanyia wema wazazi (Birr Al-Walidayn). Hata hivyo, haijuzu kwa mwanamume kumlazimisha mke wake kuwatumikia wazazi wake (mume). Ikiwa mke atafanya hivyo kwa hiari yake (kujitolea), basi atapata ujira na thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na hilo linaonesha ukarimu wa maadili yake na asili yake njema.
Maelezo
Mwenyezi Mungu Ameweka Sharia ya ndoa kwa ajili ya malengo matukufu, miongoni mwayo ikiwa ni kujistiri, kupata watoto, na utulivu). Mwenyezi Mungu anasema: "Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi aliyekuumbeni kutokana na nafsi moja..." [An-Nisaa: 1]. Na kutoka kwa Abdullah bin Mas'ud (R.A). Mtume (S.A.W). amesema: "Enyi vijana! Mwenye kuweza miongoni mwenu kuoa (Al-Ba’ah [1]), basi na aoe..." (Imepokelewa na Muslim).
Uislamu ni dini ya huruma na ihsani kwa viumbe wote wa Mwenyezi Mungu. Kati ya watu wenye haki zaidi ya kufanyiwa huruma na kutendewa wema ni mke; kwani Sharia tukufu imemuhimiza mwanamume kumkirimu mke wake na kumfanyia wema. Mwenyezi Mungu Anasema: "Na kaeni nao kwa wema..." [An-Nisaa: 19]. Hata katika hali ambapo maisha ya pamoja yameshindikana, Sharia imeamuru kutengana kwa njia nzuri: "...basi ni kukaa kwa wema au kuachana kwa ihsani" [Al-Baqarah: 229].
Kuhusu takwa la mke kwa mumewe la kutaka makazi ya kujitegemea mbali na familia ya mume, hukumu yake ni kama ifuatavyo:
Kwanza: Inajuzu kisharia kwa mke kudai makazi ya kujitegemea mbali na familia ya mume; na hiyo ni kwa sababu kadhaa, miongoni mwazo ni: kuweza kusimamia mambo ya nyumba yake bila kuona haya mbele ya mtu, na kupata uhuru wake anaoutaka katika maisha yake ya faragha na ya kifamilia.
Pili: Sharia tukufu imejaalia makazi ya kujitegemea kuwa ni haki miongoni mwa haki za mke; Mwenyezi Mungu anasema katika wasia kuhusu mwanamke aliyeachwa aliye katika eda: "Wawekeni (wanawake mlioachana nao) mnapoishi kwa kadiri ya uwezo wenu, wala msiwadhuru kwa kuwatia dhiki..." [At-Talaq: 6]. Ikiwa Qur`aniTukufu imetoa wasia huu kwa mwanamke aliyeachwa ili mwanamume ampatie makazi yanayofaa wakati wa eda, basi mke aliyeko ndani ya ndoa ana haki zaidi ya kupata makazi ya kujitegemea ili awe na utulivu na uhuru wake.
Tatu: Ikiwa mume hawezi kukaa mbali na wazazi wake kwa sababu ya uzee wao na uhitaji wao wa huduma na uangalizi, basi anapaswa kuwa karibu nao katika makazi ili awatumikie yeye mwenyewe; na hilo ni bora zaidi kwa sababu kuwafanyia wema wazazi ni miongoni mwa amali kuu mbele ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu anasema: "Na Mola wako Mlezi amehukumu kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema..." [Al-Isra: 23-24].
Nne: Haijuzu kwa mume kumlazimisha mke wake kuwatumikia wazazi wake (mume), bali anapaswa kumuomba amsaidie katika hilo kwa upole na utulivu. Ikiwa mke atafanya hivyo, basi huo ni ukarimu, maadili mema, na asili yake nzuri.
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
Uislamu umejenga uhusiano kati ya mume na mke juu ya heshima, kuthaminiana, mapenzi, na huruma; Mwenyezi Mungu anasema: "Na katika ishara Zake ni kuwa amekuumbieni wake kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao, na ameweka kati yenu mapenzi na huruma. Hakika katika hayo bila shaka kuna ishara kwa watu wanaofikiri" [Ar-Rum: 21].
Mke kumuomba mumewe makazi ya kujitegemea ni jambo linalojuzu kisharia na ni haki yake kisharia.
Mwanamume anapaswa kuwa karibu na wazazi wake wanapokuwa wazee ikiwa wanahitaji huduma, lakini haruhusiwi kumlazimisha mkewe kuwatumikia. Akijitolea kufanya hivyo (mke), atapata thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu na huo ni ukarimu, maadili mema, na asili yake nzuri
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
