Hukumu ya mwanamke na mwanamume kushikana mkono
Question
Ni ipi hukumu ya mwanamke na mwanamume kushikana mkono? Na je, wakifanya hivyo udhuu huvunjwa?
Answer
Kusalimiana kwa kupeana mikono wakati wa kukutana ni jambo linalopendekezwa kisharia ambalo Sharia tukufu imelihimiza. Ama kuhusu mwanamume kupeana mkono na wanawake miongoni mwa maharimu wake (ndugu wa karibu), ni jambo linalojuzu kisharia na halivunji udhu kwa makubaliano ya mafaqihi.
Ama kuhusu mwanamume kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu wake, msimamo wenye nguvu kwa Wanazuoni na ndio unaotolewa Fatwa, ni kujuzu kwa jambo hilo kisharia kwa yule aliyefikwa na hali hiyo; hivyo anaruhusiwa kupeana mkono bila ya matamanio ili asiingie katika fitna, na haisihi wakati huo kwa yeyote kumkataza.
Maelezo
Inafahamika kuwa dini tukufu ya Kiislamu ni dini ya rehema na amani, bali Sharia tukufu imejalia salamu ya Waislamu miongoni mwao kuwa ni neno la "Amani" (Al-Salam). Kutoka kwa Abu Huraira (R.A.), kutoka kwa Mtume (S.A.W.) amesema: “Mwenyezi Mungu alimuumba Adam kwa sura yake, urefu wake ukiwa dhiraa sitini. Alipomuumba akasema: Nenda ukawasalimie kundi lile la Malaika waliokaa, kisha sikiliza namna watakavyokusalamia, kwani hiyo ndiyo salamu yako na salamu ya jamaa zako. Akasema: Assalaamu Alikum. Wakasema: Assalaamu Alika wa Rahmatullah; wakamzidishia: "wa Rahmatullah". Basi kila atakayeingia Peponi atakuwa katika sura ya Adam, na viumbe havikuacha kupungua (urefu) tangu wakati huo mpaka sasa” [Imepokelewa na Al-Bukhari].
Na Muislamu kutoa salamu kwa kila anayekutana naye, awe anamjua au hamjui, ni jambo linalopendekezwa kisharia. Kutoka kwa Abdullah bin Amr (R.A.): “Kwamba mtu mmoja alimuuliza Mtume (S.A.W.): Ni Uislamu upi ulio bora[1]? Akasema: Kulisha chakula, na kutoa salamu[2] kwa unayemjua na usiyemjua” [Imepokelewa na Al-Bukhari].
Kueneza salamu kati ya watu hupelekea mapenzi na urafiki. Kutoka kwa Abu Huraira (R.A.) amesema: Mtume (S.A.W.) amesema: “Hamtaingia Peponi mpaka muamini, wala hamtaamini mpaka mpendane. Je, nisiwaoneshe kitu ambacho mkishafanya mtapendana? Enezeni salamu miongoni mwenu” [Imepokelewa na Muslim]. Hadithi hii inaonesha kupendekezwa kwa kueneza salamu na kuitoa kwa watu wote.
Ama kuhusu kushikana mikono wakati wa kutoa salamu, hukumu yake ni kama ifuatavyo:
Kwanza: Inapendekezwa kisharia kushikana mikono kati ya Waislamu kwa mkono wa kulia wakati wa kukutana na kutoa salamu. Wanachuoni wa wamekubaliana juu ya kujuzu kwa mwanamume kuwapa mkono wanaume wenzake, na mwanamke kuwapa mkono wanawake wenzake. Kutoka kwa Al-Baraa bin Aazib (R.A.) amesema: Mtume (S.A.W.) amesema: “Hapana Waislamu wawili wanaokutana, wakashikana mikono, isipokuwa husamehewa madhambi yao kabla ya kuachana” [Imepokelewa na Abu Dawood]. Na kutoka kwa Qatada amesema: Nilimwambia Anas bin Malik (R.A.): “Je, kulikuwa na kushikana mikono miongoni mwa Maswahaba wa Mtume (S.A.W.)? Anas akasema: Ndiyo” [Imepokelewa na Al-Bukhari].
Pili: Mwanamume kushikana mikono na wanawake miongoni mwa maharimu wake ni jambo linalojuzu kisharia na halina kizuizi kwa makubaliano ya Wanazuoni wa Fiqhi.
Tatu: Mwanamume kushikana mikono na mwanamke asiye maharimu wake[3] ni jambo ambalo Wanazuoni wa Fiqhi wametofautiana, na hiyo ni kama ifuatavyo:
1- Kundi moja la Wanazuoni wa Fiqhi linaona kuwa haijuzu kwa mwanamume kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu wake. Ushahidi wao katika hilo ni Hadithi ya Bibi Aisha (R.A.) aliyesema: “Mkono wa Mtume (S.A.W.) haujawahi kugusa mkono wa mwanamke yeyote kabisa” [Imepokelewa na Al-Bukhari], na hadithi ya Ma'qil bin Yasar (R.A.) kwamba Mtume (S.A.W.) amesema: “Kuchomwa katika kichwa cha mwanamume kwa sindano ya chuma ni bora kwake kuliko kumgusa mwanamke asiyemhalalikia”[4].
2- Kundi jingine la wataalamu wa Fiqhi linaona kuwa inajuzu kwa mwanamume kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu wake kwa sharti la usalama dhidi ya fitna, kama vile kupeana mkono na mwanamke mzee asiyetamaniwa. Kundi hili linalojuzisha limejibu ushahidi wa kundi la kwanza kama ifuatavyo:
Kwanza: Kuhusu Hadithi ya Bibi Aisha (R.A.) inayoonyesha kujizuia kwa Mtume (S.A.W.) kupeana mikono na wanawake walipohudhuria kumpa kiapo (bay'ah); Umar bin Al-Khattab (R.A.) alipeana nao mikono kwa niaba yake na Mtume (S.A.W.) hakumkataza. Hii inaonesha kuwa kuacha kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu ni katika mambo maalumu ya Mtume (S.A.W.) pekee.
Pili: Imethibiti katika Sunna yale yanayoonyesha kuwa kumgusa mwanamke asiye maharimu ni jambo linalojuzu ikiwa kuna usalama dhidi ya fitna; kutoka kwa Anas bin Malik (R.A) amesema: “Mtume (S.A.W.) alikuwa akiingia kwa Ummu Haram bint Milhan, naye alikuwa chini ya Ubada bin Al-Samit. Siku moja aliingia kwake, akamlisha chakula, na akaanza kumtafuta chawa kichwani mwake” [Imepokelewa na Al-Bukhari].
Tatu: Kuhusu Hadithi ya Ma'qil bin Yasar (R.A), haisihi kuitolea hoja kwa pande mbili:
Upande wa kwanza: Ni Hadithi dhaifu, kama walivyosema Wanazuoni wa Hadithi.
Upande wa pili: Inaweza kubeba maana ya kupeana mkono kwa matamanio inayopelekea kuingia katika fitna.
Msimamo wenye nguvu na ule unaofuatwa na Ofisi ya kutoa Fatwa ya Misri ni msimamo wa pili unaojuzisha mwanamume kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu kwa sharti la usalama dhidi ya fitna; na hiyo ni kwa sababu zifuatazo:
Kwanza: Imethibiti kuwa Mtume (S.A.W.) aliwagusa baadhi ya wanawake wasio maharimu wake, na pia imepokelewa kutoka kwa baadhi ya Maswahaba wakipeana mikono na wanawake na hapakuwa na yeyote aliyewakataza.
Pili: Ushahidi uliotolewa na wanaoharamisha haukukosa majibu na mapitio ya kiuchambuzi.
Tatu: Sharia ya Kiislamu imejengwa juu ya wepesi na kuondoa uzito; hivyo basi, yule aliyefikwa na hali ya kupeana mikono na wanawake wasio maharimu katika baadhi ya mazingira, anaruhusiwa kufuata msimamo wa wanazuoni waliojuzisha.
Kuhusu suala la kuvunjika kwa udhu ikiwa mwanamume atapeana mkono na mwanamke asiye maharimu, Wanazuoni wa Fiqhi wametofautiana kama ifuatavyo:
Kundi moja la Wanazuoni linaona kuwa kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu kunavunja udhu, iwe ni mguso wa matamanio au bila matamanio.
Kundi jingine linaona kuwa kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu hakuvunji udhu, iwe ni mguso wa matamanio au bila matamanio.
Kundi la tatu linaona kuwa suala hili lina pande mbili:
Kwanza: Ikiwa kupeana mkono ni bila matamanio, hukumu yake ni kwamba hakuvunji udhu.
Pili: Ikiwa kupeana mkono ni kwa matamanio, hukumu yake ni kwamba kunavunja udhu.
Msimamo wenye nguvu katika suala hili ni kwamba yule aliyefikwa na jambo hilo anaweza kufuata msimamo unaomnasibu miongoni mwa maoni hayo, na haisihi kwa yeyote kumkataza; kwa sababu kanuni ya kisharia inaamua kuwa: «Kinachokatazwa ni kile kilichokubaliwa na wote (kuwa ni haramu), na hakikatazwi kile mlichotofautiana», na kwamba «Kujiepusha na hitilafu kunapendekezwa».
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
1- Kusalimiana kwa kupeana mikono wakati wa kukutana ni jambo linalopendekezwa kisharia ambalo Sharia tukufu imelihimiza.
2- Mwanamume kushikana mikono na wanawake miongoni mwa maharimu wake ni jambo linalojuzu kisharia na halivunji udhu kwa makubaliano ya wanazuoni wa Fiqhi.
3- Msimamo wenye nguvu kuhusu mwanamume kupeana mkono na mwanamke asiye maharimu wake ni kujuzu kwa yule aliyefikwa na hali hiyo; hivyo anaruhusiwa kupeana mkono bila ya matamanio ili asiingie katika fitna, na haisihi wakati huo kwa yeyote kumkataza.
[1] «Ni Uislamu upi ulio bora»: Yaani matendo gani ya Kiislamu yenye manufaa zaidi na thawabu nyingi.
[2] «Kutoa salamu»: Kuwasalimia watu.
[3] «Mwanamke asiye maharimu (Ajnabiyyah)»: Yaani si miongoni mwa maharimu wa mwanamume. Na maharimu wa mwanamume ni: Mke, na kila mwanamke ambaye ni haramu kumuoa daima; kama mama, dada, shangazi, kike na mfano wake.
[4] Imepokelewa na Al-Tabarani katika «Al-Mu'jam Al-Kabir» (20/ 212).
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
