Swala ya Mgonjwa wa Figo (Kidney Fa...

Egypt's Dar Al-Ifta

Swala ya Mgonjwa wa Figo (Kidney Failure)

Question

Mgonjwa wa figo anayefanyiwa usafishaji wa damu (dialysis), je aswali akiwa kitandani hata kama si kuelekea Qibla, au asubiri mpaka amalize matibabu?

Answer

Mgonjwa wa figo anayefanyiwa usafishaji wa damu (dialysis) na muda wa Swala ukaingia wakati wa matibabu, basi akiwa anaweza kuelekea Qibla kwa juhudi zake mwenyewe au kwa msaada wa mtu mwingine, lazima afanye hivyo na aswali, lakini ikiwa ni vigumu kwake kugeuka kuelekea Qibla kwa sababu ya vifaa vya tiba au udhaifu wa mwili wake, anaweza kuswali katika hali aliyo nayo, hata kama si kuelekea Qibla, na hatalazimika kurudia Swala. Hili ndilo pendekezo la wafuasi wa Madhehebu ya Imamu Hanafi na Hanbali. Pia, ana ruhusa kukusanya kati ya Swala mbili: Kukusanyaʿ halisi (jamu`uʿ ḥaqīqī), kama wanavyosema Wanazuoni wa Imamu Hanbali na baadhi ya Shafi, yaani kuziunganisha Swala mbili kwa wakati mmoja. Au Jamu`uʿ mfano (jamu`uʿ ṣūrī), kama wanavyosema Wanazuoni wa Maliki, yaani kuswali ya kwanza mwishoni mwa wakati wake na ya pili mwanzoni mwa wakati wake.

Maelezo

Kuelekea Qibla wakati wa kuswali ni jambo la lazima na amri ya kisharia, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Basi elekeza uso wako upande wa Msikiti Mtakatifu; na popote mlipo elekezeni nyuso zenu upande huo} [Surat Al-Baqara: 144] Pia imesimuliwa na Abu Huraira (R.A.) kwamba Mtume (S.A.W.) alimfundisha mtu aliyekuwa akiharibu Swala yake akisema: "Ukisimama kwa ajili ya Swala, kamilisha udhu wako, kisha elekea Qibla na useme ‘Allahu Akbar’” (Wamekubaliana Al-Bukhari na Muslim)

Wanazuoni wa Fiqhi wote wamekubaliana kwamba kuelekea Qibla ni sharti la usahihi wa Swala. Hata hivyo, wamesema kwamba sharti hili linaondoka ikiwa mtu amezuiliwa kulielekea kwa sababu ya ugonjwa au udhuru mwingine, kwa maelezo na tofauti fulani katika Madhehebu kuhusu masharti na iwapo inampasa kurudia Swala baada ya kupona au la.

Madhehebu ya Hanafi na Hanbali yanasema: Mtu anayeshindwa kuelekea Qibla na hana wa kumgeuza, au kugeuzwa kunamdhuru, basi anafutwa wajibu wa kuelekea Qibla na anaswali kwa hali aliyo nayo, na hatapaswa kurudia Swala baada ya kupona.

Hii ni kwa sababu kuelekea Qibla ni sharti la ziada ambalo huondoka pale inapokuwa haiwezekani kutekelezwa. Lakini kama ana mtu wa kumsaidia kumgeuza kuelekea Qibla, anapaswa kumwomba msaada huo; na kama hakufanya hivyo akaswali bila kuelekea Qibla, basi Swala yake itahesabika kuwa sahihi kwa mujibu wa Imamu Abu Hanifa, lakini si sahihi kwa mujibu wa Muhammad na Abu Yusuf (wanafunzi wake wawili).

Madhehebu ya Maliki na Shafi yameona kuwa: Mtu anayeshindwa kuelekea Qibla na hana wa kumsaidia hata kwa malipo, basi ataswali kwa hali aliyo nayo, lakini ni lazima arudie Swala baada ya kupona au kupata uwezo wa kuelekea Qibla.

Wafuasi wa Madhehebu ya Maliki wameweka sharti kwamba arudie Swala ndani ya wakati wake ikiwa uwezo wa kuelekea Qibla umepatikana kabla ya muda wa swala kuisha au amepata msaada wa kumgeuza.[1]

Kuhusu mgonjwa anayepata ugumu kuswali kwa wakati wake, baadhi ya Wanazuoni wa Shafi na Hanbali wameruhusu kuunganisha Swala mbili (jamu`uʿ) kwa sababu ya ugonjwa, wakitegemea maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Mwenyezi Mungu anataka kukupeni wepesi wala hataki kukutieni katika uzito} [Al-Baqara: 185],

{Mwenyezi Mungu hataki kukuwekeeni taabu katika dini} [Al-Ma’ida: 6]. Kutokana na aya hizi, wanazuoni wote wamekubaliana juu ya kanuni ya kisheria: “Mashaka huleta wepesi.” Na kwa kuwa Uislamu umehalalisha kuunganisha Swala kwa sababu ya mvua au safari ili kuondoa uzito, basi kuiruhusu wakati wa ugonjwa ni muhimu zaidi; kwani hali ya ugonjwa humpunguzia mtu nguvu na humzuia kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Wafuasi wa Madhehebu ya Maliki wameruhusu pia jamʿ wa mfano (jamu`uʿ ṣūrī), yaani: Kuswali Swala ya kwanza mwishoni mwa wakati wake, na Swala ya pili mwanzoni mwa wakati wake, ili kuepuka tofauti za kifiqhi kuhusu uhalali wa kuunganisha Swala kwa sababu ya ugonjwa.

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Mgonjwa wa figo (anayefanyiwa usafishaji wa damu – dialysis), endapo muda wa Swala utaingia wakati wa matibabu, basi: ikiwa anaweza kuelekea Qibla kwa juhudi zake mwenyewe au kwa msaada wa mtu mwingine, anapaswa kuelekea Qibla na kuswali.

Ikiwa kuelekea Qibla ni jambo gumu kwake, basi anaweza kuswali katika hali aliyo nayo, hata kama si kuelekea Qibla, na hatapaswa kurudia Swala hiyo, kama walivyosema wanazuoni wa Madhehebu ya Imamu Hanafi na Hanbali. Anaweza pia kuunganisha Swala mbili, kwa jamʿ halisi (jamu`uʿ ḥaqīqī) kama walivyosema Wanazuoni wa Imamu Hanbali na baadhi ya Shafi, au kwa jamu`uuʿ wa mfano (jamʿ ṣūrī) kama walivyosema Wanazuoni wa Maliki.

[1] “Badā’i‘ as-Sanā’i‘” (Juzuu ya 1, uk. 118, toleo la Dār al-Kutub al-‘Ilmiyyah),“Al-Muḥīṭ al-Burhānī fī al-Fiqh an-Nu‘mānī” (Juzuu ya 2, uk. 148, toleo la Dār al-Kutub al-‘Ilmiyyah), “Al-Inṣāf” (Juzuu ya 2, uk. 3, toleo la Dār Iḥyā’ at-Turāth al-‘Arabī), “Sharḥ at-Talqīn” (Juzuu ya 1, uk. 867, toleo la Dār al-Gharb al-Islāmī), “Al-Majmū‘” (Juzuu ya 3, uk. 243, toleo la Dār al-Fikr).

Share this:

Related Fatwas