Swala ya Iddi kwa aliyeshindwa kuis...

Egypt's Dar Al-Ifta

Swala ya Iddi kwa aliyeshindwa kuisali

Question

Mimi ni mwanaume ambaye usingizi wangu ni mzito, na nimekosa Swala ya Iddi kwa sababu ya hilo. Nimehuzunika sana kwa jambo hilo. Je, inajuzu kwangu kuilipa (kadhaa) Swala ya Iddi baada ya wakati wake kupita, au haiswaliwi tena?

Answer

Kama muda wa kuswali Swala ya Iddi ukiisha na mtu akakosa kuiswali pamoja na jamaa, basi inajuzu kuirudia (kuiswali peke yake) kwa mujibu wa kauli iliyo sahihi zaidi kwa ajili ya Fatwa, kwa kuwa Swala ya Iddi ni kama Swala nyinginezo — inaweza kuswaliwa na mtu binafsi endapo atakuwa ameikosa na jamaa.

Maelezo

 

Mwenyezi Mungu Mtukufu amefaradhisha Swala za Iddi mbili — Iddi ya Fitr na Iddi ya Adh-ha — ili ziwe ni ishara ya furaha na shukrani kwa ibada kuu mbili zilizotangulia: Saumu (kwa Iddi ya Fitr) na Hijja (kwa Iddi ya Adh-ha).
Pia ni njia ya kuwakusanya Waislamu wote katika siku hizi mbili za furaha, wakisherehekea kwa pamoja matunda ya utiifu wao kwa Mwenyezi Mungu. Imepokewa kutoka kwa Anas bin Malik (R.A.) kwamba alisema: “Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.) alifika Madina, na watu walikuwa na siku mbili ambazo walikuwa wakicheza na kujifurahisha ndani yake. Mtume (S.A.W.) akawauliza: ‘Ni siku gani hizi mbili?’ Wakasema: ‘Ni siku mbili ambazo tulikuwa tukicheza katika zama za ujinga (jahiliyyah).’ Mtume (S.A.W.) akasema:‘Hakika Mwenyezi Mungu amewabadilishia hizo kwa bora zaidi: Siku ya Adh-ha na Siku ya Fitr.’” (Imepokewa na Imamu Ahmad katika Musnad, na Al-Hakim katika Al-Mustadrak, naye akaisahihisha hadithi hii).

Kwa kuwa siku ya Iddi ni siku ya furaha na shukrani. Mwenyezi Mungu anasema: {Na ili mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa kuwa amewaongoza, na ili mpate kushukuru} [Surat Al-Baqarah: 185]

Swala ya Iddi ni Sunnah iliyosisitizwa (Sunna Muakkadah) kwa mujibu wa wanazuoni wengi — wakiwemo Maalikiy, Shafi’iy, Hanafiy (katika kauli moja), na Imamu Ahmad (katika riwaya moja).

Wanazuoni wa Fiqhi wametofautiana kuhusu hukumu ile, ambapo Jumhuri (Maliki, Shafi na Hanbali) wanasema kuwa ni Sunna kuilipa Swala ya Iddi ikiwa imepita, ila Maliki wamesema inafaa tu kabla ya jua kupinduka (kabla ya Adhuhuri) Wahanafi na Imamu Shafi katika kauli nyingine wamesema kuwa Swala ya Iddi hairejelewi (haifanywi tena) baada ya wakati wake kuisha na kundi la waumini kuondoka.

Wakati huo huo, wanazuoni wa Madhehebu ya Hanafi na Imamu Shafi katika kauli moja wamesema kwamba Swala ya Iddi hairejelewi (haifanywi tena) ikiwa mtu ameikosa na wakati wa kuiswali pamoja na jamaa umeshapita, Ibn Taymiyya, miongoni mwa wanazuoni wa Madhehebu ya Hanbali, aliunga mkono kauli ya kutokuwa nafasi ya kuilipa.[1]

Hayo ni kwa kuwa Swala ya Iddi mbili – Iddi ya Fitr na Iddi ya Adh-ha – ilijulikana kuwa ni ibada ya karibu kwa Mwenyezi Mungu kupitia matendo ya Mtume (S.A.W.), na Mtume hakuiswali isipokuwa kwa jamaa, kama ilivyo kwa Swala ya Ijumaa. Kwa hiyo, wamesema kuwa haiwezi kuswaliwa peke yake, kwa sababu ni ibada yenye masharti maalumu ambayo hayawezi kutimia katika hali ya kuirudia; hivyo hairejelewi, kama ilivyo kwa Swala ya Ijumaa.

Hata hivyo, kauli iliyo bora zaidi kwa Fatwa ni kwamba Swala ya Iddi inaweza kuswaliwa tena pale mtu anapokosa Swala ya Iddi pamoja na jamaa, kwa kuwa inachukuliwa kama Swala nyingine yeyote. Hili linategemea Hadithi ya Anas bin Malik (R.A.) kwamba Mtume (S.A.W.) alisema: “Atakayelala akakosa Swala au akaisahau, basi aiswali mara tu atakapoikumbuka.” kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: {Na usimamishe swala kwa ajili ya kunikumbuka Mimi.} [Surat Taha, aya ya 14]. (Riwaya ni ya Bukhari na Muslim, maneno ni ya Muslim peke yake).

Na imepokelewa kutoka kwa ‘Ubaydullah bin Abi Bakr bin Anas bin Malik, mtumishi wa Mtume (S.A.W.), amesema: “Anas alikuwa akikusanya watu wa nyumbani kwake na kuwaswalisha kama Swala ya Iddi ya Imamu pale alipokosa Swala ya Iddi pamoja na jamaa.” (Imepokewa na Al-Bayhaqiy katika As-Sunan Al-Kubra na Al-Bukhari kwa muhtasari). Imamu Al-Bukhari pia alieleza mlango huu akasema: “Anayekosa Swala ya Iddi, aswali rakaa mbili; vivyo hivyo wanawake na wale walio nyumbani au vijijini, kwa kuwa Mtume (S.A.W.) alisema: ‘Huu ni Iddi yetu sisi Waislamu” Anas bin Malik alimwamuru mtumwa wake Ibn Abi ‘Utbah akiwa katika eneo la Az-Zawiya awakusanye watu wa nyumbani kwake na watoto wake, kisha akaswali nao kama wanavyoswali watu wa mji, pamoja na takbira zao. Aidha, ‘Ikrima alisema: “Watu wa vijijini hujumuika siku ya Iddi na kuswali rakaa mbili kama anavyofanya imamu.” Na ‘Ata alisema: “Anayekosa Swala ya Iddi na aiswali rakaa mbili.”

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Si tatizo mtu kuswali Swala ya Iddi kwa nia ya kuilipa pale inapomkosa, kwa mujibu wa kauli ya Wanazuoni walioruhusu kufanya hivyo. Lakini asipoiswali tena, hana dhambi wala lawama.

 

[1] “Adh-Dhakhīrah” (Juzuu ya 2, uk. 424, toleo la Dār al-Gharb al-Islāmī), “Nihāyat al-Muḥtāj” (Juzuu ya 2, uk. 390, toleo la Dār al-Fikr),“Al-Mabsūṭ” (Juzuu ya 1, uk. 119, toleo la Dār al-Ma‘rifah), “Al-Fatāwā al-Kubrā”  Juzuu ya 5, uk. 356, toleo la Dār al-Kutub al-‘Ilmiyyah).

Share this:

Related Fatwas