Kukopa Benki katika Nchi Zisizo za ...

Egypt's Dar Al-Ifta

Kukopa Benki katika Nchi Zisizo za Waislamu

Question

Nini hukumu ya Sheria ya kiislamu ya kukopa Benki kwa riba katika nchi zisizo za Waislamu, pamoja na kuwepo haja ya dharura? 

Answer

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na rehma na amani zimwendee bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, masahaba wake na wanaomfuata. Na baada ya hayo:
Mtendeano usio sahihi kama vile kuuza pombe na riba na wasio waislamu katika nchi zisizo za waislamu ni miongoni mwa masuala ya tangu zamani ambayo wanachuoni waliyazungumzia, na kutokana na rai iliyochaguliwa na wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy naweza kusema:
Maimamu wawili Abu-Hanifa na Muhammad, kinyume ya Abi-Yusuf, walielekea kuwa: Hakuna riba kati ya mwislamu na asiye mwislamu katika mji usio wa waislamu, na kuwa mwislamu katika mji huu ana haki ya kuchukua mali zao kwa njia yeyote iwayo, hata kwa njia ya matendeano yasiyo sahihi kama vile kamari, kuuza nyamafu na pombe, na riba n.k., muda wa kuwa ni kwa maridhiano yao. Imamu Muhammad anasema: “Mwislamu akiingia mji wa vita kwa ahadi ya amani, hakuna kosa kuchukua mali zao kwa maridhiano ya nafsi zao kwa njia yeyote iwayo”. [Sharh as-siyar Al-kabiir, 4/141].
Nasema kuwa: Imamu Muhammad na wengineo waliita nchi zisizo za waislamu kuwa ni mji wa vita kutokana na mgawanyo uliokuwepo katika zama za maimamu ambao tunanukuu kutoka kwao hukumu hii, ambapo ulimwengu wote ulikuwa ukipambana na waislamu, hivyo wanachuoni waligawanya nchi zote kuwa aina mbili: Mji wa waislamu ambapo unasimamishwa uislamu na maamrisho yake, na mji wa vita ambapo hukumu za waislamu hazitekelezwi.
Lakini mgawanyo wa kisasa wa wanachuoni wa Uislamu baada ya hali ya vita vilivyochochewa dhidi ya waislamu baada ya kumalizika ni nchi za waislamu na nchi zisizo za waislamu, na hukumu zake ni zilezile za mji wa vita, isipokuwa mambo yanayohusu vita vyenyewe, ambapo havipo kwa sasa na shukrani zote ni za Mwenyezi Mungu.
Na lazima tuzingatie hivi, kwa sababu tunanukulu kutoka vitabu vya zamani kwa ajili ya kubainisha madhehebu ya Hanafiy, hivyo tuzingatie maana ya maneno yao: Maana ya mji wa vita kwa wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy nchi zisizo za waislamu, ni sawa pawepo vita au la, na dalili yake kuwa hoja zao nyingi zilihusiana na mji wa ukafiri bila ya kuwepo vita, yaani wanakusudia Makkah kabla ya Al-Hijrah, kama itakavyokuja, na haukuwepo mji wa vita ulimwenguni kote, na lengo la dalili ni kushirikiana na uwajibikaji wa hukumu kwa pamoja.
Kisha Imamu Muhammad, Mwenyezi Mungu amrehemu, alisema kuwa: “Mwislamu katika mji wa vita akiuzia makafiri Dirham moja kwa Dirham mbili kwa muda wa mwaka mmoja, kisha akatoka kwenda mji wetu, akarudi tena, au akatoka muda wa mwaka, kisha akarudi kwao akachukua Dirham baada ya ukapita mwaka , basi hakuna kosa”. [Sharh As-siyar Al-Kabiir, 4/148].
Al-Sarkhasiy, baada ya kutaja Hadithi Mursal ya Makuhuul anasema: “Hakuna riba kati ya waislamu na watu wa mji wa vita katika mji wa vita, na kuhusu Hadithi Mursal ya Makuhuul ni dalili kwa Abi-Hnifa na Muhammad, Mwenyezi mungu awarehemu, kuwa inajuzu kwa mwislamu kumwuzia kafiri dirham moja kwa dirham mbili katika mji wa vita, vile vile akiwauzia nyamafu au akacheza kamari nao, na akachukua mali zao kwa njia hiyo, na mali hii ni halali, kwa mtazamo wa Abi-Hanifa na Muhammad, Mwenyezi Mungu awarehemu”, [Al-Mabsuut14/56].
Na kauli za Maimamu wawili Abi-Hanifa na Muhammad ndiyo inayotegemewa na kuchaguliwa na wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy.
Imamu As-Sarkhsiy baada ya matini yake iliyotangulia anasema: “Hoja ya wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy ni Hadithi iliyopokelewa na Ibn Abbas R.A na wengineo kuwa Mtume S.A.W alisema katika hotuba yake: “Kila riba iliyokuwa katika wakati wa ujahili sasa imetenguliwa, na riba ya kwanza kutenguliwa ni riba ya Al-Abbas ibn Abdul-Muttalib”, hivyo kwa sababu Al-Abbas R.A baada ya kusilimu, akarejea Makkah na alikuwa anakula riba, na tendo lake hili halifichiki kwa Mtume S.A.W, na Mtume S.A.W hakumkataza, na hii ni dalili ya kujuzu. Kuhusu riba iliyotenguliwa nayo ni riba ambayo haikudhibitiwa hadi wakati wa kufungua Makkah na ikawa mji wa Uislamu. [Al-Mabsuut, 14/56].
Al-Mirghinaniy na Al-Kamal ibn Al-Humam na Al-Haskafiyna ibn Abidiin wote wanasema: “Hakuna riba kati ya waislamu na kafiri katika mji wa vita, wakataja pia kuwa mwislamu katika mji wa vita ana haki ya kuchukua mali ya makafiri kwa njia yeyote, lakini bila ya hadaa kwa upande wake”, kwa sababu hadaa ni haramu. [Tazama.: Al-Hidayah na Sahrhe yake Al-Binayah, 7/384-385; Fathul-kadiir 6/177; Addurrul-Mukhtat na Hashiyat Ibn Abidiin, 4/188].
Udhahiri wa maneno ya wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy kuwa hukumu ni kwa ujumla kwa mwislamu katika kutendeana na riba katika mji wa vita, lakini Al-Kamal ibn Al-Humam alitaja kuwa Maimamu wa madhehebu ya Hanafiy katika masomo yao waliweka sharti la uhalali wa riba kwa mwislamu katika mji wa vita kuwa mwislamu aipate kutoka kwa kafiri, kwa hiyo anasema: “Haifichiki kuwa uhalali wa kufunga mkataba yaani wa riba ikiwa mwislamu ataipata ziada, hata hivyo riba ni pana kuliko hivi ilivyo kwa sababu inakusanya kuwa dirham moja kwa dirham mbili na pande mbili kafiri au mwislamu, na hukumu yake ni halali kwa kila njia, vile vile kamari huenda ziada ndani yake itakuwa kwa kafiri hali ya kushinda, kwa hiyo uhalali wake hali ya mwislamu apate ziada.
Wanachuoni waliamua katika masomo yao kuwa makusudio yao ya kuhalalisha riba na kamari ikiwa ziada ya kupata mwislamu kwa mujibu wa sababu yake, ingawa hukumu kwa jumla ni uhalali kinyume cha maoni yao, na mfano huu umenukuliwa na Ibn Abidiin. [Tazama.: Fathul-Qadiir, 6/178; Hashiyat Ibn Abidiin, 4/188].
Inawezekana kutegemea kwa udhahiri wa madhehebu ikiwa masilahi ya mwisho itakuwa kwa mwislamu hata atalipa ziada, wanachuoni wa madhehebu ya Hanafiy walitoa dalili ya maoni yao kama ifuatavyo:
1- Kama Ilivyopokelewa katika Hadithi ya Makuhuul kutoka kwa Mtume S.A.W: “Hakuna riba kati ya waislamu na watu wa mji wa vita katika mji wa vita”, As-Sarkhasiy anasema katika kitabu cha Al-Mabsuut [14/56]: “Ikiwa Hadithi hii ni Mursal, basi Makuhuul ni mjuzi na mwaminifu, na Hadithi Mursal kwa upande wake ni kukubaliwa”, na dalili hiyo ilitumiwa na Al-Mighinaniy na Al-Kamal ibn Al-Humam, [Tazama.: Fath Al-Qadiir, 6/178].
2- Imamu Muhammad , Mwenyezi Mungu amrehemu, alitoa dalili ya Hadithi ya Bani-Qainuqaa’, ambapo Mtume S.A.W aliwahamisha, walisema: “Tuna madeni na bado hatujapokea”, akasema: “Zichukueni upesi au ziacheni”, na ambapo aliwahamisha Bani-Nadhiir walisema: “Tuna madeni kwa watu”, akasema: “Ziacheni au zichukueni upesi”, As-Sarkhasiy alibainisha maana ya dalili kuwa: “Inajulikana kuwa matendeano kama hayo, yaani Riba, iliyopo katika kauli yake Mtume S.A.W: “Acheni au pokeeni upesi” hayajuzu kati ya waislamu, kwa sababu mwenye deni kwa mwingine kwa muda maalum haijuzu kuiacha sharti apokee baadhi yake upesi, kwa kuwa Umar, zaid ibn Thabit na Ibn Umar R.A walichukia hivi, lakini Mtume S.A.W aliruhusu kwa mayahudi kwa sababu wao ni watu wa vita katika wakati huo, kwa hiyo aliwahamisha, hivyo tulijua kuwa inavyojuzu kati ya kafiri na mwislamu haijuzu kati ya waislamu wenyewe kwa wenyewe”. [Sharh As-Siyar Al-Kabiir, 4/141].
3- Na ilivyotokea katika kupigana mieleka kwa Mtume S.A.W na Rukanah alipokuwa katika Makkah, na Mtume S.A.W alimshinda, kila mara kwa theluthi ya kondoo wake, na lau tendo hilo ni la kukatazwa basi Mtume S.A.W asingefanya, na Mtume alipomshinda kwa mara ya tatu Rukanah alisema: “Hakuna yeyote aliyeweza kunishinda na hata wewe hukuweza”, lakini Mtume S.A.W alimrudishia kondoo wake. As-Sarkhasi anasema: “ Hakika Mtume S.A.W alirudishia kondoo kwa njia ya kufadhili, na Mtume S.A.W alifanya hivi siku zote na washirikina ili awapendezeshe na kuwavutia ili waingie Uislamu”. [Sharh As-Siyar Al-Kabiir, 4/141]], na haifichiki kuwa Makkah katika wakati huo haukuwa mji wa vita bali ulikuwa mji wa ukafiri.
4- Na Hadithi aliyoisema Mtume S.A.W na ile iliyopokelewa na Ibn Abbas R.A na wengineo kuwa Mtume S.A.W alisema: “Hakika kila kitu cha mambo ya ujahili kimetenguliwa na kimo chini ya miguu yangu miwili, na Riba ya ujahili ni ya kutenguliwa, na riba ya kwanza ninayo itengua ni Riba ya Al-Abbas in Abdul-muttalib nayo ndiyo ya kutenguliwa kwa jumla”.
Upande wa dalili katika Hadithi hii kuwa: Al-Abbas R.A baada ya kusilimu baada ya kuletwa mateka katika vita vya Badr, alitaka ruhusa kwa Mtume S.A.W arejee Makkah baada ya kusilimu, na Mtume akamruhusu, na Al-Abbas alikuwa anakula riba katika Makkah mpaka wakati wa kuifungua (Makkah), na tendo lake hili halifichiki kwa Mtume S.A.W, na kwa kuwa Mtume hakumkataza basi ni dalili ya kujuzu, hivyo riba iliyotenguliwa katika mji wa vita ni ile haikuchukuliwa mpaka wakati wa kuifungua Makkah, na ukawa mji wa Uislamu, kwa hiyo Mtume S.A.W alitengua Riba wakati wa Kufungua Makkah. [Sharh As-Siyar Al-Kabiir, 4/148; Al-Mabsuut, 14/75].
5- Kwa kuwa Abu-Bakr R.A alicheza kamari na washirikina wa Quraish kabla ya Al-Hijrah wakati Mwenyezi Mungu alipoteremsha kauli yake: {Alif Lam Mym. Warumi wameshindwa}. [AR RUM: 1-2]…, Quraish walimwambia: Waona kuwa Warumi watashindwa? Akajibu: Naam, wakasema: Unakubali kuweka rehani? Akajibu: Naam, hapo wakapigana kwa rehani, akamwambia Mtume S.A.W, Mtume akamwambia: “Waendee, uzidishe kiasi cha rehani”, akazidisha, kisha Warumi walishindwa na Waajemi, Mtume S.A.W alijuzisha hivi, na hii ndiyo ni kamari yenyewe iliyopo kati ya Abi-Bakr na washirikina wa Quraish, na Makkah katika wakati huo ulikuwa mji wa ushirikina, pia haifichiki kuwa Makkah katika wakati huo haukuwa mji wa vita, kwa sababu tokeo hili lilitokea kabla hata kutunga sheria ya Jihaad. [Fath Al-Qadiir, 6/178; Sharh As-siyar, 4/141; Al-mabsuut, 14/57].
6- Kwa sababu mali ya makafiri ni halali, basi mwislamu ana haki ya kuichukua bila ya hadaa kwani hadaa ni haramu; na kwa sababu waislamu wakiziteka nyumba zao, basi watazichukua mali zao kwa ngawira. [Sharh As-siyar, 4/1410; Al-Binayah, 7/385; Al-mabsuut, 14/85; Fathul-Qadiir, 6/178; Hashiyat Ibn Abidiin, 4/188].
Baada ya hayo, muhtasari wa maoni ya wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy kuwa: Inajuzu kutendeana na mikataba isiyo sahihi katika miji isiyo ya waislamu kati ya mwislamu na wakazi wa miji hii, ikiwa mkataba huu ni wa kuuza nyamafu, nguruwe, pombe au kamari. Na inavyolazimika kuangaliwa na msomaji wa matini hii ya wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy kuwa: Wafuasi wa madhehebu nyingine wana misingi inayowezesha kutendeana na hali za dharura na shida, pamoja na kuwepo uhusiano kati ya maoni ya wafuasi wa madhehebu ya Hanafiy na maoni ya madhehebu nyingine katika suala lenyewe. Miongoni mwa misingi hii ni:
1- Kufuata aliyejuzisha wakati wa dharura kwa ajili ya kuepusha dhiki, kwa hiyo Sheikh Ibrahim Al-Baijuuriy anasema: “Alipata mtihani wa kitu kama hiki, afuate aliyeruhusu “.
2- Katazo linakuwa katika kauli ya pamoja, Imamu As-Sayuutiy alitaja kuwa: “Hakikanushwi kitendo cha kutofautiana, bali inakanushwa kauli ya pamoja”, maana ya hayo kuwa: Wafuasi wa madhehebu ya kifiqhi wakihitilafiana katika suala moja haisihi kwa wafuasi wa madhehebu moja kupingana na wafuasi wa madhehebu nyingine, kwa sababu suala lina tofauti.
3- Kutofautisha kati ya mpaka wa fiqhi na hukumu na mpaka wa uchamungu, kwa sababu wanachuoni wamekubaliana kuwa mpaka wa uchamungu ni mpana zaidi kuliko mpaka wa hukumu ya kifiqhi; maana mwislamu huenda akaacha mambo mengi halali kutokana na uchamungu, kama walivyoacha masahaba R.A sehemu ya tisa ya kumi ya matendo ya halali wasije kuanguka katika haramu, lakini hii si kwa maana wao wanaharamisha uhalali, hivyo uchamungu ni mpana hata ikafikia mtu kuacha mali yake yote kutokana na uchamungu kisije kitu cha haramu kuingia ndani yake.
Kwa mujibu wa yaliyotangulia na madhehebu ya wafuasi wa Hanafiy: Kukopa Benki kwa riba katika nchi zisizo za waislamu kunajuzu na hakuna uharamu ndani yake, kwa sababu nchi hizi si mahali pa kusimamisha maamrisho ya kiislamu ndani yake; na pia mikopo katika hali hii ni kwa maridhiano ya nafsi zao, pamoja na kuwa kuna masilahi kwa waislamu, kwa kuwachanganya katika jamii zao, na kutojiepusha nao, kwa namna ambayo unahifadhika uwepo wao, masilahi yao, na kuwawezesha kulingania dini iliyo sahihi, bila ya mapigano wala ugomvi usio na sababu.
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mjuzi zaidi ya wote.

 

 

Share this:

Related Fatwas