Maswali ya Kutiba kwa Watoto Mapach...

Egypt's Dar Al-Ifta

Maswali ya Kutiba kwa Watoto Mapacha Waliogandana

Question

- Ipi hukumu ya kisharia ya kuwatenganisha watoto mapacha waliogandana?
- Ni nani mwenye mamlaka ya kutoa ruhusa ya kufanyiwa upasuaji: Je ni familia ya watoto mapacha, madaktari, mahakama au watoto wenyewe watakapofikia baleghe?
- Na kazi inakuwaje ikiwa kuna nafasi kubwa ya kufanikiwa upasuaji wa kuwatenganisha lakini familia ya watoto mapacha ikakataa?
- Je inafaa kuondoa mimba ikiwa itaonekana watoto mapacha wamegandana wakiwa tumboni?
- Je watoto mapacha waliogandana wanakuwa na roho moja au mbili, ni mtu mmoja au watu wawili?
- Je watoto mapacha waliogandana wana haki ya kuoa hukumu ipoje na ni namna gani?
 

Answer

Shukrani zote za Mwenyezi Mungu peke yake, sala na salamu ziwe kwa yule ambaye hakuna utume tena baada yake naye ni Mtume wetu Muhammad pamoja na watu wake na Masahaba wake na wale wote wanaomfuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.
Inafahamika kuwa mimba huanza pindi yai jeupe la mwanamke linapopokea tone la mwanamume, na kutunga mtoto tumboni ambaye anakuwa ndani ya mfuko wa uzazi na kuanza hatua za kukuwa, pindi anapokamilika kukuwa ndipo anapotoka na kuja kwenye uhai wa dunia kwa njia ya kawaida, na hutokea yai la mwanamke kuzalisha mayai mengi, na kila moja hugawanyika sehemu mbili kisha kila moja huungana na kutengeneza mtoto kamili, hapa ndipo huja watoto mapacha.
Na hutokea wakati mwingine kutotengana kwa ukamilifu na huzaliwa kutokana na hilo kile kinachofahamika mapacha wawili waliogandana, katika hali hii watoto hao wawili wanakuwa wameungana wao kwa wao katika sehemu fulani ya mwili na kupelekea kufanyika upasuaji wa kuwatenganisha.
Ama kuita aina hii ya pacha ni pacha Siyamia, inanasibishwa na mapacha wawili waliozaliwa kwenye mji wa Siyami kusini Mashariki mwa bara la Asia mwaka 1811 wazazi wao wakiwa ni wachina na watoto hao walikuwa wamegandana sehemu ya kifua, na inasemekana: Watoto hawa mapacha walioa dada wawili wa Uingereza na kuzaa nao watoto ishirini na wawili, na walifariki mwaka 1874, wala haikuchukua muda mrefu baada ya kufariki kwao ambapo mmoja wao alifariki kabla ya mwingine kwa masaa mawili, na inasemekana kunasibishwa kwa mapacha hao kwa sababu ni hali ya kwanza kimatibabu kupatikana, lakini Imamu Abalfaraj Ibn Al-Jauziy ameelezea katika historia yake kuhusu hali ya mapacha wawili waliogandana waligundulika mwaka wa arobaini na akataja hilo katika matukio ya mwaka 352, kwa maana kabla ya kutokea hali ya mapacha hao wawili wa Siyamia kwa karne nyingi, amesema Ibn Al-Jauziy: “Ametupa habari Muhammad Ibn Aby Twahir, ametupa habari Ally Ibn Al-Muhsin At-Tuughy kutoka kwa baba yake amesema: Alinipa habari Abu Muhammad Yahya Ibn Muhammad Ibn Fahd, na Abu Umar Ahmad Ibn Muhammad Al-Khalal, wamesema: Wametupa habari watu wengi kutoka maeneo ya Al-Muuswal na watu wengine miongoni mwa tunaowaamini na tunaamini ni sahihi kile walicho kizungumza kuwa waliona katika mji wa Muuswal mwaka wa mia tatu na arobaini watu wawili walikuwa na umri wa kati ya miaka thelathini wakiwa wamegandana upande mmoja sehemu ya juu mpaka kwenye kwapa, na walikuwa na baba yao, akawaambia kuwa wamezaliwa hivyo wakiwa mapacha waliogandana utawaona wakivaa mashati mawili na suruali mbili kila mmoja na vazi lake, isipokuwa mapacha hao shati halikuwa linawatosha kwa sababu ya kugandana kwa mabega yao na mikono yao wanapotembea na kuwaletea kero, na kufanya kila mmoja kuwa na mkono wake ambao unakutana na wa mwenzake nyuma ya mgongo wa mwenzake na hutembea hivyo, na walikuwa wanapanda mnyama mmoja na wala mmoja wao hawezi kwenda isipokuwa mpaka na mwengine naye atembee pamoja naye, ikiwa mmoja wao anataka kwenda kujisaidia basi anakwenda na mwenzake hata kama mmoja hana haja ya kwenda kujisaidia, baba yao aliwaambia kuwa pindi walipozaliwa watoto hao alitaka kuwatenganisha, akaambiwa, wataumia kwa sababu upande walioungana ni upande wa chini ya kwapa, hivyo haiwezekani ndipo akawaacha, watu wa mji wa Muuswal waliokuwa wakienda kuwaona na kushangaa pamoja na kuwapa zawadi mbalimbali.
Amesema Abu Muhammad: Kuna watu walinipa habari kuwa vijana hao wawili waliondoka katika mji wao, mmoja akapatwa na ugonjwa mwisho akafariki na akabakia mwingine akiwa hai kwa masiku mengi mpaka ikafikia huyu ndugu aliyehai hawezi kufanya chochote wala baba hawezi kumzika yule aliyefariki mpaka yule aliye hai akapatwa na ugonjwa kutokana na harufu ya yule aliyefariki naye huyu aliyebaki hai akafariki pia kisha wakazikwa wote wawili, na kiongozi wa nchi alikuwa amewaandalia madaktari, na akasema je kuna uwezekano wa kuwatenganisha? Aliwauliza madaktari kuhusu njaa je wanahisi njaa kwa wakati mmoja? Akasema: Pindi mmoja akiwa na njaa basi mwingine anakuwa na njaa kwa muda mdogo tu, mmoja wetu akinywa dawa baada ya muda wa saa mwingine hupata nafuu, mmoja anapokuwa na haja mwingine anakuwa hana, ila anapatwa na haja baada ya saa moja, wakaangalia wakagundua kuwa wana sehemu moja ya haja kubwa, kitovu kimoja, utumbo wa chakula mmoja, ini moja, bandama moja, lakini uti wa mgongo haukushikana, wakafahamu kuwa kuwatengenisha kutaleta madhara zaidi, wakagundua kuwa wana uume tofauti kila mmoja na wake wakiwa na korodani nne, na huenda kukitokea ugonvi kati yao mmoja wao huenda akawa hazungumzi na mwenzake kwa siku kadhaa kisha wakazungumza.
Imepokelewa kuwa kuna hali nyingine aliiona Imamu Shafi, imeelezewa na Abu Nuaeem kwenye kitabu cha: [Al-Hilliya] lakini hata hivyo Al-Haafidh Ad-dhahbiy ameipinga taarifa hiyo kwenye kitabu cha: [As-saiir].
Ama hukumu ya kisharia ya kufanyika upasuaji kwa ajili ya kuwatenganisha, asili ya suala hili ni kuwa inafaa, na asili ya kufaa kwake ni pamoja na Hadithi iliyopokelewa na Imamu Muslim kutoka kwa Jaabir amesema: “Mtume S.A.W. alimpeleka daktari kwa Ubayy Ibn Kaab alivunjika mfupa kisha akaichoma ngozi moto kwa ajili ya matibabu”. Hadithi hii asili ni kufaa kufanya kazi za upasuaji pale inapohitajika, kwani kuvunjika mfupa na kuchoma moto ngozi kwa ajili ya kutibia mfupa ni aina katika aina za upasuaji, hakuna shaka kuwa kuwatenganisha mapacha wawili waliogandana ni katika mahitaji muhimu ambayo ikiwa watacheleweshwa basi kutakuwa na uzito na kuhitajika juhudi kubwa na tabu za kihisia na zisizo za kihisia ambapo Mwenyezi Mungu ndio mjuzi zaidi.
Lakini wakati wa kuwapeleka kufanyiwa upasuaji mapacha waliogandana ili kutenganishwa basi yapaswa kuzingatiwa yafuatayo:-
La Kwanza: Watakaofanya upasuaji huo ni lazima wawe madaktari wenye weledi mkubwa wa upasuaji huo.
La Pili: Kupata ruhusa ya mapacha wenyewe kufanyika kwa upasuaji ikiwa hao mapacha ni wenye sifa ya kushauriwa, kama vile kuwa wameshabaleghe wenye akili na hiyari ya kutenda, wakiwa ni wenye mapungufu ya sifa hizo basi mwenye haki ya kusimamia na kutoa ruhusa ya upasuaji huzingatiwa kutokana na ukaribu zaidi, kwanza anatangulizwa baba kisha babu mzaa baba na kuendelea juu, kisha mtoto – akiwepo – kisha ndugu wa baba mmoja mama mmoja, kisha ndugu kwa upande wa baba, kisha watoto wa ndugu wa baba mmoja mama mmoja, kisha watoto kwa upande wa baba kisha wakina baba wadogo wa baba mmoja mama mmoja na baba, kisha wakina baba wadogo kwa upande baba, kisha watoto wa baba mdogo wa upande wa baba na mama, kisha watoto wa baba mdogo kwa upande wa baba, na utaratibu huu ndio asili katika mirathi, na hufuata wale wakaribu wengine katika mamlaka ya kutoa ruhusa kama kiongozi mkuu naye ni hakimu katika zama zetu hizi.
La Tatu: Kutenganishwa kwa mapacha hawa kusiendane na madhara zaidi ya madhara ya kubakia wakiwa wamegandana, kama kupelekea kuharibu kiungo cha mmoja wao kwa usalama wa mwingine, katika hali hiyo ni haramu kufanya upasuaji ikiwa dhana ya karibu zaidi ni kuwa yatatokea hayo, katika misingi ya sharia iliyopitishwa ni kuwa ikiwa kutakuwa na mgongano wa madhara ya aina mbili aina moja ikawa ina madhara zaidi basi yafanywe madhara yaliyo madogo, na madhara hayaondolewi na madhara yaliyo sawa au zaidi, anasema Imamu Al-Baghwiy katika sherehe ya Sunna: “Tiba ikiwa ndani yake ina hatari kubwa basi tiba hiyo inakuwa haifai”.
Vile vile ikiwa madaktari wenye weledi wana uhakika au wana dhana iliyokaribu zaidi kuwa mmoja wao ataishi baada ya kutenganishwa na mwengine atakufa kwa sababu ikiwa wataendelea kuishi katika hali hiyo wote wawili watakufa basi inafaa kutenganishwa.
Lakini pia tunaashiria kuwa ni ngumu kuweka sharti moja katika hali zote, isipokuwa tunasema kuwa inapaswa kufanyiwa utafiti kila hali peke yake, kwa sababu inaweza kuwa hali moja ni bora zaidi, baadhi ya hali nyingine ikahitajika kutoa muhanga kiungo cha mmoja au wote wawili ili kukamilike salama upasuaji wa kutenganishwa, na uharibifu unaotokana na hali hii unakuwa ni mwepesi zaidi kuliko uharibifu wa kubakia wamegandana wakiwa na viungo vyao salama.
La Nne: Haifai kwa daktari kufanya upasuaji ikiwa hajakubali kutoa ruhusa mwenye haki ya kutoa ruhusa, ikiwa kutakuwa na fursa kubwa ya kufanikiwa upasuaji wa kutenganishwa na familia ya mapacha hao ikakataa, basi upasuaji hautofanyika isipokuwa baada ya kufikishwa suala hilo mahakamani, ili mahakama iondoe mzozo uliopo kati ya mlezi na watu wenye weledi ambao wanaona ni lazima ufanyike upasuaji.
La Tano: Hawalazimishwi mapacha kufanyiwa upasuaji ikiwa wamefikia umri wa baleghe na wana akili timamu, tofauti ikiwa mmoja amekubali na mwingine akawa amekataa, katika hali hiyo jambo litarudishwa kwa madaktari, ikiwa watasema upo uwezekano wa kufanyiwa upasuaji wa kutenganishwa na wakawa salama basi inafaa kulazimishwa upasuaji yule aliyekataa, kwa sababu kukataa kwake kuna madhara kwa ndugu yake.
Ama kuhusu hukumu ya kutoa mimba ikiwa daktari amegundua kuwepo mapacha waliogandana tumboni, hapa hutofautishwa kati ya hali mbili.
Hali ya Kwanza: Ujauzito uwe umepita siku mia moja na ishirini na zaidi, ikiwa hivyo mtoto anakuwa tayari ameshapuliziwa roho, na dalili ya hilo ni Hadithi iliyopokewa na Imamu Bukhari na Muslim kutoka kwa Ibn Masuud R.A. kuwa Mtume S.A.W. amesema: “Hakika mmoja wenu hukusanywa viungo vyake akiwa tumboni siku ya arobaini, kisha anakuwa mfano wa pande la damu, kisha anakuwa mfano wa pande la nyama, kisha Mwenyezi Mungu anatuma Malaika na kumuamrisha maneno manne, na huambiwa: Andika matendo yake riziki yake muda wake wa kuishi ni mtu mbaya au mwema, kisha anapuliziwa roho”, ikiwa atapuliziwa roho basi haifai kutoa mimba, na kutoa mimba ndani wakati huo ni kuuwa nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharamisha kuuwa isipokuwa ni kwa njia ya haki.
Hali ya Pili: Ujauzito ulio chini ya muda huo na mtoto tumboni bado hajapuliziwa roho basi inafaa kuutoa, hali hii pindipo hakuna madhara kwa mama kutoa hiyo mimba, na hii ni kuepusha matatizo ambayo yataendana na hali ya kujifungua mapacha waliogandana, baadhi ya wanachuoni wamepitisha kitendo cha kutoa mimba kabla ya kupuliziwa roho ikiwa ni kwa dharura inayozingatiwa, kama vile kukatika maziwa baada ya kuingia kwa ujauzito na baba wa mtoto akawa hana mtu wa kumuajiri na akawa ana hofu huenda akafiriki mtoto wake atakaye zaliwa, kama ilivyonukuliwa na Ibn Abideen katika kitabu chake kutoka kwa Ibn Wahaban miongoni mwa wanasharia wa madhehebu ya Imamu Abu Hanifa, hakuna shaka kuwa matatizo tuliyotaja ni dharura kubwa kama alivyosema Ibn Wahaban.
Amesema Sheikh Al-Islaam Zakaria Al-Answaary katika sharhe ya Bahjah: “Kutoa mimba ikiwa ni kabla ya muda wa kupuliziwa roho kwa mtoto inafaa, au baada ya kupuliziwa roho ni haramu”.
Katika matini ya kitabu cha: [Al-Iqnaa cha Hijawy] miongoni mwa vitabu vya fiqhi ya Imamu Hanbal: “Inafaa kunywa dawa ili kuondoa tone la manii”.
Katika vitabu vya Ibn Muflihu Al-Hambaliy ni kuwa maneno ya wazi ya Ibn Aqiil ni kuwa: Inafaa kutoa mimba kabla ya mtoto kupuliziwa roho. Akasema: “Kuna mtazamo”.
Ama ikiwa mmoja wa pacha wawili ni mtu anayejitegemea ana roho yake tofauti na roho ya mwingine basi hili ni miongoni yasiyopaswa kuangalia kufaa kwake, miongoni mwa dalili ya hilo ikiwa mmoja miongoni mwao anaweza kufikiri na kupenda pasi na kushirikiana na mwenzake, na huenda mmoja akafariki na mwingine akabakia hai baada ya kifo cha mwenzake kwa muda mrefu, haya hayawezi kuwa isipokuwa kwa kila mmoja kujitegemea tofauti na mwenzake kuwa na roho yake na haiba yake.
Ama kuhusu kuoa mapacha waliogandana, ndoa ni makubaliano wakati wowote masharti yanapokamilika na nguzo zake basi makubaliano haya yanakuwa ni sahihi, kama maelezo yalivyotangulia kila mmoja yupo huru kwa mwenzake kihukumu, ikiwa makubaliano ya ndoa yamepita masharti yametimia na nguzo zake basi ndoa hiyo ni sahihi, hali ya kugandana haikuathiri na kuharibu ndoa kwa sababu ni jambo lipo nje na sharti za ndoa.
Ama namna ya kuendesha maisha ya ndoa jambo hili ni la ufafanuzi zaidi linaendana na hukumu za sharia na misingi yake mikuu ambayo miongoni mwake ni: Madhara huondolewa, Dharura huhalalisha yaliyo katazwa, Kilicho halalishwa kwa dharura hukadiriwa kwa kiwango chake, Mahitaji huchukua nafasi ya dharura ni sawa mahitaji ya umma au mahitaji binafsi, Matatizo huleta wepesi, Jambo linapobana basi hutanuka, Kunapokuwa na madhara mawili huachwa madhara makubwa zaidi na kuchukuliwa madhara madogo, na mfano wa misingi kama hii ambayo inayopelekea katika hili ulazima wa kufanya jambo, na uharamu wa kufanya jambo, kupendezesha kufanya jambo, kuchukiza kufanya jambo, kuhalalisha kufanya jambo, na sharia hufanyia kazi haya na mengine kutokana na ulaini wa sharia na upana wake pamoja na wigo wake, na ufafanuzi wa kila hali ni kwa mujibu wa hali yenyewe.
Naye Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mjuzi zaidi.


 

Share this:

Related Fatwas