Kwenda Kinyume na Kiongozi wa Nchi ...

Egypt's Dar Al-Ifta

Kwenda Kinyume na Kiongozi wa Nchi na Kumpindua.

Question

Ni hali zipi ambazo zitafaa kwenda kinyume na Kiongozi wa nchi na kumng’oa madarakani? Na je, sharti la kwenda kinyume na kiongozi wa nchi ni kutokana na ukafiri wake wa wazi tu, kwa namna ambayo kama atakuwa dhalimu au fisadi lakini sio ukafiri wa wazi haijuzu kwenda kinyume dhidi yake? Na nini udhibiti wa ukafiri wa wazi? 

Answer

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na rehma na amani zimwendee bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, masahaba wake na wanaomfuata, na baada ya hayo:
Uimamu au Uongozi, ni katika mambo yaliyokuwa na tofauti za watu tangu mwanzo wake, na ushahidi wa hayo ni Matukio mbalimbali yaliyotokea mwanzoni na baadaye, na ni moja ya mambo yenye tofauti baina ya makundi mbalimbali ya Waislamu.
As Sharistaniy amesema katika kiyabu cha: [Al Milal wa An Nihal 22/1, Ch. ya Al Halabiy]: "Na tofauti kubwa kuliko zote baina ya Umma ni ile ya Uimamu; kwani Upanga haujatumika katika Uislamu juu ya kuweka Msingi wa Dini kama ulivyotumika katika Uimamu katika nyakati zote, na Mwenyezi Mungu Mtukufu alirahisisha hivyo tangu mwanzo, na Answar na Muhajirina wakahitilafiana ndani yake".
Na Kiongozi ni mwakilishi wa umma katika ukhalifa wa unabii ili kulinda dini na siasa ya ulimwenguni. Ibn Khalduun Amesema katika kitabu chake cha: [Historia 239/1, Ch. ya Dar Al Fikr]: "Ukhalifa ni kuwasisitizia watu wote kwa mujibu wa Mtazamo wa Sheria kwa ajili ya masilahi yao ya Akhera na duniani yanayorejea kwenye Ukhalifa huo; kwani hali zote za duniani kwa ujumla zinarejea katika Sheria kwa kuyazingatia kuwa ni masilahi ya Akhera, ukweli ni kwamba, hayo ni kutokana na ukhalifa wa mwenye Sheria katika kuilinda Dini na siasa ya ulimwengu kwayo."
Wanachuoni wa Fiqhi wanaeleza katika vitabu vyao kuwa anayeshughulikia jukumu la Uimamu mkubwa, hakika yeye ni mwakilishi wa Waislamu. As Sarkhasiy amesema katika kitabu cha: [Al Mabsuutw 219/10, Ch. ya Dar Al Maarifa]: "Imamu ni mwakilishi wa Waislamu katika kuwatimizia haki zao, na haki zao zipo katika yale yanayowafaa." [Na kama hiyo katika kitabu cha: Manhi Aj Jalil, Sharhu Mukhtaswar Khalil 78/2, Ch. ya Dar Al Fikr, Mughniy Al Muhataaj 272/4, Ch. ya Dar Al Kutub Al Elmiyah, na Kashaafu Al Qinaa' 160/6, Ch. ya Dar Al Kutub Al Elmiyah].
Na ikiwa hilo ndilo lengo la Uimamu, basi hakika hili lenyewe linafanikishwa na yale anayoyafanya Kiongozi wa nchi ya kisasa, na ambayo yalifanywa na viongozi wa nchi ndogo ndogo hapo kale, na ndicho kilichofanywa na Ukhalifa wa Madola mbalimbali yaliyotokana na Ukhalifa Mkuu, kwani mmoja miongoni mwa Viongozi wa Kiislamu hii leo ana maana ile ile ya Uimamu.
Na Rai ya Ahlu Sunna imethibiti kwamba Kiongozi haifai kwa Muislamu kumgeuka na kwenda kinyume naye hata kama Kiongozi huyo atakuwa dhalimu, na kwamba haijuzu kumgeuka Kiongozi isipokuwa atakapodhihirisha ukafiri wazi wazi kwa dalili tulizo nazo kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Na dalili ya hayo ni yaliyotajwa kutoka kwa Mtume S.A.W. kwamba amesema: "Itakuwa na athari pamoja na mambo mnayoyakataa .Wakasema: ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, ni kitu gani unachotuamrisha? Akasema: muifikishe Haki ambayo mnadaiwa, na mumuombe Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa yale yaliyo yenu".
Na kauli ya Mtume S.A.W. "Viongozi wenu wema ni wale mnaowapenda na wanaokupendeni, mnaowatakia rehma na wanaokutakieni Rehma, na viongozi wenu wabaya ni wale mnaowachukia na wanaokuchukieni, na mnaowalaani na wanaokulaanini. Wakasema Maswahaba kumuuliza Mtume S.A.W: Je, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu, je, tuende nao kinyume? Akasema Mtume S.A.W: Hapana. Msifanye hivyo kwa kuwa wanakusimamishieni Swala, Hapana. Msifanye hivyo kwa kuwa wanakusimamishieni Swala. Isipokuwa Kiongozi atakayeenda kinyume na hilo na mkamwona analeta kitu kiovu cha kumwasi Mwenyezi Mungu Mtukufu basi na mchukie kwa kile kitendo cha maasi ya kumwasi Mwenyezi Mungu Mtukufu na wala msiouondoshe mkono wa utiifu kwake." Imepokelewa na Muslim.
Na kauli ya Mtume S.A.W.: "Mwislamu anapaswa kusikiliza na kutii kwa yale anayoyapenda na anayoyachukia, isipokuwa atakapoamrishwa kufanya maasi, na ikiwa ataamrishwa kufanya maasi basi hakuna kusikia wala kutii".
Na kutoka kwa Hudhaifah Bin Al Yaman R.A. alisema: Tukasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu: Sisi tulikuwa katika shari, basi Mwenyezi Mungu Mtukufu Akutuletea Heri sisi sasa tunayo, basi je, itakuwa heri baada ya shari hiyo? Mtume S.A.W. akasema: Ndiyo, basi nikasema: je, itakuwa heri baada ya shari hiyo? Mtume S.A.W. akasema: Ndiyo, nikasema: Je. Itakuwa shari baada ya heri hiyo? Mtume S.A.W. akasema Ndiyo. Nikasema vipi? Mtume S.A.W. akasema: " Watakuja baada yangu mimi viongozi wasioufuata mwongozo Wangu, wala hawaufuati mwenendo wangu mimi, wasimama miongoni mwao Wanaume ambao nyoyo zao ni nyoyo za mashetani katika miili ya binadamu, nikasema: nifanye nini ikiwa nitafikiwa na wakati huo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu? Akasema: Usikilize na Umtii kiongozi wako, hata kama mgongo wako utapigwa, na mali yako ikachukuliwa, basi wewe sikia na utii".Imepokelewa na Muslim.
Kutokana kwa Ibada Bin As Swametw R.A., alisema: Mtume S.A.W, alituita na tukampa kiapo cha utiifu, basi akasema kwa alichotubebesha: Hakika sisi tumechukua Kiapo cha utiifu kwa ajili ya kusikia na kutii, katika mazuri na mabaya yetu, mazito na mepesi yetu na ya athari juu yetu, na kwamba hatutagombana katika jambo la kiongozi, akasema: "Isipokuwa mtakapouona ukafiri wa wazi, na mkawa nyinyi mna dalili yake kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. [Imepokelewa na Bukhari na Muslim]
Na Imamu At Twahawiy alisema katika kitabu chake kinachojulikana: [Akidah Uk. 34. Ch. ya Dar Al Baiyareq]: "Na wala hatuoni kuwa ni vyema kuwageuka viongozi wetu na wale wenye madaraka juu yetu pale wanapofanya ujeuri, wala hatuwatolei wito wa kufanya hivyo wala hatuunyanyui mkono wa kutowatii wao, na tunaona kwamba kuwatii wao ni kumtii Mwenyezi Mungu Mtukufu na ni lazima kufanya hivyo kama wao hawajaamrisha Maasi, na tunawaombea wajirekebishe na kusamehewa makosa yao".
Na mtazamo wa Kisheria wa kwamba Kiongozi hatolewi madarakani kwa ufasiki tu na Maasi: ni kwamba hakuna mtu yeyote mwenye kinga baada ya Mitume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu A.S, na kwamba kama hali hiyo ingetokea basi jambo la raia lingekosa utulivu na mambo yao yangekuwa Magumu na wasingeweza kupata usalama wowote.
Imamu wa Al Haramain Aj Juweniy alisema katika kitabu cha: [Ghayaath Al Umam, Ku. 101-104, Ch. ya Maktabat Imamu Al Haramiain]: "Mwelekeo wa kwamba ufasiki wa Kiongozi unapelekea kung’olewa madarakani ni mbali na kutokea kwake; kuyagusa yale yanayokuwa na ufisadi wa Kiongozi juu ya Haki ya yule ambaye sio wajibu kuwa na Kinga, kwa Uwazi wake, iwe kwa siri au wazi wazi, …na wala haifichiki kwa mwadilifu ya kwamba kushurutisha kudumu kwa uchamungu kunapelekea mwenye kushindwa kuwa na ugumu wa Uongozi Mkuu. Na kisha, kama ufasiki ambao Wanavyuoni wanakubaliana juu yake kwamba unawajibisha kumng’oa Kiongozi madarakani au yeye mwenyewe kung’atuka basi maneno yangekuwa yanaelekea kwenye vitendo vyake vyote na maneno yake kwa aina na hali zake mbalimbali, na kwa kuwa muda umepita wa watu kuufuatilia ufasiki wake unaoweza kupelekea aondoshwe madarakani, na kwa kukusanyikia watu makundi kwa makundi, kimeonekana katika nyakati nyingi kuwa hali hiyo hupelekea ukinzani wa kukana na kuthibitisha, na pindi utiifu bora kwa Imamu ulipotulizana katika saa ya… Kinacholazimika kuamuliwa ni kwamba Uovu unaotokana na Kiongozi hausitishi kumtazama, na kuna uwezekano mkubwa akatubu na kurejea nyuma na kujutia alichokifanya, na sisi tumeamua kwa kila aina ya zingatio, kwamba katika kuelekea kumng’oa Kiongozi madarakani, kwa kila kosa la kuteleza kwa Kiongozi ni kuukana Uongozi wenyewe na kuukataa, na ni kuondosha faida zake na kuondosha pia matunda yake, na kuondosha Imani katika Uongozi na ni kuwahimiza watu waiepushe mikono yao dhidi ya Utiifu kwa Kiongozi".
Al Hafidh Ibn Abdulbar alisema katika kitabu cha: [At Tamhiid 279/23, Ch. ya Wizarat Umuum Al Awqaaf na Mambo ya Kiislamu, Moroko]: "Na katika kugombana na Kiongozi aliye Jeuri, Kundi katika Muutazilah, na Makhawaariji wote wanajuzisha kupambana na Kiongozi na kumng’oa madarakani. Lakini Watu wa Haki ambao ni Ahlu Sunna wamesema kuwa hili ni chaguo ambalo Kiongozi anatakiwa awe mbora Kimaadili, mwadilifu, na mwema, na hata kama hakuwa hivyo, uvumilivu na kumtii Kiongozi jeuri ni bora zaidi kuliko kwenda kinyume naye; kwani katika kugombana naye na kwenda kinyume naye kuna kuubadilisha Usalama kwa hofu. Kwani hivyo hupelekea umwagaji damu na mapigano pamoja na ufisadi ardhini, na jambo hili ni kubwa sana kuliko kumvumilia Kiongozi Jeuri na mwovu, na Misingi Mikuu ya Dini inashuhudia hivyo na Akili pamoja na Dini zinashuhudia hivyo kwamba linalochukiza zaidi kati ya mambo mawili ni bora kuliacha, na kila Kiongozi anaesimamisha Swala ya Ijumaa, na Iddi na anapambana na adui na anawalinda watu wake wote na anasimamisha Sheria zote dhidi ya maadui na anafanya uadilifu kwa watu kwa kutetea wanavyodhulumiana, na anakubalika na waungwana na njia zote zinakuwa na u salama basi ni wajibu kumtii kwa kila anachokiamrisha katika maboresho ya lolote au jambo lolote lililo Halali."
Na Al Ezz Ibn Abdusalaam anasema katika kitabu cha: [Al Fatawa Al Kubra 79/1, Ch. ya Dar Al Kutub Al Elmiyah]: "Na kuhusu Uongozi au Uimamu Mkuu, kushurutisha uadilifu ndani yake kuna hitilafu za Wanachuoni kutokana na uovu kuwa mwingi zaidi kwa Viongozi Wakuu, na kama tungeshurutisha uadilifu juu yao basi vitendo vyote vinavyoafikiana na Haki vingesita kwa kumsindika madarakani miongoni mwa Makadhi na Maafisa mbalimbali, na Wakuu na wakuu wa Jeshi la Ulinzi watakaomweka na kuchukua watakachokichukua na kutoa watakachokitoa, na kushikilia Sadaka na Mali za Umma na hasa hasa zile zilizo chini ya mamlaka yao, uadilifu haukushurutishwa katika vitendo vyao vinavyoafikiana na Haki kutokana na kushurutisha huko kuleta madhara kwa Umma, na kupotea kwa masilahi haya yote ni jambo ovu zaidi ya kupotea Uadilifu wa Kiongozi."
Na Ibn Taimiah amesema katika kitabu cha: [Minhaaj As Sunnah An Nabawiyah 390/3, Ch. ya Chuo Kikuu cha Imamu Mohammad Bin Suod Al Islamiyah]: "Kilicho Mashuhuri kwa Madhehebu ya Ahlu Sunna, wao wanaona kwamba haifai kuwageuka viongozi na kupambana nao kwa silaha hata kama wao wana dhulma kama zilivyosema hivyo Hadithi nyingi Sahihi za Mtume S.A.W; kwa sababu ufisadi katika vita pamoja na fitna ni mkubwa zaidi kuliko ule unaopatikana kwa wao kudhulumiwa bila ya kupigana vita au fitna na kuwasukuma mafisadi wakubwa kufuata ya chini kati ya viwili hivyo, na huwenda ikawa haijulikani kwa umma wowote ulioenda Kinyume na Kiongozi wake na hali hiyo inapelekea ufisadi mkubwa kuliko ule ufisadi ulioondoshwa na Umma huo".
Na pia katika kitabu hicho hicho: [561/1, Ch. ya Chuo Kikuu cha Imamu Mohammad Bin Suod Al Islamiyah]: kwamba Mtume S.A.W. aliambia kuwa: "Watakuja baada yangu mimi Viongozi wasioufuata mwongozo wangu, wala hawaufuati mwenendo wangu mimi, wasimama miongoni mwao Wanaume ambao nyoyo zao ni nyoyo za Mashetani katika miili ya binadamu, nikasema: nifanye nini ikiwa nitafikiwa na wakati huo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu Mtukufu? Akasema: Usikilize na Umtii Kiongozi wako, hata kama mgongo wako utapigwa, na mali yako ikachukuliwa, basi wewe sikia na utii". Na pamoja na hayo Mtume S.A.W. akaagiza kusikiliza na kumtii kiongozi, basi ilibainika kuwa Imamu ambaye anatiiwa na mwenye madaraka hata kama akiwa mwenye uadilifu au mwenye dhulumu".
Ama ukafiri wazi wazi ulifasiriwa na Imamu An Nawawiy kama ni maasi ambayo haifai kutafsiri kwa kuyafananisha, na akajaalia mzozo ni kuhubiri na kukemea kwa ulimi, basi akasema katika kitabu cha: [Sharhu Sahihi Muslim 229/12, Ch. ya Dar Ihyaa At Turath Al Arabiy]: "Na Ukafiri unaokusudiwa hapa ni maasi, na maana yake: mna nyinyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, ndani yake Dalili: kwa maana ya kwamba mnajua kutokana na Dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, na maana ya Hadithi: Msigombane na wenye Madaraka juu yenu katika Madaraka yao wala msiwapinge katika Madaraka hayo isipokuwa mtakapoona uovu kutoka kwao uliotokea kweli na mna uhakika nao ambao unahusu Misingi ya Dini ya Uislamu, basi iwapo mtaona hivyo basi wakemeeni na mseme kweli popote mlipo.
Ama kwa upande wa kuwakataa na kupambana nao ni Haramu kabisa kwa kukubaliana Waislamu wote hata kama viongozi hao ni waovu wenye kudhulumu, na kuna Hadithi nyingi zilizoizungumzia maana hiyo tuliyoitaja, na Ahlul Sunna wamekubaliana wote kwamba Kiongozi haondoshwi madarakani kwa uovu wake, na kile kinachotajwa na baadhi ya Wanavyuoni wetu ni kwamba katika Vitabu vya Fiqhi kwamba Kiongozi anatengwa na imesimuliwa kutoka kwa Muutazilah pia lakini msemaji akachanganya kuhusu msemaji kuwa ameenda kinyume na wengine wote.
Na Ali Al Qariy alining'nizia yaliyosemwa na An Nawawiy yaliyo tofauti nayo katika kitabu cha: [Merqatu Al Mafatih 2394/6, Ch. ya Dar Al Fikr] basi akasema: "Na Kauli yake: (maana ya ukafiri iliyopo hapo ni maasi) pamoja na kwamba uwazi ni kuwa ukafiri uko katika mlango wake na utenganishaji uko katika kulitumia kwake, kinyume na ikiwa itakusudiwa maasi basi hakika mambo yalivyo, haitasihi kutenganisha kilichounganika ambacho ni asili; na kwa hivyo haijuzu kuliondosha jambo kwa watu wake kwa sababu ya kuasi kwake kama ilivyofahamika kutokana na maelezo na ufafanuzi wake."
Na Alhaafidh Ibn Hajar anaonesha maelezo katika sehemu ya ugomvi na namna yake kwa mujibu wa uwepo wa mapokezi mengi ya Hadithi ambayo yalipokelewa mara moja kwa kutaja Ukafiri wa wazi, na mara nyingine kwa kutaja maasi badala ya ukafiri, kwa hiyo yeye anaona kuwa mzozo hapo katika hali ya kutokea ukafiri wa kweli utakuwa ni kwenda dhidi ya Kiongozi na kumng’oa madarakani hata kama ni kwa nguvu, kwa hiyo kukemea hapa kunakuwa kwa mkono.
Ama katika hali ya ufisadi, dhuluma na mabavu, basi hapo mzozo utakuwa kwa maana ya kumnasihi na kuchukizwa naye tena kwa upole, na kuchukizwa naye katika hali hii kutakuwa ni kwa ulimi au kwa moyo kama mtu hatakuwa na uwezo wa kuchukua hatua, kwa mfano kama atajihofia yeye mwenyewe nguvu za Kiongozi huyo Dhalimu. [Kitabu cha; Fathu Al Bariy 8/13, Ch. ya Dar Al Maarifa, Bairut].
Na usahihi ulivyo hapo ni kwamba ukafiri wa wazi unachukuliwa kwa mwonekano wake; kwani hicho ndicho kinachofuatwa, na kuzingatia kinachofuatwa ndilo jambo bora zaidi, na panakusudiwa kumjulisha Kiongozi kinachohukumia Kuritadi kwake na kutoka katika Uislamu.
Na kwa maana yoyote iwayo, jambo hili linategemea pia uwianishaji baina ya Masilahi na Mabaya, hata kama Kiongozi atakuwa anastahiki kung’olewa madarakani na sisi tukakuta kwamba hatua mbalimbali za kumng’oa madarakani zinaweza zinapelekea Madhara makubwa, basi haijuzu kwa wakati huo sisi kwenda Kinyume naye.
Ilitajwa katika kitabu cha: [Al Mawaqef] kwa mwanachuoni mkuu Al Qadhi Adhudiin Al Aijiy na sharhu yake kwa Bwana As Sharifu Al Jorjaniy [595/3, Ch. ya Dar Aj Jeel, Bairut]: Na wananchi wanalazimika kumng’oa kiongozi madarakani kwa sababu inayolazimisha jambo hili litokee, kama vile akawa na jambo linalowajibisha kuvuruga hali za Waislamu na kuharibiwa mambo ya dini kama walivyokuwa wao na nafasi ya kumsindika madarakani na kusimamisha kwake nidhamu ya Nchi na kuitanguliza. Na ikiwa kuondoshwa kwake madarakani kutapelekea Fitna, basi pataangaliwa moja dogo zaidi kati ya madhara haya mawili.
Na kunalingana katika kuzuia na kuharamisha kubeba silala dhidi ya Kiongozi pamoja na njia nyingine nyingi kama hizo nyingine zitapelekea matokeo yale yale ambayo kwa ajili yake kumeharamishwa kubeba silaha hizo, nayo ni Fitna, Umwagaji damu, Uvurugaji wa maelewano ya watu, na kwa hivyo unakuwa uovu wa kumwondosha madarakani kiongozi ni mkubwa zaidi kuliko kuendelea kuwa kwake madarakani.
Imamu Al Ghazaliy alisema katika kitabu chake cha: [Ihyaa' Aulumu Ad Deen 140/2, Ch. ya Dar Al Maarifah]: "Kiongozi Jeuri na Mjinga, hata anapochomwa na mwiba na ukawepo ugumu wa kung’oa, na kumbadilika kwake kunaonekana kutaleta fitina, basi hakutekelezwi, na ni lazima kumwacha na kumtii".
Na wingi wa maovu yaliyojitokeza kwa sababu ya kuwa dhidi ya Kiongozi wa Nchi ilikuwa ndio sababu kubwa ya kuondosha tofauti iliyokuwepo baina ya wema waliotutangulia katika Jambo hili.
Ibn Hajar Al Asqalaniy amesema katika Tarjamat Al Hasan Bin Swaleh: [Tahdheeb At Tahdheeb 288/2, Ch. ya Dairat Al Maarif An Nidhamiya, India]: "Na Kauli yao alikuwa anaona Upanga; ina maana: alikuwa anafuata rai ya kubeba upanga dhidi ya Kiongozi Jeuri, na haya ni madhehebu ya tangu zamani ya Wema waliotangulia, lakini rai iliyotulizana ni kuachana na jambo hilo; kutokana na walivyoliona jambo hili lilipelekea hali ngumu zaidi kuliko ile ya mwanzo; na katika Tukio la Hurrah na Tukio la Ibnul Ash-ath na mengine mengi, kuna Mazingatio kwa mwenye kuzingatia.
Na katika zama hizi zinapatikana aina nyingi za njia bora ambazo kwazo kuna uwezekano wa kutaka marekebisho; kama vile maandamano ya amani na kupeleka madai ya kisiasa, na kufuata Katiba na sheria za kimataifa na kumchukulia hatua mwenye kuzikiuka na nyingine nyingi ambazo vyombo mbalimbali vya kisasa vinakuwa chini yake na kuzingatia kuwa ni haki ya kisheria ya wananchi.
Na hivi sasa, Utawala wenye mfumo wa Urais wa Nchi unasimama kwa Nadharia ya Mfungamano wa Kijamii baina ya Kiongozi na wananchi wake, na kutokana na mfumo huo kuna masharti na nguzo zake, na vinafungamana na haki pamoja na wajibu, na wakati wowote Kiongozi anapokiuka wajibu wake kwa wananchi basi wananchi hao wanaweza kuitumia haki yao katika kumpitishia maamuzi kupitia njia zilizowekwa kisheria.
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mjuzi zaidi.
Ofisi ya Misri ya kutoa Fatwa.
 

Share this:

Related Fatwas