Hukumu ya Mwanamume Kupeana Mikono ...

Egypt's Dar Al-Ifta

Hukumu ya Mwanamume Kupeana Mikono na Mwanamke wa Mbali

Question

Kwa Jina la Mwenyezi Mungu, shukrani zote Anastahiki Mwenyezi Mugu, rehema na amani zimwendee Mtume wa Mwenyezi Mungu pamoja na watu wa nyumbani kwake na Masahaba zake na wale waliomfuata.

Answer

Kwa Jina la Mwenyezi Mungu, shukrani zote Anastahiki Mwenyezi Mugu, rehema na amani zimwendee Mtume wa Mwenyezi Mungu pamoja na watu wa nyumbani kwake na Masahaba zake na wale waliomfuata.

Baada ya Utangulizi

Huu ni utafiti katika hukumu ya mwanamume kupeana mikono na mwanamke wa mbali kwa maana asiye ndugu, pamoja na kubainisha maelezo ya madhehebu ya Wanachuoni kwenye hilo.

Maana ya kupeana mikono

Kupeana Mikono: Ni kuchukua mkono na kuuingiza ndani ya mkono mwingine([1]).

Na Ibn Mandhur amesema: Ni kukutanisha kiganja na kiganja na kukutanisha uso na uso([2]).

Al-Hafidh Ibn Hajar amesema: Kusudio la kupeana mikono ni kupeleka kiganja cha mkono kwenye kiganja cha mkono mwingine([3]).

Kusudio la mwanamke wa mbali

Mwanamke wa mbali: Ni yule ambaye si mke wala aliyeharamishwa kuoa kwa sababu ya undugu au kunyonya naye au ukwe([4]).

Imamu An-Nawawi amesema: “Fahamu kuwa ukweli mwanamke aliye haramu ambaye inafaa kumwangalia na kukaa naye chemba pamoja na kusafiri naye ni kila mwanamke aliye haramu moja kwa moja kumwoa kwa sababu ya uhalali wa uharamu wake. Kauli yetu tuliyosema: Moja kwa moja: Ni kumtenga dada wa mke mama yake mdogo shangazi yake na mfano wao. Na kauli yetu: Kwa sababu halali: Ni kumwondoa mama mkwe na binti yake, kwani wawili hao ni haramu moja kwa moja na wala si watu wa mbali, kwa sababu kuingilia kwa shaka hakuna sifa ya uhalali. Na kauli yetu: Kwa umbali wake: Kutenga kulaani, kwani ni haramu moja kwa moja kwa sababu ya halali na wala si mtu wa mbali, kwa sababu uharamu wake si umbali wake bali ni adhabu nzito.

Naye Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua zaidi([5]).

Fahamu kuwa wanawake walioharamu moja kwa moja kuoa ni wale ambao si halali kuwaoa kwa hali yeyote, na uharamu wao ima kwa nasaba au kunyonya au kwa sababu ya ukwe.

Walio haramu kwa nasaba: Ni saba, nao ni: Mama – wanaingia katika kundi hili wakina bibi na kuendelea juu, kisha mabinti – wanaingia katika kundi hili binti zao na kushuka,  kisha wakina dada – ni sawasawa wa baba mmoja mama mmoja au baba mmoja au mama mmoja, kisha mama wadogo mashangazi na kupanda – ni sawasawa kwa upande wa baba au mama, kisha mabinti wa ndugu wa kiume na mabinti wa dada.

Walio haramu kwa kunyonya: Ni saba pia, kama ilivyo kwenye nasaba, kwa kauli ya Mtume S.A.W.: “Ni haramu kwa ndugu wa kunyonya yale yaliyo haramu kwa ndugu wa nasaba”([6]).

Ama walio haramu kwa sababu ya ukwe: Ni mke wa baba, mke wa mtoto, mama wa mke - kwa kule tu kufunga ndoa na binti, na binti wa mke – kwa kule tu kumwingilia mama yake.

Waliotangulia kutajwa hao ni haramu moja kwa moja.

Ama walio haramu kwa muda nao ni: Dada wa mke, aliyeachwa talaka tatu, na anayefanya kazi kwa mume mwingine wa ndoa au eda na ambaye hana dini ya mbinguni, na watano ni mwenye ndoa ya wake wanne.

Kauli za Madhehebu manne katika hukumu ya kupeana mikono na mwanamke wa mbali:

Mdhehebu ya Abu Hanifa

Watu wa madhehebu ya Abu Hanifa wamesema kuwa ni haramu mwanamume kumpa mkono mwanamke ikiwa ni kijana hata kama hakutakuwa na fitina, kama hakuna umuhimu wa kufanya hivyo, lakini kwa upande mwingine wamepitisha kumpa mkono mwanamke mtu mzima ambaye hatamanishi.

Katika kitabu cha Tabiyin Al-Hakaik sherehe ya kitabu cha Kanzu dakaik cha Zailay: “Wala haifai kwa mwanamume kugusa sura yake wala viganja vyake hata kama atajilinda na matamanio, kwa kuwepo umbali na kukosekana umuhimu au dharura ya hilo, na Mtume S.A.W. amesema: “Mwenye kugusa kiganja cha mwanamke bila ya dharura, basi Siku ya Kiyama atawekewa katika kiganja chake kaa la moto”, hii ikiwa mwanamke ni msichana mwenye kutamanisha, ama akiwa ni mtu mzima kwa maana ya mzee hatamanishi hakuna ubaya kupeana naye mikono na kugusa mkono wake, kwa kukosekana wasiwasi wa fitina, imepokewa kuwa Abu Bakr R.A. alikuwa anaingia kwa watu wa baadhi ya makabila ambayo alikuwa amenyonya kwa watu hao, na alikuwa akipeana mikono na wakina mama vikongwe, na Abdillah Ibn Zubeir alimwajiri mama mtu mzima ili kumuuguza, na mama huyo alikuwa akibonyeza miguu ya Abdillah Ibn Zubeir na kugeuzageuza kichwa chake([7]).

Madhehebu ya Imamu Maliki

Madhehebu ya Imamu Maliki yamesema kuwa kupeana mikono na mwanamke si ndugu ni sawasawa kwa mtamanio au si kwa matamanio, ni sawasawa mwanamke alikuwa msichana au mtu mzima, akichukua mjumuiko wa dalili zilizothibiti ni haramu.

Katika sherehe ya kitabu Saghiir cha Sheikh Dardir na kitabu cha Mwanachuoni As-Sawy: “Wala haifai mwanamume kupeana mikono na mwanamke”, kwa maana ya mwanamke siye ndugu, hata kama atakuwa mkongwe; kwa sababu halali ni kuona tu, lakini inapendeza kupeana mikono kati ya wanawake wawili na wala si kati ya mwanamume na mwanamke aliyehalali kumuona([8]).

Madhehebu ya Imamu Shafi

Maana ya maneno ya Wanachuoni wa madhehebu ya Imamu Shafii ya kutofaa mwanamume kupeana mikono na mwanamke si ndugu isipokuwa kwa masharti mawili: Kuwepo usalama wa fitina, na uwepo wa kizuizi ikiwa itahitajika hivyo.

Katika kitabu cha Al-Minhaj na sherehe yake: “Hilo linafaa kwa mwanamume kwa sharti la kuwepo kizuizi na kulinda fitina, likachukuliwa kuwa ni halali kumpa mkono mwanamke wa mbali kwa kuwepo kizuizi, na inafahamika uhalali wa kumpa mkono kwa sharti hizo mbili ikiwa ni haramu kumgusa sehemu nyingine isiyokuwa uso wake na viganja vyake bila ya kizuizi hata kama hakutakuwa na fitina na kuleta matamanio, na hili linakubaliana pia na kumkumbatia hata kama kutakuwa na kizuizi”([9]).

Katika kitabu cha Hashiyati Sharwani kauli ya mtunzi: “Imechukuliwa uhalali wa kumpa mkono mwanamke wa mbali kukiwa na kizuizi” Inapaswa kuwepo kigezo kwa mtoaji mkono na mpewa mkono”([10]).

Makusudio ya kuzuia kumpa mkono – kwa upande wa Imamu Shafi – ni kuzuia sababu ya matamanio na kuondoa dhana chafu, haya masharti mawili yaliyotajwa yanafikia hili kusudio, miongoni mwa sababu muhimu zaidi za kuleta matamanio ni kukutana kwa ngozi mbili kati ya mwanamke na mwanamume, na kizuizi huwa kinazuia huku kukutana kwa ngozi mbili hivyo kunaondoa sababu.

Vilevile ikiwa kutakuwa na kizuizi na ikahofiwa fitina kwa kupata ladha huyu mwenye kutoa mkono kupitia mwenye kupewa mkono kwa mfano, basi inapaswa kuondoa hii mada pia, na kuwekwa sharti la usalama wa fitina wakati wa kupeana mikono, na kutokana na hilo yamekuja haya masharti mawili.

Madhehebu ya Imamu Hanbal

Watu wa Imamu Hanbal wamesema kuwa haifai kumpa mkono msichana wa kigeni, ama kwa upande wa mwanamke mtu mzima inafaa kumpa mkono, na kuna mapokezi mengine kutoka kwa Imamu Ahmad kuwa inachukiza kabisa.

Katika kitabu cha Al-Iqnaa na sherehe yake: “Wala haifai kumpa mkono msichana asiye ndugu” kwa sababu inaangaliwa kuwa ni uovu, ama mwanamke mzee basi mwanamume anaweza mpa mkono kama ilivyotajwa katika milango mbalimbali, na katika upokezi wa Ibn Mansour: Inachukiza kuwapa mkono wanawake, Mohammad Ibn Abdillah Ibn Mahran amesema: Aliulizwa Abu Abdillah kuhusu mwanamume kumpa mkono mwanamke, akasema: Hapana haifai, na akasisitiza sana nikauliza: Je kumpa mkono kwa nguo yake, akasema: Hapana haifai, yule mtu akauliza: Ikiwa ni ndugu akasema: Hapana, nikasema, je binti yake, akasema: Ikiwa binti yake hakuna ubaya, kuwa haramu moja kwa moja ni kauli iliyopitishwa na Sheikh Taqiyyudeen, ama kwa upande wa mzazi wa kiume kwake inafaa – ameyasema hayo katika kitabu cha Adabu – “([11]).

Tuliyoyanukuu kwenye madhehebu manne tunafupisha kama ifuatavyo:

Kwanza: Jamhuri ya Wanachuoni – ukimuondoa Imamu Shafi – hawajapitisha mwanamume kumpa mkono mwanamke wa mbali kwa maana asiye ndugu wakiwa wote wawili ni vijana, ama Imamu Shafi amepitisha kwa masharti mawili: Kukosekana fitina, na uwepo wa kizuizi ikiwa itahitajika.

Pili: Jamhuri ya Wanachuoni – ukimwondoa Imamu Malik – wamepitisha mwanamume kumpa mkono mwanamke wa kigeni kwa maana asiyekuwa ndugu akiwa ni mzee asiyetamanisha.

Tatu: Kuna upokezi mwingine kutoka kwa Imamu Ahmad Ibn Hambali unasema, inachukiza moja kwa moja.

Dalili za wenye kuzuia

Wenye kuzuia kumpa mkono mwanamke wanachukua dalili zifuatazo:

Kujizuia kwa Mtume S.A.W. kuwapa mkono wanawake wakati wa kiapo cha utiifu, na katika hili kuna Hadithi nyingi: Kutoka kwa Mama wa Waumini Bi. Aisha R.A. mke wa Mtume S.A.W. amesema: Waumini wa kike walikuwa pindi wanapokuja kwa Mtume S.A.W. akiwafanyia mtihani kwa kauli ya Mwenyezi Mungu: {Enyi mlio amini! Wakikujilieni wanawake Waumini waliyohama, basi wafanyieni mtihani} Al-Mumtahinah: 10. Bi. Aisha amesema: Mwenye kukubali sharti hili katika Waumini wa kike atakuwa amekubali mtihani, na Mtume S.A.W. alikuwa pindi wanapokubali kwa kauli zao aliwaambia: “Nendeni kwani mmeapa kiapo cha utiifu” Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu mkono wa Mtume S.A.W. haujagusa kabisa mkono wa mwanamke zaidi ya wao kutoa kiapo cha utiifu kwa maneno, Ninaapa kwa Mola Mtukufu Mtume wa Mwenyezi Mungu hajawahi kushirikiana na wanawake isipokuwa kwa kile Mwenyezi Mungu Alichoamrisha, Anawaambia pale wanapokubali kuwa: “Mmetoa kiapo cha uaminifu” kwa maneno([12]).

Hafidhi Ibn Hajar amesema, kauli yake: “Nimekupa kiapo cha utii kwa maneo” ni kusema hayo kwa maneno tu na si kwa kumpa mkono, kama ilivyokuwa kawaida ya wanaume kutoa mkono wakati wa kiapo cha utii” ([13]).

Na amesema Imamu An-Nawawi kwenye kauli yake: “Ninaapa kwa Mwenyezi Mungu mkono wa Mtume S.A.W. haujagusa kabisa mkono wa mwanamke zaidi ya wao kutoa kiapo cha utiifu kwa maneno” ndani yake kuna utoaji wa kiapo wanawake kwa maneno pasi na kumshika kiganja, na ndani yake ni kuwa kiapo cha utii cha wanaume ni kushikana viganja vya mikono na kuzungumza, na pia maneno ya mwanamke wa mbali kwa maana si ndugu ni halali kusikiliza, na sauti yake sio uchi, na kuwa haifai kugusa ngozi ya mwanamke wa mbali kiundugu pasina dharura yeyote kama vile daktari na utoaji damu”([14]).

Kutoka kwa Umaima Binti Raqiqa amesema: Nilikwenda kwa Mtume S.A.W. akiwa na wanawake wakitoa kiapo cha utii wakasema: Tunakutii wewe Mtume wa Mwenyezi Mungu kuwa hatutamshirikisha Mwenyezi Mungu na chochote wala hatutaiba wala kuzini wala kuuwa watoto wetu au kuonesha mapambo yetu ya mikononi na miguuni wala hatutakuasi katika jema, Mtume S.A.W. akasema: “Kwa yale mliyoyaweza na kuyatamka” nikasema: Mwenyezi Mungu na Mtume wake ni wenye huruma sana na sisi kuliko sisi wenyewe, haya tumtii Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mtume S.A.W. akasema: “Kwa hakika mimi sipeani mikono na wanawake bali kauli yangu kwa wanawake mia  ni kama kauli yangu kwa mwanamke mmoja au ni kama mfano wa kauli yangu kwa mwanamke mmoja”([15]).

Baadhi watafiti wa sasa wametoa maelezo juu ya Hadithi za huu Utiifu kwa Mtume S.A.W. kwa kusema: Hizi Hadithi zinatufahamisha kuwa Mtume S.A.W. hakuwahi kuwapa mkono wanawake katika kiapo cha Utii nazo ni tamko la wazi katika hilo, ikiwa Mtume S.A.W. hajawahi kuwapa wanawake mkono katika kiapo cha Utii basi ni bora zaidi kuwa Mtume hajawahi kuwapa mkono wanawake katika jambo lingine lisilo la Utiifu, kwani Mtume S.A.W. ni kutakaswa kwake kuacha kuwapa mkono wanawake, ni jukumu letu kuacha yaliyoachwa na Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. kwa sababu yeye ni kigezo chetu([16]).

Hadithi iliyopokelewa na At-Tabarani kutoka kwa Maakal Ibn Yasar anasema: Mtume S.A.W. amesema: “Mtu kuchomwa na sindano ya chuma kichwani ni bora zaidi kuliko kumgusa mwanamke si halali yake kumgusa” na katika tamko lingine: “Kuchomwa na sindano ya chuma kichwani kwa mwanamume ni bora kwake kuliko kumgusa mwanamke si halali kwake kumgusa”([17]).

Mundhiri amesema: Hadithi imepokelewa na At-Tabari pamoja na Baihaqy, na watu wa At-Tabari ni wenye kuaminika na sahihi([18]), na Haithami amesema: Imepokelewa na At-Tabarani na watu wake ni sahihi([19]).

Kutoka kwa Abi Huraira kutoka kwa Mtume S.A.W. amesema: “Imeandikwa kwa mwanadamu sehemu yake ya uzinifu na atakifikia tu, kwani macho mawili kuzini kwake ni kuangalia, masikio mawili kuzini kwake ni kusikiliza, ulimi kuzini kwake ni maneno, mkono kuzini kwake kupora, mguu kuzini kwake kutembea, moyo unapenda na unatamani na hilo kukubaliwa na tupu na kukataliwa”([20]).

Imamu An-Nawawi anasema maana ya Hadithi ni kuwa: “Mwanadamu amekadiriwa sehemu ya uzinifu, miongoni mwao zinaa yao inakuwa ya kweli kwa kuingiza uchi ndani ya uchi wa haramu, wengine uzinifu wao ni wa maana ya fumbo kwa kuangalia kilicho haramu kuangalia, au kusikiliza ya uzinifu na yanayohusiana na kufikiwa kwa uzinifu, au kwa kugusa kwa mkono kwa kumgusa kwa mkono wake mwanamke si ndugu au kumbusu, au kwenda kwa miguu kwenye uzinifu, au kuangalia, au kugusa, au mazungumzo haramu na mwanamke si ndugu na mfano wa hayo, au kufikiria moyoni, yote haya ni katika aina za uzinifu wa fumbo, na tupu inakubali yote hayo au kuyakataa, maana yake: Ni kuwa inaweza kufikiwa zinaa kwa kutumia tupu na inaweza isifikiwe  kwa kuingiza tupu ndani ya tupu. Mwenyezi Mungu ndiye Anayejua zaidi.

Kisha ikanukuliwa kauli ya Ibn Abbas katika mapokezi mengine ndani ya Sahihi mbili: Sijawahi kuona kitu kinachofanana sana na dhambi ndogo kama alivyosema Abu Huraira kwa maana yaliyomo kwenye Hadithi miongoni mwa dhambi za kutazama kugusa na mfano wake, na kati ya tafasiri yake ya dhambi ndogo hivyo akasema: Maana yake ni tafasiri ya kauli ya Mola Mtukufu: {Ambao wanajiepusha na madhambi makuu na vitendo vichafu, isipokuwa makosa mepesi. Hakika Mola wako Mlezi ni Mkunjufu wa msamaha} An-Najmi: 32. “Maana ya Aya na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kujua zaidi: Ni wale ambao wanajiepusha na maasi isipokuwa yale mepesi husamehewa maasi hayo, kama ilivyokuja katika kauli ya Mwenyezi Mungu: {Mkiyaepuka makubwa mnayo katazwa, tutakufutieni makosa yenu madogo} An-Nisaai: 31. Maana ya Aya hizi mbili: Ni kuwa kujiepusha na kufanya makosa makubwa kunaleta msamaha wa makosa madogo, nayo ni yale makosa mepesi, na Ibn Abbas akafasiri yaliyomo kwenye Hadithi miongoni mwa kuangalia kugusa na mfano wake, nayo ni kama alivyosema, hii ndiyo maana sahihi katika tafsiri ya makosa madogo”([21]).

Kumpa mkono mwanamke si ndugu ni kishawishi cha fitina: Si jambo lenye kukubalika Sharia kuharamisha kitu kisha ikafanya sababu inayopelekea kwenye haramu hiyo ni halali, wala haina shaka kwa yeyote aliyesawa kuwa mwanaume kugusa kitu katika mwili wa mwanamke si ndugu kama hali ilivyo katika kupeana mkono ni kishawishi cha fitina, na kupeana mkono na mwanamke wa mbali kumeharamishwa kwa sababu ni utangulizi na njia ya kuelekea kumfitinisha mwanamke.

Uislamu umeaharamisha kumuangalia mwanamke si ndugu pasina sababu za Kisharia, basi kumgusa ndiyo mbaya zaidi, kwa sababu kumuangalia ni kudogo zaidi ya kumgusa, na kumgusa kuna athari kubwa zaidi katika nafsi kuliko kumuangalia, kwani kugusa kunapelekea matamanio na kuyachemsha zaidi kuliko kuangalia.

Imamu An-Nawawi amesema: “Wamesema watu wetu: Kila kilichoharamishwa kuangaliwa ni haramu kugusa, bali kugusa ndiyo mbaya zaidi, kwani kuna uhalali wa kumuangalia mwanamke ikiwa mtu anataka kumuoa, na katika hali ya kuuza na kununua kuchukua na kutoa na mfano wa hayo, haifai kumgusa mwanamke katika hayo”([22]).

Hivyo basi kipimo cha kuzuia kugusa na kipimo cha kuangalia ni katika kipimo cha kipaombele ni: Kilichokuwa tawi ni bora zaidi kuhukumiwa kutokana na asili kwa sababu ya uwepo wa nguvu ya sababu, mfano: Aina ya kipimo cha machungu ya maudhi basi kuharamisha ni bora zaidi kwa sababu ya uzito wa kero([23]), na kugusa ni mbaya zaidi kuliko kuangalia, na Imamu Ar-Ramli amesema katika sherehe ya Minhaj: “Ikiwa imeharamishwa kuangalia basi imeharamishwa kugusa” kwa sababu kugusa kunaibua matamanio zaidi ambapo ikiwa mtu aliyefunga atatoa maji ya uzazi basi anakuwa amefungua, tofauti na kuangalia ikiwa atateremsha maji ya uzazi hafungui”([24]).

Rai ya Dkt. Al-Qaradawi

Mwanachuoni Dkt. Yousuf Al Qardhawi anasema kuwa hakuna dalili toshelezi iliyotamkwa na kuonesha uharamu wa kupeana mikono ikiwa kama hakuna matamamio, na dalili kubwa inayochukuliwa hapa ni kule kuzuia fitina, hili ni jambo linalokubalika bila ya shaka yeyote pale inapopelekea hamasa ya matamanio, au wasi wasi wa fitina kwa kuwepo viashiria vyake, lakini kunapokuwepo usalama wa hilo na hili linafikiwa zaidi ya mtazamo wa kuharamisha([25]).

Akazungumzia baadhi yanayochukuliwa dalili ya kuzuia kumpa mkono mwanamke wa mbali kama vila dalili ya Mtume S.A.W. kuacha kutoa mkono kwenye kiapo cha Utii na kwa sababu hiyo imezuiliwa moja kwa moja, ifahamike kuwa Mtume S.A.W. kuacha jambo kulifanya haina maana ya uharamu wa hilo jambo…kwani ni kweli anaweza kuacha kwa sababu ni haramu, na wakati mwingine anaacha kwa sababu ni jambo lisilopendeza, na anaacha kwa sababu tu hapendi kama kuacha kwake kula kenge pamoja na kuwa ni halali.

Maelezo ya Sheikh Kardhawi anayapa nguvu kwa sababu Mtume S.A.W. amesema: “Kwa hakika mimi sipokei zawadi ya mtu mshirikina”([26]), lakini aliwahi kupokea zawadi ya mshirikina sehemu nyingine, kwani alikubali zawadi kutoka kwa Al-Muqawqis mfalme wa Wakopti ambapo alipewa zawadi ya wajakazi wawili akiwemo Bi. Maria Coptic mama wa mtoto wake Ibrahim na kuongezea pia zawadi ya mnyama aina ya nyumbu([27]), kisha hiyo ni ruhusa ya Mtume S.A.W. ya kutopokea zawadi ya mshirikina inayobeba hali maalumu, vilevile na sisi kwa upande wa kauli yake S.A.W.: “kwa hakika yangu siwapi mkono wanawake”.

Kitendo cha Mtume S.A.W. kuacha tu hakupelekei uharamu, lazima kuambatane na dalili nyingine, katika hili turejee maelezo ya Mwanachuoni Sheikh Abdillah Ibn Siddiq Al-Khabari kwenye kitabu cha “Uelewa mzuri na ufahamu wa masuala ya kuacha” ndani yake kuna maelezo ya kina zaidi kuhusu hii maudhui.

Na pia akasema: Mtume S.A.W. kuacha kuwapa mikono wanawake katika viapo vya Utii sio jambo la makubaliano, kwani yamekuja maelezo kutoka kwa Ummu Atiya Al-Ansaar yanayonesha utoaji mkono katika kiapo cha Utii, tofauti na maelezo yaliyosahihishwa kutoka kwa Mama wa Waumini Bi. Aisha R.A. ambapo amepinga hilo na akaapa juu ya kulikanusha.

Imepokelewa kutoka kwa Ibn Habban na Bazzar kwa njia ya Ismail Ibn Abdulrahman kutoka kwa bibi yake Mama Atiya kisa cha kiapo cha Utii, amesema: Alinyosha mkono wake kutoka nje ya nyumba, na tukamnyoshea mikono yetu kutoka ndani ya nyumba, kisha akasema: “Ewe Mwenyezi Mungu ninashuhudia”([28]). 

Vilevile katika Sahihi ya Imamu Bukhari kutoka kwa Ummu Atiya R.A. amesema: Tuliapa kiapo cha Utii kwa Mtume S.A.W. kisha akatusomea:{Kutomshrikisha Mwenyezi Mungu kwa chochote} na akatukataza maombolezo kuna mwanamke akashika mkono wake na akasema: Nimefurahishwa na fulani ninataka kumpa zawadi yake, Mtume S.A.W. hakumwambia kitu chochote, akaondoka na akarejea na kutoa kiapo cha Utii([29]), jumla inayosema: “Mwanamke akashika mkono wake” inaleta maana kuwa wanawake walikuwa wakitoa viapo vya Utii kwa mikono yao.

Hafidhi amesema katika kitabu cha Al-Fat’hu: Inawezekana jibu la maelezo ya kwanza ni kuwa, kutoa mkono wakiwa nyuma ya pazia ni ishara ya kufanyika kiapo cha Utii hata kama haikutokea kupeana mikono…na jibu la maelezo ya pili: Ni kuwa kusudio kushika mkono: Ni kuchelewa kukubali… au kiapo cha Utii kilikuwa kinafanyika kwa kuwepo kizuizi, kwani Abu Daud amepokea katika kitabu cha Al-Maraasiil kutoka kwa Shaaby kuwa Mtume S.A.W. pindi wanawake wanapotoa kiapo cha Utii huja na kitu na kukiweka kwenye mkono wake na akasema: “Siwapi wanawake mikono” na kwa Mughazi Ibn Is-haq: Ni kuwa Mtume S.A.W. alikuwa anaingiza mkono wake kwenye chombo  chenye maji na kuingiza pamoja na mkono wa mwanamke, na akasema: Inawezekana kuwa na kauli nyingi([30]).

Maana yake: Kiapo cha Utii kimefanyika mara nyingi, miongoni mwa mara hizo hajawahi kabisa kugusa mkono wa mwanamke ima kwa kuwepo kizuizi au bila kuwepo lakini kiapo cha Utii kilikuwa kwa maneno tu, nayo ni yaliyoelezewa na Bi. Aisha R.A….na katika hali nyingine aliwapa mikono wanawake kwa kuwepo kizuizi, hayo ni katika maelezo yaliyopokelewa na Shaaby… ikiwa ni pamoja na sura ambayo Ibn Is’haq ameitaja ya kuingiza mkono kwenye chombo cha maji, na sura ambayo inaonekana kupitia maelezo ya Ummu Atiya ya kupeana mikono moja kwa moja,  hasa maelezo yanapokuwa ya ukweli na wala si ya fumbo, na katika yanayoimarisha hayo ni maelezo ya Imamu Ahmad katika kitabu chake, kutoka kwa Ummu Atiya: Kuwa Mtume S.A.W. aliwaamrisha wanawake wasiiname, mwanamke mmoja akasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu hakika kuna mwanamke amenifurahisha je sipaswi nami kumfurahisha, akamshika mkono wake na Mtume S.A.W. akashika mkono wake wala hakutoa kiapo cha Utii([31]), na yanayoipa nguvu haya ni pamoja na yaliyopokelewa na kutoka kwa Bi. Aisha R.A. kuwa Hindu Binti Atabah amesema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu nipe mkono wa kiapo, Mtume S.A.W. akaangalia mkono wake akasema: “Siwezi kukupa mkono wa kiapo mpaka ubadilishe kiganja chako”([32]), na inatiliwa nguvu pia na maelezo yaliyotolewa na Al-Hafidh Ibn Katheer katika tafasiri yake kutoka kwa Ibn Abi Hatim kuwa Bi. Aisha R.A. alisema: Hindu binti Utuba alikuja kwa Mtume S.A.W. ili kumpa kiapo cha Utii, kisha Mtume S.A.W. akangalia mkono wa Hindu na akasema: “Nenda na ubadilishe mkono wako”, hivyo akaondoka na akabadilisha kwa kupata hina kisha akarudi tena, ndipo Mtume S.A.W. akasema: “Nakupa kiapo cha kutomshirikisha Mwenyezi Mungu kwa chochote” hivyo Bi. Hindu akala kiapo hiko na mkononi mwake akiwa na vikuku viwili vya dhahabu, Hindu akauliza: “Unasemaje kuhusu hivi vikuku viwili? Akasema: “Ni sehemu mbili za moto wa jahanamu”([33]).

Muongozo wa kubadilisha kiganja cha mkono kwa kupaka hina kunaweza pelekea uwezekano wa kupeana mikono.

Jambo linalotoa uzito wa kuwepo uwezekano mbalimbali: Ni kuwa Bi. Aisha anazungumzia kiapo cha Waumini wa kike waliohama baada ya suluhu ya Hudaibia mbele ya Ummu Atiya akizungumza kuhusu yanayonekana mapana zaidi ya kiapo cha Utii cha wanawake Waumini kwa ujumla, miongoni mwao ni pamoja na wanawake wa Madina kama vile Ummu Atiya mpokezi wa Hadithi…na haya Imamu Bukhari alifasiri Hadithi ya Bi. Aisha kwa anuwani, mlango: (Pindi wanapowajieni wanawake Waumini wenye kuhama), na Hadithi ya Ummu Atiya kwa mlango: (Pindi wanapokujia wanawake Waumini wakikupa kiapo).

Ninaongeza na kusema:  Mchunguzaji wa kina katika Hadithi hizi kwa maana Hadithi za kiapo cha Utii kama vile Hadithi ya Bi. Aisha na Ummu Atiya ataona tu ni wasifu wa ukweli, na kukugundua kuwa haifai kuwa ni ushahidi wenye nguvu wa moja kwa moja wa kuharamisha kuwapa mikono wanawake, kwa kuwa Mama wa Waumini anakanusha upeaji mkono bila ya kulifanya ni kosa kubwa, kujizuia kwake tu Mtume S.A.W. kuwapa mikono wanawake hakumaanishi ni haramu. Kama vile Mama wa Waumini hakuelezea kumaliza kwa Mtume S.A.W. kitendo kwa maelezo ya kumalizika kwa kilichoharamu, kwa maana mapokezi hayakuelezea uwepo wa kiingizi cha kusema kama (Ninajilinda kwa Mwenyezi Mungu kufanya hiki), au kiingizi cha hali kama vile (Kukasirika kwa upande wa Mama wa Waumini) vinavyonesha kwa uchache uharamu wa kitendo ambacho amekiacha Mtume wetu aliyezuiliwa kufanya dhambi S.A.W. lakini upokeaji wake ulikuwa unalenga kukataa sawa uelewa wake, kukataa kwake R.A. hakumaanishi uthibiti wa uharamu zaidi ya kuonesha kutotokea, bali inachukuliwa uwezekano wa kutokea utoaji mkono wake S.A.W. kama maana iliyopita katika Hadithi ya Ummu Atiya iliyopokelewa na Imamu Bukhari na Imamu Ahmad, kwani wote wamezungumza vile walivyoona au kufahamu, Mama wa Waumini Bi. Aisha R.A. kwa mfano amekanusha Mtume S.A.W. kujisaidia haja ndogo akiwa amesimama – kama ilivyokuja katika sunani na Musnad – amesema: Mwenye kukuambieni kuwa Mtume S.A.W. alikuwa anajisaidia haja ndogo akiwa amesimama basi msimwamini, kwani hakuwa akijisaidia haja ndogo isipokuwa alikuwa mwenye kuchutuma([34]). Lakini imekuja katika Sahihi mbili na vitabu vingine kutoka kwa Hudhaifa R.A. amesema: Mtume S.A.W. alikuja kwenye jalala na akajisaidia haja ndogo akiwa amesimama kisha akaitisha maji akaletewa na akatawadha([35]), ukweli ni kuwa wote Bi. Aisha na Hudhaifa wameelezea walichokiona na kufahamu katika matendo ya Mtume S.A.W. wala hakuna mgongano kati ya Hadithi mbili.

Makusudio ya kunukuu yote haya: Ni kuwa yaliyotegemewa na wengi katika kuharamisha kupeana mikono ni kule kuacha kwa Mtume S.A.W. kufanya hivyo katika viapo vya Utii vya wanawake, sio dalili ya moja kwa moja ya madai ya uharamu, lakini pia si katika maudhui iliyokubalika na wote, bali imekuwa na tofauti ambayo tumeitaja.

Ama kuhusu Hadithi: “Mtu kuchomwa kichwani sindano ya chuma ni bora kuliko kumgusa mwanamke bila ya kizuizi”. Sheikh Kardhawi amesema: Dalili iliyochukuliwa kuharamisha kumpa mkono mwanamke ni Hadithi ilitokana na At-Tabari pamoja na Al-Baihaqi kutoka kwa Maaqal Ibn Yasaar kutoka kwa Mtume S.A.W. amesema: “Kuchomwa kichwani na sindano ya chuma ni bora zaidi kuliko kumgusa mwanamke bila ya kizuizi”.

Hii Hadithi kuifanya dalili yanafahamika yafuatayo:

Maimamu wa Hadithi hawakuelezea usahihi wake, na wakatosheka tu kama vile Mundhiri au Al-Haithami kusema: Wapokezi wake ni watu wenye kuaminika au ni watu sahihi…. Na hili neno peke yake halitoshi kuthibitisha usahihi wa Hadithi kutokana na uwezekano wa kukatika mtiririko wa wapokezi au kuwepo kasoro iliyojificha, hivyo haikupokelewa na yeyote miongoni mwa Maimamu maarufu, kama vile haikufanywa dalili na Mwanachuoni yeyote wa Sharia wa zama za mwanzo juu ya uharamu wa kumpa mkono mwanamke na mfano wake.

Tuchukulie tumekubali usahihi wa Hadithi, na uwezo wa kuchukuliwa uharamu, tunakuta kuwa dalili ya Hadithi juu ya hukumu kinachofanyiwa dalili haipo wazi, kwani neno “Kumgusa mwanamke bila ya kuwepo kizuizi” halimaanishi kule kugusana tu ngozi kwa ngozi bila kuleta hisia ya matamanio, kama inavyokuwa katika kupeana mkono kikawaida…bali neno “Kugusa” kwa mujibu wa matumizi yake katika maandishi ya Kisharia ndani ya Qur'ani na Hadithi lina maanisha moja ya mambo mawili:-

Lenyewe ni fumbo linalokusudiwa mahusiano ya kijinsia “Kuingiliana” kama ilivyokuja kutoka kwa Ibn Abbas R.A. katika tafasiri yake kauli ya Mwenyezi Mungu: {Au mmewagusa wanawake} An-Nisaai: 43, amesema: Neno mguso kugusana na kugusa ndani ya Qur'ani ni fumbo kwa maana ya kuingilia([36])… na kutohoa Aya ambazo imekuja ndani yake neno kugusa zinaonesha kwa uwazi kama vile kauli ya Mwenyezi Mungu kupitia ulimi wa Bi. Maryamu: {Vipi nitampata mwana na hali hajanigusa mwanadamu?} Aal-Imran: 47. Na kauli yake Mola Mtukufu: {Na mkiwapa talaka kabla ya kuwagusa} Al-Baqarah: 237. Na katika Hadithi Mtume S.A.W. alikuwa akiwakaribia wake zake pasi na kuwagusa([37]).

Lenyewe lina maana isiyo na kujamiana ikiwa ni pamoja na kubusu kukumbatia na mfano wa hayo miongoni mwa mambo ya utangulizi wa kuingilia, na hii ni miongoni mwa yaliyokuja kutoka kwa baadhi ya waja waliotangulia katika kutafasiri neno kuingiliana: Al-Hakim amesema ndani ya kitabu cha Al-Mustadrak: “Wamekubaliana Imamu Bukhari na Muslim upokezi wa Hadithi mbalimbali ndani ya Sahihi mbili inaonesha kuwa kugusa ni bila ya kujamiiana.

Miongoni mwa Hadithi hizo: Ni Hadithi ya Abi Huraira: “Mkono zinaa yake ni kugusa”.

Na Hadithi ya Ibn Abbas: “Huenda umegusa”.

Na Hadithi ya Ibn Masoud Na shika Sala katika ncha mbili za mchana, inaonesha Hadithi iliyopokelewa na Masheikh wawili na wengine kutoka Hadithi ya Ibn Masoud na katika baadhi ya mapokezi yake: Kuwa mtu mmoja alikuaja kwa Mtume S.A.W. na kumuambia kuwa yeye amepatwa na mwanamke, ima kumbusu au kumgusa kwa mkono wake au kitu kingine, kana kwamba anaulizia kuhusu kafara yake, ndipo Mwenyezi Mungu Akataremsha Aya: {Na shika Sala katika ncha mbili za mchana na nyakati za usiku zilizo karibu na mchana. Hakika mema huondoa maovu} Huud: 114. Akasema: Zimebakia Hadithi sahihi katika tafasiri miongoni mwazo:

Kutoka kwa Bi. Aisha R.A. amesema: “Haipiti siku moja au chini ya siku isipokuwa Mtume S.A.W. alikuwa anatuzungukia sisi sote – kwa maana wake zake – hubusu na kuwagusa bila ya kuingilia, anapokwenda kwa yule ambaye mwenye siku zamu yake hubakia huko”([38]).

Kutoka kwa Abdillah Ibn Masoud R.A. katika maana ya kauli ya Mola Mtukufu: {Au mmewagusa wanawake} An-Nisaai: 43 amesema: Mguso si kuingilia, na akasema: Kubusu ni katika kugusa, na kunapelekea kutawadha([39]).

Kutoka kwa Umar amesema: “Kubusu ni katika kugusa wanapaswa kutawadha kutokana na hilo”([40]).

Kutokana na haya madhehebu ya Imamu Malik na madhehebu ya Imamu Ahmad yanasema: Kumgusa mwanamke ambaye anapelekea kutenguka udhu ni kule kugusa kunakopelekea hisia za kutamani, na kutoka na mtazamo wamefasiri kauli ya Mola Mtukufu: {Au mmewagusa wanawake}.

Na kwa sura hii Sheikh wa Uislamu Ibn Taimiya amedhaifisha katika Fatwa zake kauli ya waliofasiri kugusana au kugusa ndani ya Aya kwa maana ya kugusa ngozi hata kama si kwa matamanio, miongoni mwa aliyoyasema katika hayo:-

“Ama maelezo ya kuvunjika udhu kwa kule kumgusa tu, maelezo ni tofauti na asili na tofauti na makubaliano ya Masahaba na tofauti na Hadithi, kwani msemaji wa haya hana andiko wala kigezo, ikiwa kugusa ndani ya kauli ya Mola Mtukufu: {Au mmewagusa wanawake} inakusudiwa kugusa kwa mkono kubusu na mfano wa hayo kama alivyosema Ibn Umar na wengine basi amefahamu kuwa imetajwa ndani ya Qur'ani na Hadithi lakini kusudio lake ni kule kugusa kunakoleta matamanio, mfano wa kauli yake Mola Mtukufu katika Aya ya Itikafu: {Wala msichanganyike nao na hali mnakaa Itikafu Msikitini} na kauli yake:{Hapana ubaya kwenu mkiwapa talaka wanawake ambao hamjawagusa} ni kuwa ikiwa atamgusa ugusaji usio na hisia za matamanio haipaswi kwake kukaa eda, wala mahari haibaki kwa mwanamke, wala hauenei uharamu wa ukwe kwa makubaliano ya Wanachuoni.

Mwenye kufikiria kuwa kauli yake Mola Mtukufu: {Au mmewagusa wanawake} kunaelezea kugusa hata kama kugusa kusiko na matamanio basi atakuwa ametoka nje ya lugha ambayo imekuja kwenye Qur'ani Tukufu, bali na hata lugha ya watu iliyozoeleka kwao, kwani pindi inapotajwa kugusa ambako kunaunganisha kati ya mwanamke na mwanamume imefahamika kuwa ni kugusa kwa matamanio, kama vile inapotajwa kuingilia kunakounganishwa kati ya mwanamume na mwanamke kumefahamika kuwa huko ni kuingilia kwa tupo na wala si kwa mguu([41]).

Ibn Taimia amesema sehemu nyingine: Kuwa Masahaba walivutana katika kauli ya Mola Mtukufu: {Au mmewagusa wanawake} An-Nisaai: 43, ambapo Ibn Abbas na kundi lingine walikuwa wanasema: Kuingilia, na wanasema: Mwenyezi Mungu yu hai na mkarimu, anaita atakavyo kile atakacho. Amesema: Hizi ndiyo kauli mbili sahihi. Waarabu na wasio Waarabu wamevutana katika maana ya neno kugusa: Je kusudio lake ni kuingilia au mambo ya kabla ya kuingilia? Waarabu wakasema: Kusudio ni kuingilia, na wasiokuwa Waarabu wakasema: Ni kabla ya kuingilia, wakataka kauli ya Ibn Abbas akapitisha kauli ya Waarabu, na kuikosesha kauli isiyo ya Waarabu([42]).

Kusudio la kunukuu haya maneno yote ni kufahamu kuwa neno “Kugusa” au “Guso” pindi mwanamume anapolitumia kwa mwanamke, hakusudii kugusisha ngozi na ngozi, bali kusudio ima kumuingilia au utangulizi wake kama vile kumpiga busu kumkumbatia na mfano wa hayo katika kila mguso unaofuatana na matamanio pamoja na kupata ladha.

Kama tutaangalia yale yaliyonukuliwa kwa Mtume S.A.W. ndani yake tutakuta yanayo maanisha kuwa kugusana tu mkono kwa mkono kati ya mwanamume na mwanamke bila ya kuwepo matamanio wala fitina ni jambo halizuiliwi, bali inachukuliwa kuwa Mtume S.A.W. alilifanya, na asili ya kulifanya ni kwa upande wa Sharia na kumwiga: {Hakika nyinyi mna kigezo chema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu} Al-Ahzaab: 21.

Amepokea Imamu Bukhari katika Sahih yake kutoka kwa Anas Ibn Malik R.A. amesema: “Ikiwa mjakazi katika wajakazi wa Madina atakuwa anahitaji kuchukua mkono wa Mtume S.A.W. basi atakwenda nao atakako”([43]). Na mapokezi mengine ya Imamu Ahmad kutoka kwa Anas pia amesema: “Ikiwa mjakazi katika wajakazi wa Madina atakuja na kuchukua mkono wa Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. basi Mtume S.A.W. hatauvua mkono wake mpaka aende nao popote atakapo”([44]).

Al-Hafidh amesema katika kitabu cha Al-Fat’hu: Kusudio la kuchukua mkono, ni upole na unyenyekevu, na imekusanya aina za viwango vya juu vya unyenyekevu, kwa kutajwa mwanamke pasina mwanamume, na mjakazi ni mwanamke asiye huru, ambapo limetumika neno mjakazi kwa maana ya mjakazi yeyote yule, na kauli yake “Popote atakapo” sehemu yeyote katika sehemu, na kuelezea kuchukua mkono ni ishara ya haja yake hata kama itakuwa nje ya mji, atapata msaada wake katika haja hiyo.

Na hii ni dalili ya unyenyekevu wake na kuepukana kwake S.A.W. na aina zote za kiburi([45]).

Yaliyoelezwa na Hafidh R.A. yanakubalika kwa ujumla wake, lakini matumizi yake maana ya kuchukua mkono kwa uwazi wake na kuambatana nao upole na unyenyekevu haikubaliki, kwa sababu inaweza kuwa uwazi na kuambatana ni maana moja…asili katika maelezo ni kuchukuliwa uwazi wake, isipokuwa kunapokuwepo dalili maalumu tofauti na huu uwazi, katika mapokezi ya Imamu Ahmad: “Mkono wa Mtume S.A.W. hautoacha mkono wa mjakazi na kwenda nao anapotaka” katika maelezo haya kuna ishara ya uwezekano wa kukusudiwa maana ya wazi.

Bali zaidi ya hayo ni maelezo yaliyokuja kwenye Sahihi mbili na Sunan kutoka kwa Abasi pia: “Kuwa Mtume S.A.W. alisema wakati wa mchana alipokuwa kwa shangazi wa Anas Ummu Haram binti Mulhaan mke wa Ibadatu Ibn Samit na alikuwa amelala akiwa ameweka kichwa chake kwenye mapaja yake na kuangusha kichwa chake….mpaka mwisho yaliyopokelewa kwenye Hadithi([46]).

Hafidh Ibn Hajar ametaja katika maelezo yatokanayo na Hadithi, amesema: “Ndani yake ni ruhusa kumuhudumia mgeni nje ya nyumba yake kwa sharti kama kuruhusu na kuwepo usalama wa fitina ... Na yafaa mwanamke si ndugu kutoa huduma kama ya chakula kumuandalia na mfano hayo.

Na mwanamke kumuhudumia mgeni kwa kumtikisa kichwa chake hili limekuwa na tofauti kwa Wanachuoni, Ibn Abdibarr amesema: Ninadhani kuwa Ummu Haramu alimnyonyesha Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. au dada yake Ummu Salim, wote wawili wakawa mama zake au mama zake wa kunyonya, kwa sababu hiyo ndiyo maana alikuwa analala kwake, na kupata yale yanayofaa kuyapata ndugu wa karibu kutoka kwa ndugu yake….kisha akaelezea yanayoashiria kuwa Ummu Haram alikuwa ni ndugu kwa upande wa shangazi zake kwa sababu mama wa mzee Abdul Mutalib babu wa Mtume S.A.W. mama yake ni katika ukoo wa Bani Najjar…..n.k.

Akasema mwingine: Bali Mtume S.A.W. alikuwa amezuiliwa kufanya dhambi, amekuwa na shaka kwa mkewe ni vipi kwa mwanamke mwingine ambaye ameepukana naye? Naye Mtume ameepukana na kila kitendo kiovu na kauli chafu hilo linakuwa ni maalumu kwake.

Kadhi Ayyadh amelijibu hilo kuwa umaalumu hauthibiti kwa kukisia, kuthibiti kwa kuzuiliwa kufanya dhambi kunakubalika lakini asili ni kutokuwa maalumu, kwani inafaa kumuiga katika vitendo vyake hata huo umaalumu uwe na dalili.

Al-Hafidh Dumyati akamjibu mwenye kusema uwezekano wa kwanza, nao ni madai ya uharamu akasema: Inashangaza kila mwenye kudhani kuwa Ummu Haramu ni mmoja wa shangazi wa Mtume S.A.W. anayetokana na kunyonya au nasaba, ambao wamehusika na kumnyonyesha Mtume S.A.W. wanafahamika hakuna hata mmoja katika wanawake wa Kiansar zaidi ya mama wa mzee Abdul Mutalib naye ni Salma binti Amru Ibn Zaidi Ibn Labid Ibn Kharash Ibn Amir Ibn Ghanam Ibn Ady Ibn Najjar, mama Haramu ni binti wa Mulhan Ibn Khalidi Ibn Zaidi Ibn Haramu Ibn Jandab Ibn Amir aliyetajwa….hawakutani kati ya Ummu Haramu na Salma isipokuwa kwa Amir Ibn Khalid Ibn Ghanam babu yao mkubwa…na huu ushangazi hauthibitishi uharamu, kwa sababu ni ushangazi si wa moja kwa moja, nayo ni kama kauli yake – S.A.W. – kwa Saad Ibn Abi Wiqaas: “Huyu ni mjomba wangu” kwa vile anatokana na ukoo wa Bani Zahara, nao ni ukoo uliokaribu na Mama yake Bi. Amina, na wala Saad si ndugu wa Amina si kwa nasaba wala kunyonya, kisha akasema: Ikiwa hili limekubalika basi imethibiti katika Sahihi kuwa Mtume S.A.W. alikuwa haingii kwa mwanamke yeyote isipokuwa kwa wakezake, na Ummu Sulaim, akaulizwa katika hilo akasema: “Ninamuhurumia, ndugu yake alipigana vita akiwa na mimi” kwa maana ya Haramu Ibn Mulhan…na aliuwawa siku ya Biir Mauna…

Ikiwa hii Hadithi imemuhusu Umma Sulaim mfano wake ni Ummu Haram aliyetajwa hapa…hao wawili ni dada na walikuwa kwenye nyumba moja, kila mmoja kati ya wawili hao kwenye hiyo nyumba Haram Ibn Mulhan ndugu yao walikuwa naye pamoja, sababu ni moja kwao wawili kama Hafidh Ibn Hajar alivyoelezea…

Imeongezeka sababu iliyotajwa kuwa Ummu Sulaim ndiyo mama wa Anas mtumishi wa Mtume - S.A.W. – imekuwa ni kawaida kuchanganyika tajiri na mtumishi wake pamoja na ndugu wa mtumishi pia, na kuleta heshima ambayo inapatikana baina yao.

Kisha Dumyati akasema: Pamoja na kuwa katika Hadithi hakuna dalili ya kuwa chemba na Ummu Haramu, huenda hilo lilikuwa na mtoto au mfanyakazi au mume au ndugu wa Ummu Haramu.

Ibn Hajar amesema: Nayo ni kauli yenye uwezekano mkubwa lakini haiondoi asili ya tatizo la kubakia kugusana katika kutikisa kichwa, vilevile kulala kwenye paja.

Al-Hafidh amesema: Jibu zuri la madai ya umaalumu, wala halijibiwi kuwa kwake hauthibiti isipokuwa kwa dalili kwa sababu dalili ya hilo lipo wazi sana na Mwenyezi Mungu anajua zaidi([47]). 

Sheikh Kardawi anasema: Ambalo ni sahihi katika haya mapokezi ni kuwa kumgusa tu si haramu…ikiwa kutapatikana sababu za kuchanganyika kama ilivyokuwa kati ya Mtume S.A.W. na Ummu Haram pamoja na Ummu Sulaim, na kukawa na usalama wa fitina kwa pande zote mbili, basi hakuna ubaya wowote wa kupeana mikono panapo hijtajika kama vile mtu kuja kutoka safari, mtu wa karibu anapotembelea ndugu zake au kutembelewa yeye, ambalo napenda kulisisitiza mwishoni mwa huu utafiti mambo mawili:

La Kwanza: Kupeana mikono kunafaa pale pasipokuwepo hisia za matamanio, usalama wa fitina, ikiwa itakosekana fitina kwa moja ya pande mbili, au kukawa na hisia za matamanio na ladha kwa mmoja wapo hakuna shaka kupeana mikono kwenye hali hiyo kutakuwa ni haramu.

Bali ikiwa haya masharti mawili yatakosekana la kukosekana hisia za matamanio na usalama wa fitina kati ya mwanamume na mwanamke aliye haramu kwake mfano shangazi yake au mama yake mdogo au dada yake wa kunyonya au binti wa mke wake au mke wa baba yake au mama wa mkewe au wasiokuwa hao, basi wakati huo kupeana mikono kutakuwa haramu, bali ikiwa yatakosekana masharti mawili kati ya mwanamke na mtoto mdogo wa kike pia kupeana naye mkono kutakuwa ni haramu, na huenda ilikuwa katika baadhi ya mazingira na kwa baadhi ya watu ni hatari zaidi kuliko mwanamke.

La Pili: Inapaswa kuhusisha katika kupeana mikono uwepo wa haja ya hilo, mfano kama ilivyokuja kwenye swali kama vile mtu wa karibu wakwe ambao kati yao kuna kuchanganyika na mahusiano makubwa, si vizuri kuongeza katika hilo kwa lengo la kuzuia kuingia kwenye haramu, na kuwa mbali na mazingira ya shaka, na kuchukua tahadhari. Lakini pia kumfuata Mtume S.A.W. na ni bora zaidi kwa Muislamu mwanaume na mwanamke wenye dini kutoanza mmoja wao kumpa mkono mwenzake, lakini ikiwa atapewa basi naye na atoe mkono.

Tumepitisha hukumu ili kufanyiwa kazi na mwenye kuhitaji pasi na kuhisi kuwa amevuka mipaka katika dini yake, wala kumpinga mwenye kumuona anafanya hivyo maadamu jambo lenyewe linakubali jitihada mbalimbali. Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua zaidi([48]). 

Huu ni ufupi wa utafiti wa Sheikh Kardhawy.

Ufupi wa Utafiti

Maelezo yaliyotangulia yanatubainikia kuwa kauli ya uharamu wa kupeana mikono kati ya mwanamme na mwanamke si ndugu ni kauli ya Jamhuri ya Wanachuoni wa Sharia, na kauli ya kuchukiza kupeana mikoni ni kauli iliyopokelewa kutoka kwa Imamu Ahmad, na baadhi ya Wanachuoni wa zama za sasa wameelezea kuwa inafaa moja kwa moja pale panapokosekana matamanio, na kila mmoja katika watu wa rai hizi ana egemezo la Kisharia.

Wanachuoni wameeleza kuwa inafaa kwa mwenye kuhofia kuingia katika haramu kuwafuata Wanachuoni waliopitisha ili kuachana na haramu, kwani kuna maeneo mawili: Eneo la kwanza: Ni eneo la haramu moja kwa moja, na eneo la pili: Ni eneo la haramu kwa mitazamo ambayo huenda imevuta mtazamo wa Wanachuoni, kwa kuwepo dhana katika dalili ya uharamu ni sawasawa kwa upande wa dalili au maana, eneo la kwanza sio ambalo tunakusudia, bali tunalokusudia ni eneo la pili, kwani kadhia ya uharamu kwa upande wa mwenye kufuata msemaji wake haichukuliwi kuwa upande wa dhana, na hii dhana inakabiliana na dhana nyingine katika kauli ya kufaa, hivyo kauli imekuja ya kufaa kufuata mtazamo wa mwana jitihada mwenye kusema inafaa, kwa sababu mwenye kufuatwa haizingatiwi kuwa amehama kutoka dhana moja kwenda dhana nyingine, na kauli mbili – sawasawa ya kuharamisha au kuhalalisha – zipo chini ya mwanvuli wa Sharia hakuna kauli inayoachana na mwanvuli huo wala kuwezekana kwa yeyote kupitisha kuwa kauli moja ndiyo hukumu ya Mwenyezi Mungu katika jambo hilo.

Miongoni mwa aliyeashiria sehemu ya hili ni Sheikh wa Uislamu Mwanachuoni Al-Baijuri katika kitabu chake cha Fiqhi – kwenye kauli ya kusherehesha: “Wala haifai pasina dharura kwa mwanamume au mwanamke kutumia chombo chochote cha dhahabu na madini ya fedha” – ambapo amesema: “Al-Balqini na Ad-Damiiry wamezingatia ni katika makosa makubwa, na akanukuu Al-Adhrai kutoka Jamhuri kuwa ni makoda madogo nayo ni kauli inayokubalika zaidi, na Daudi Dhahiry amesema: Inachukiza kutumia vyombo vya madini ya dhahabu na fedha uchukizo wa kuepukwa, nayo ni kauli ya Imamu Shafi katika Fiqhi yake ya zamani, na ikasema uharamu umehusishwa kwenye kula kunywa na si vinginevyo, ikiwa imechukuliwa sura ya nje ya Hadithi nayo inasema: “Wala msinywe kwenye chombo cha dhahabu wala fedha, wala msilie kwenye vyombo hivyo”, kwa upande wa Imamu Abu Hanifa kauli ya kufaa kwa dharura kubwa, japo kuwa kauli yenye nguvu kwao ni haramu, hivyo inapaswa kwa mwenye kukubaliana na hayo kama inavyokuwa kwa wengi kufuata yaliyoelezwa ili kumaliza uharamu”([49]).

Haina maana kauli yetu ya kufaa kufuata mhalalishaji ni kuwa sisi tunapitisha kwa yeyote kutoka kwenye eneo la Sharia bali makusudio ya haya ni kusahihisha matendo ya watu na mashirikiano yao kadiri inavyowezekana, na mtu atangulize kufanya kitu akiwa na mwelekeo unaofaa Kisharia ni bora kwake kuliko kufunga mbele yake milango yote bila kukuta mbele yake njia isipokuwa ni kuvamia mtazamo wa haramu.

Masuala ya kupeana mikono kwa huu mlango ikiwa hakuna matamanio na kuna usalama wa fitina basi anaweza kupanua nafsi yake kwa kufuata mtazamo wa kufaa, wakati huo hakuna ubaya kwake wala dhambi.

Naye Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mjuzi Zaidi

Imeandikwa Na:

Mustafa Abdul Kareem Muhammad

 28/06/2007.

 

([1]) Kitabu cha As-Sihah: Sehemu ya kupeana mikono, 1/385.

([2]) Kitabu cha As-Sihah: Sehemu ya kupeana mikono, uk. 342.

([3]) Kitabu cha Fat-h Al-Bari 11/54.

([4]) Kamusi elezi ya Fiqhi chapa ya Kuweit 19/267.

([5]) Kitabu cha sherehe ya An-Nawawi 9/105.

([6]) Sahih Muslim 1445, 1447.

([7]) Kitabu cha Tabyiin Al-Hakaik sherehe ya Kanzu Dakaik 6/18. Zailai amesema katika kitabu cha Nasbi Raya katika upokezi wa Hadithi za uongofu 6/128 Hadithi iliyotajwa, pia amesema kutoka kwa Abi Bakri na Ibn Zubeir R.A. na Al-Hafidhi Ibn Hajar akasema katika Hadithi ya uongofu 2/224 katika Hadithi iliyotajwa.

([8]) Kitabu cha Imamu Sawy cha sherehe ndogo cha Sheikh Dardiry 4/760

([9]) Kitabu cha Nihayatul-Muhtaaj sherehe ya Minhaaj 6/191, 192.

([10]) Kitabu cha Hashiyatu Sharwany 7/198.

([11]) Kitabu cha Kashaafu Al-Qinaai kutoka matini ya Al-Iqnaai 2/154, 155. Na kitabu cha Adaabu Sharia cha Ibn Muflah 2/257, 258, pia kitabu cha Ghidhaaul-Al-baab katika sherehe ya muundo wa adabu cha Safariiny 1/325.

([12]) Wamekubaliana wapokezi wa Hadithi: Inapatikana kwenye Sahih Bukhari Hadithi nambari 4983, na katika Sahih Muslim Hadithi nambari 1866 na tamko la Imamu Bukhari.

([13]) Kitabu cha Fat-h Al-Bari 8/636.

([14]) Sherhu An-Nawawi, 13/13.

([15]) Sunani At-Tirmidhi Hadithi nambari 1597. Sunani An-Nisaai Hadithi nambari 4181. Sunani Ibn Maja Hadithi nambari 2874. Sahihi Ibn Habban Hadithi nambari 417/10. Kitabu cha Muutaa Malik Hadithi nambari 982/2. Musnad Ahmad Hadithi nambari 357/6. Kitabu cha Muujamul-Kabeer cha At-Tabarani Hadithi nambari 186/24. Kitabu cha Daar Qutny Hadithi nambari 147/4. Na tamko la Habban.

([16]) Kitabu cha Dalili za Kisharia juu ya uharamu wa kumpa mkono mwanamke asiyendugu, cha Dkt. Hussam Deen Afanah.

([17]) Kitabu cha Muujamul-Kabeer cha At-Tabarani, 20/211, 212.

([18]) Kitabu cha Targhiibu wa Tarhiib 3/26, wala hajaelezea ndani ya kitabu cha Sunani Al-Kubraa wala kwenye kitabu cha Shuabu Al-Iman katika vitabu vya Baihaqy.

([19]) Kitabu cha Majmaa Zawaaid 4/326.

([20]) Imekubaliwa na wapokezi wote wa Hadithi: Kwenye kitabu cha Sahih Bukhari Hadithi nambari 5889. Na kitabu cha Sahihi Musilmu Hadithi nambari 2657. Na tamko ni lake.

([21]) Sherehe ya An-Nawawi ya Sahih Muslim 16/206.

([22]) Kitabu cha Al-Adhkaar, uk. 266.

([23]) Kitabu cha Misingi ya Sharia cha Muhammad Abi Nuur Zuheir - Mungu Amrehemu – 4/259, 260.

([24]) Kitabu cha Nihaayatul-Muhtaaj, sherehe ya Minhaaj 6/195.

([25]) Fatawa Muaasira 2/291 na kuendelea.

([26]) Kitabu cha Muujamu Al-Kabeer cha Imamu At-Tabari 19/70, 71. Haithimi amesema katika kitabu cha Majmaa Zawaaid 6/126: “Wapokezi wake ni watu sahihi”.

([27]) Kitabu cha Mustadriku cha Hakim 4/41. Na kitabu cha Muujamu Al-Kabeer cha At-Tabari 24/306. Na Haithami amesema pia kwenye kitabu cha Majmaa Zawaaid 4/103: “Imepokelewa na Bazzar pamoja na At-Tabari katika kitabu cha Al-Awsat, na watu wa Bazzar ni watu sahihi”.

([28]) Sahihi Ibn Habban 7/313. Na Musnad Bazzar 1/374.

([29]) Sahih ya Imamu Bukhari Hadithi nambari 4610.

([30]) Kitabu cha Fat-h Al-Bari sherehe ya kitabu cha Sahih Bukhari 8/636. 637.

([31]) Musnad Ahmad 6/408.

([32]) Sunan Abi Daud 4165.

([33]) Tafasiri ya Qurani Tukufu 8/99 nayo ni ushahidi wa Hadithi iliyokuja hapo mwanzo, na Hadithi hii imepokelewa pia na Abu Yaala katika kitabu chake 8/194, na ameizungumzia Al-Haithami katika kitabu cha Majmaa Zawaaid.

([34]) Sunan At-Tirmidhi Hadithi nambari 12. Na Sunani An-Nisaai Hadithi nambari 29.

([35]) Imekubaliwa na Maimamu wa Hadithi: Ktika sahihi Bukhari ni Hadithi ya 222. Sahih Muslim Haidithi ya 273.

[36] Tafasiri ya Qurani Tukufu ya Ibn Katheer 2/314. Kitabu cha Sahih Bukhari, 5/1962.

[37] Sunan Abi Daud 2135. Na kitabu cha Musnad cha Ahmad 6/107.

[38] Kitabu cha Mustadraku juu ya sahihi mbili cha Hakim 1/228. Na Sunan Al-Kubraa cha Baihaqy 7/300.

([39]) Kitabu cha Mustadrak juu ya sahihi mbili cha Hakim 1/228. Kitabu cha Jaamii Al-Bayaan cha Ibn Jarir At-Tabari 8/393.

([40]) Kitabu cha Mustadrak juu ya sahihi mbili cha Hakim 1/228, 229.

([41]) Majmuui Al-Fatawa 21/233. 234.

([42]) Majmuui Al-Fatawa 21/237.

([43]) Sahihi Bukhari 5724.

([44]) Musnad Ahmad 3/174.

([45]) Kitabu cha Fat-h Al-Bari sherehe ya kitabu cha Sahihi Bukhari 10/490.

([46]) Imekubaliwa na wapokezi wote: Kwenye kitabu cha Sahih Bukhari Hadithi nambari 2636, 6600. Sahih Muslim Hadithi nambari 1912.

([47]) Kitabu cha Fat-h Al-Bari sherehe ya kitabu cha Sahih Bukhari 11/77: 79.

([48]) Fatawa Muasara 2/301, 302.

([49]) Kitabu cha Mwanachuoni Al-Bajuri sherehe ya Ibn Kassim Al-Ghuza kweye matini ya Abi Shujaa 1/41.

Share this:

Related Fatwas