Utukufu Ukubwa wa Lengo na Ukuu wa...

Egypt's Dar Al-Ifta

Utukufu Ukubwa wa Lengo na Ukuu wa Madhumuni

Question

Vipimo vya utukufu havipimwi kwa wingi wa mali au wafuasi, wala kwa ukubwa wa ufalme, ushawishi wa utawala, au nguvu ya hadhi. Bali, utukufu hupimwa kwa ukarimu wa nafsi, utakaso wa maadili, na ukubwa wa athari zinazoendelea. Sifa hizi zote zilikusanyika kwa Mtume mtukufu (S.A.W). Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

Answer

Vipimo vya utukufu havipimwi kwa wingi wa mali au wafuasi, wala kwa ukubwa wa ufalme, ushawishi wa utawala, au nguvu ya hadhi. Bali, utukufu hupimwa kwa ukarimu wa nafsi, utakaso wa maadili, na ukubwa wa athari zinazoendelea. Sifa hizi zote zilikusanyika kwa Mtume mtukufu (S.A.W). Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

(Yeye ndiye aliye mpeleka Mtume kwenye watu wasio jua kusoma, awasomee Aya zake na awatakase, na awafunze Kitabu na hikima, ijapo kuwa kabla ya haya walikuwa katika upotofu ulio dhaahiri.) [Al-Jumu'ah: 2]

Yeyote anayeitazama tabia ya Mtume (S.A.W), atajikuta mbele ya tabia yenye pande za utukufu ambazo zinaonesha mfano adimu na wa kipekee. Hili linathibitishwa na wema wake na urekebishaji wake, ambavyo vilikuja bila mfano wowote. Ushuhuda tosha wa hili ni mabadiliko aliyoyaleta katika dunia ya wanadamu; kwayo aliurudisha ubinadamu kwenye njia sahihi na na uongofu wake.

Mtume (S.A.W) alitumwa katika wakati ambapo mizani ilikuwa imepotoka, mambo yalikuwa yamebadilika, haki na wajibu zimepotea. Mpaka ikiwa ni sahihi, kusema kwamba alitumwa katika wakati ambapo hakukuwa na "umma wenye tabia njema, wala jamii iliyojengwa juu ya maadili na wema, wala serikali iliyojengwa juu ya haki na huruma, wala uongozi uliojengwa juu ya elimu na hekima, wala dini sahihi iliyotoka kwa Manabii." ([1]).

Katikati ya haya yote, Mtume (S.A.W) alikuwa bila kuathiriwa na imani za mazingira yake wala desturi za kabila lake. Tangu mwanzo, alihakikisha kujiepusha na desturi hizi za kipagani na kujitenga na tabia zisizofaa ambazo akili ya kawaida na asili ya binadamu inazikataa. Kwa sababu hii, alikulia akiwa na asili safi, tabia njema, na sifa za heshima na matendo matukufu zilikua ndani yake. Maisha yake, yenye maana kubwa, maadili mema, na mfano bora, yakawa mwongozo kwa wale wanaotafuta maadili yaliyokamilika, maadili kamili, ubinadamu katika sifa zake, uongozi katika njia yake sahihi, na ushujaa katika uzuri wake. Hivyo, alikuwa mfano bora na kamilifu zaidi. Na kwa sababu hiyo, Mwenyezi Mungu Mtukufu alijumuisha kati yake na Kitabu chake katika aya moja:

(Enyi Watu wa Kitabu! Amekwisha kujieni Mtume wetu anaye kufichulieni mengi mliyo kuwa mkiyaficha katika Kitabu, na anaye samehe mengi. Bila shaka imekujieni kutoka kwa Mwenyezi Mungu nuru na Kitabu kinacho bainisha) [Al-Ma'ida: 15].

Imamu At-Tabari anasema: "'Nuru' anamaanisha Muhammad (S.A.W) ambaye Mwenyezi Mungu amefanya haki kung'aa kupitia yeye, na Uislamu ukafunuliwa kupitia yeye, na ushirikina ukafutika kupitia yeye. Hivyo, yeye ni nuru kwa yeyote anayetaka kuongoka, anaibainisha haki." ([2])

Tabia yake (S.A.W) ilikuwa tukufu kwa maana zote za neno hilo, na utukufu huu uliathiri kila upande wa maisha yake. Hili lilimfanya awe mfano wa kuigwa na kufuatwa. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

(Hakika nyinyi mnayo ruwaza njema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwa anaye mtaraji Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho, na akamkumbuka Mwenyezi Mungu sana.) [Al-Ahzab: 21].

Yeyote anayetafiti pande za utukufu katika maisha yake (S.A.W) atazikuta zikiwa nyingi zaidi ya kuhesabika na tukufu zaidi ya kudhibitika. Inatosha kwa mtu kuzingatia baadhi yao, kama ifuatavyo:

Utukufu wa Lengo na ukubwa wake

Mtume (S.A.W) aliainisha lengo lake tangu mwanzo wa utume wake, ambalo lilikuwa kuirejesha binadamu kwenye asili yao, na kuwaongoza kwenye njia inayowarekebisha na kuwafahamisha hadhi na cheo chao, haswa kwa sababu alitumwa katika wakati ambapo giza na dhulma viliitawala dunia kote. Sheikh Ahmed Deedat anaelezea hali za ulimwengu na historia yake tangu mwanzo wake hadi leo kwa usahihi akisema: "Wakati ambao Mwenyezi Mungu Mtukufu alimuamuru Mtume wake wa mwisho, Muhammad (S.A.W), atangaze ujumbe wake kwa wanadamu, ulikuwa ni wakati wa giza kubwa."

"Kulikuwa na haja kubwa ya mojawapo ya mambo mawili: ama kutuma nabii wa mwisho kwa kila pembe na kila taifa la ulimwengu, au kutuma nabii wa mwisho kwa wanadamu wote katika kila taifa na pembe ya ulimwengu; ili aweze kuwaokoa na kuwakomboa wanadamu wote kutoka kwenye udanganyifu, ushirikina, ubinafsi, miungu wengi, upotofu, dhulma na ukandamizaji wa mwanadamu kwa ndugu yake mwanadamu, na ili ujumbe wa Nabii wa mwisho uwe umetoka kwa Mwenyezi Mungu na uelekezwe kwa binadamu wote."

"Na ilipendeza kwa hekima na mapenzi ya Mwenyezi Mungu kumchagua Mtume Muhammad (S.A.W) kwa ajili ya ujumbe huu wa mwisho. Na alitoka kwenye maeneo ya giza zaidi duniani kabla ya utume wake, kutoka kwenye rasi ya Kiarabu. Ukweli huu - kwamba ujumbe wa Nabii wa Uislamu ulikuwa ujumbe kwa wanadamu wote - uliandikwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Qur'ani tukufu, aliposema:

(Nasi hatukukutuma ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote.) [Al-Anbiya: 107].  ([3])

Kinachoshangaza ni pale mwanadamu anapojidharau, kushusha umuhimu wake na hadhi yake, na kutafuta kiumbe aliye chini yake ambaye atampa utii na kumwabudu. Kisha anaamini kuwa anaweza kupata uongofu na hekima kupitia kiumbe huyo. Hili na mambo mengine hayalingani na ukamilifu wa uumbaji wa Mwenyezi Mungu, ambao aliuweka kwa ajili ya kiumbe chake kitukufu zaidi, na kiumbe cha juu cha ulimwengu wake. Mwenyezi Mungu amemfanya mwanadamu kuwa mtawala wa kila kitu katika ulimwengu huu, vitu vya juu na vya chini, na amemkirimu kwa neema zake za ndani na za nje; ili aweze kutimiza majukumu yake, kutimiza uwepo wake, na kufaidika na ulimwengu huu ili kufikia furaha na uongozi kwa ajili yake na kwa ajili ya wanadamu wenzake.

Mwanadamu alijidharau mwenyewe alipopindua mizani ya ulimwengu, na kukifanya kile alichodhalilishiwa kuwa kuwa mungu. Jambo hili lilimfanya yeyote mwenye akili hata kidogo ahukumu kwamba wafanyao hivyo hawana hekima, hawana akili na wameharibikiwa na hali ya maumbile, tabia zao zimepotoka, na njia yao ni ya upotevu.

Ujumbe huu wa Muhammad (S.A.W) ulikuja katika wakati wake na sehemu yake, na lengo lake kuu lilikuwa kuheshimu utu wa binadamu, na kulinda tabia ya ubinadamu. Nao ulijumuisha "kuwajulisha wanadamu hadhi yao, na kumpa kila mtu haki yake, bila kupunguza chochote katika haki yake, na bila kumwinua mtu yeyote zaidi ya hadhi anavyostahili. Kama vile hakupunguza heshima anaestahili heshima, pia haukumwinua yeyote zaidi ya hadhi inayomfaa. Kwa hivyo, uliwaonesha wanadamu utukufu wao na heshima yao, na ukawafundisha kwamba hata kama mtu atakuwa na hadhi ya juu na nguvu na mamlaka, hawezi kufikia hadhi ya kuabudiwa, kama vile Firauni walivyotaka kuabudiwa, hata kama atakuwa safi, mcha Mungu, na mwenye kujitenga na dunia, haipaswi kwa mwanadamu kumsujudia, au kutaraji kwake kitu ambacho hakitarajiwi isipokuwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu peke yake, au kumcha kama kumcha Mwenyezi Mungu. Na hata kama awe na mali nyingi na utajiri mkubwa, haipaswi kwake kujiweka juu ya ndugu zake katika viumbe vya Mwenyezi Mungu. Hakika ujumbe wa Muhammad (S.A.W) umekemea ufisadi, na kuondoa uovu katika mizizi yake, na kutangaza waziwazi ukweli huu kwa wanadamu:

(Sema: Enyi Watu wa Kitabu! Njooni kwenye neno lilio sawa baina yetu na nyinyi: Ya kwamba tusimuabudu yeyote ila Mwenyezi Mungu, wala tusimshirikishe na chochote; wala tusifanyane sisi kwa sisi kuwa Waola Walezi badala ya Mwenyezi Mungu. Na wakigeuka basi semeni: Shuhudi- eni ya kwamba sisi ni Waislamu.) [Aali Imran: 64]. ([4])

Lengo hili lilikuwa moja ya malengo makuu yaliyomshughulisha Mtume (S.A.W). Ilikuwa ni lengo kuu na madhumuni makuu ambayo alijitahidi kuyafikia tangu Mola wake alipomwamuru kubeba amana na kutangaza ujumbe, na katika haya yote alimtegemea Mwenyezi Mungu Mtukufu. Hivyo, Mtume (S.A.W) alifanya kazi kufikia lengo hili, akivumilia magumu, akishinda maumivu, akisubiri kwa maudhi na machungu ya maisha, mpaka alipofikia alichotaka kupitia imani nzuri na yakinifu, kazi nzuri na adhimu, uchunguzi sahihi wa mambo na matukio. Alikuwa na uwezo wa kusoma watu, jambo lililomwezesha kuwatumia kulingana na uwezo wao na mahitaji yao. Na kwa fadhila za Mwenyezi Mungu na msaada wake kwake, alitimiza lengo lake tukufu na madhumuni yake makubwa. "Alipuliza uhai mpya katika ubinadamu uliokuwa unakufa, na aligeukia hazina za ubinadamu ambazo zilikuwa zimefunikwa, ambazo hakuna mtu aliyefahamu utajiri wake, na ambazo zilikuwa zimepotea katika kipindi cha ujinga. Kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, alijenga imani na itikadi ndani yao, na akawapa roho mpya, na akafichua hazina zao, na akaibua vipaji vyao. Kisha akamweka kila mmoja katika nafasi yake, kana kwamba ameumbwa kwa ajili yake, na kana kwamba mahali hapo kulikuwa kunamsubiri. Kana kwamba alikuwa maiti asietikisika na kurudi katika uhai akiitawala dunia, Kana kwamba alikuwa alikua kipofu asiyeona njia akawa kiongozi mwenye kuona anayeongoza mataifa. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

(Je, aliye kuwa maiti kisha tukamhuisha, na tukamjaalia nuru inakwenda naye mbele za watu, mfano wake ni kama aliyoko gizani akawa hata hawezi kutoka humo? Kama hivyo makafiri wamepambiwa waliyo kuwa wakiyafanya.) [Al-An'am: 122]. ([5])

Kwa kifupi, pande za utukufu kwa Mtume (S.A.W) zinadhihirisha malengo yake, juhudi zake, na madhumuni yake. Utukufu wa lengo lake na utukufu wa madhumuni yake vilionekena katika kuukomboa na kuuokoa ubinadamu kutokana na matokeo mabaya ya yale yaliyotokea na kuendelea kwa karne nyingi, ambapo mizani ya haki ilipotea, na sheria ya uadilifu haikuwepo. Lakini yeye Mtume (S.A.W), akisaidiwa na wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliweza kuwaongoza kwenye njia iliyonyooka, akisaidiwa kwanza na Mwenyezi Mungu, kisha na kizazi kilichokuwa msaada wake mkuu katika kufikia lengo hilo kuu na madhumuni matukufu.

Hivyo, unaweza kusema kwamba ubinadamu uliamka baada ya "usingizi mzito na mrefu, uliodumu kwa karne nyingi, na ukataka kuyawahi yaliyoukosa mpaka ukatengeneza kila sehemu katika asehemu zake walinganizi wa Mungu wenye imani, wapigania jihadi wema, walimu, wenye kumjua Mwenyezi Mungu, wanaotoa nafsi zao kwa ajili ya wema wa ubinadamu na kuuokoa kutokana na hatari iliyokuwa ikiwazunguka katika kila upande. Hao ni wanaume wanaoonewa wivu na, ambao waliiamsha mioyo iliyolala, waliwasha upendo wa Mwenyezi Mungu, na wakafungua mito ya elimu, maadili, hekima na maarifa. Walifungua chemchemi ya iliyojaa, inayochimbuka elimu na maarifa, imani na huruma. Waliweka ndani ya nafsi za wanadamu chuki kali ya kuchukia dhulma, ukatili, uadui na chuki. Walifundisha mataifa yaliyokandamizwa na kudhalilishwa masomo ya usawa, na waliwapokea waliofukuzwa, waliohamishwa na maskini ambao jamii ilikuwa imewatupa na familia zao ziliwaacha, ndani ya mioyo yao iliyojaa upendo na huruma. Utaziona athari zao na dalili zao katika kila sehemu ya ardhi, kama vile matone ya mvua; hakuna nyumba ya jangwa wala ya jiji isiyo na athari zao." ([6])

Mtume (S.A.W) alijitahidi tangu mwanzo kuwaongoza wanadamu kupitia ujumbe wake kwenye lengo kuu, na madhumuni matukufu, ambayo yalisababisha kuzaliwa kwa ulimwengu mpya na uumbaji wa binadamu mpya. Hili halikuwa rahisi, bali lilikuwa jukumu gumu, lililohitaji kujitolea na kujitoa; kwa sababu watu wenye malengo makubwa huangalia kile wanachokitafuta, sio kile ambacho nafsi zao zinakitamani au wanachokipenda. Na alipata alichokitaka: "Dunia ilibadilika baada ya utume wa Mtume (S.A.W), kwa sababu ya mafundisho hayo matukufu, kama vile hali ya hewa inavyobadilika. Ubinadamu ulihama kutoka msimu wa ukame, vuli, upepo mkali na joto, hadi msimu wa vuli, wenye maua, na bustani zinazopita na mito. Tabia za watu zilibadilika, na mioyo yao ikang'aa kwa nuru ya Mola wao. Kuwa karibu na Mwenyezi Mungu kulikuwa jambo la kawaida, na mwanadamu alionja ladha mpya ambayo hakuijua, na msisimko ambao hakuwahi kuupata.

Mioyo iliyokuwa tupu, iliyodhoofika, baridi na iliyokufa ilipata uhai kwa joto la imani na nguvu za upendo. Akili ziliangazwa na nuru mpya, na nafsi zikajazwa na msisimko mpya. Binadamu walitoka kwa makundi wakitafuta njia sahihi, na hadhi yao ya juu, na wakitamani hadhi yao tukufu. Hakuna taifa au nchi yoyote unayoiona isipokuwa ilitaka kushindana katika uwanja huu." ([7]).

 

 

 

 

 

 

 

 


([1])  Je, Ulimwengu ulipoteza nini kwa kupungua kwa Waislamu? Abu al-Hasan al-Nadwi, uk. 63, Maktaba ya Al-Iman, Mansoura.

([2])  Jami’ Al-Bayan fi Ta’wil al-Qur’an, cha al-Tabari, kilichohaririwa na Dk. Abdullah bin Abdul Mohsen al-Turki, 8/264, Dar Hijr kwa Uchapishaji, Uchapishaji, Usambazaji na Utangazaji, toleo la 1, 1422 AH - 2001 AD.

([3])  Muhammad, (S.A.W), ni mkubwa wa watu mashuhuri duniani. hmed Deedat - Michael Hart, iliyotafsiriwa na: Ali Al-Jawhari, ukurasa wa 68-69, Maktaba ya Quran.

([4])  Ujumbe wa Muhammad, Sayyid Sulayman al-Nadwi, uk. 190-191, Dar Ibn Kathir, Damascus, toleo la 1, 1423 AH - 2002 AD.

([5]) Je, ulimwengu ulipoteza nini kwa kupungua kwa Waislamu? Abu al-Hasan Al-Nadwi, uk. 102

([6]) Sira ya Mtume, Abu Al-Hasan Al-Nadwi, uk. 485, Dar al-Shorouk, toleo la 8, 1409-1410 AH - 1989 AD

([7]) Sira ya Mtume, Abu Al-Hasan Al-Nadwi, uk. 484.

Share this:

Related Fatwas