Ni fasaha yake na ufasaha wa usemi ...

Egypt's Dar Al-Ifta

Ni fasaha yake na ufasaha wa usemi wake.

Question

Alijulikana (S.A.W) miongoni mwa watu na akawa maarufu kwa watu wake kwa fasaha ya usemi wake, uzuri wa maelezo yake, usafi wa maneno yake, urahisi wa kauli zake, mtiririko wa mtindo wake, ukamilifu wa maelezo yake, na uzuri wa maelezo yake. Yalikusanyika haya yote na mengineyo; kwa sababu alipewa maneno mafupi yenye maana pana

Answer

Na kwa ukubwa wa kipengele hiki kwake (S.A.W) Wanazuoni wa zamani na wa sasa wamekizingatia; kwa kuonyesha ukubwa wa utu huu katika uwanja huu ambao hakuna aliyemshinda ndani yake, hakuna aliyemfananisha, na hakuna aliyeweza kufikia kiwango chake katika ufasaha wa maelezo, fasaha ya ulimi, pamoja na uzuri wa uwekaji wa wazi (bayani), na uzuri wa maneno na misamiati, na kutokuwa na ukinzani kati ya maneno wala herufi. Wala si ajabu kwa hilo; kwani ni jambo linalokubalika, na linalojulikana kuwa yule anayekaa na wanazuoni na kulelewa katika mazingira ya watu wenye ufasaha, basi usemi wake unatoka ukiwa wa fasaha, wenye mtiririko, na unaochota kutoka kwenye ufasaha, ukiwa mtamu na laini.

Na ikiwa jambo hili limeshathibiti kwa watu wa akili, basi vipi kwa yule aliyefunzwa na Mola wa wanazuoni na watu wenye ufasaha, na akateremshiwa wahyi wa kipekee na kauli ya kimuujiza mpaka wamekiri wapinzani wake, na wakakubali makafiri ufasaha wake, na hawakuweza ila kukiri ukubwa wa usemi wake juu ya kila kauli, na ukubwa wa mamlaka yake juu ya kila hotuba! Na hapa ndipo ulipotoka sifa njema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Rehma na amani zimshukie) kwa mujibu wa kauli yake Aliyetukuka:

“Wala husemi kwa matamanio. Hakika haya si chochote ila ni ufunuo unaofunuliwa. Amemfundisha mwenye nguvu nyingi.” (An-Najm: 3-5)

Top of Form

Na katika mambo yasiyo na shaka na wala haiwezekani kwa namna yoyote kupuuzia kuwa huu wahyi wa kimuujiza una athari katika ufasaha wa mpenzi aliyechaguliwa (S.A.W) isiyoweza kushindaniwa, na mwanga wa kipekee katika maneno yake usiolinganishwa, uliomiminika katika nafsi yake tukufu, na ukapenya ndani ya hisia zake, na ukazama katika kina cha nafsi yake; hivyo athari yake ikaonekana katika ulimi wake, na ukamilifu wa dhahiri yake ukadhihirika katika ufasaha wa maneno yake na fasaha ya kauli zake (S.A.W)

Na hili ndilo alilolieleza msomi mkubwa, Imamu Al-Jahiz, alipokutana na ufasaha wa Mtume (S.A.W); akasema: “Ni maneno yaliyopungua idadi ya herufi zake na yakaongezeka idadi ya maana zake, yakajiepusha na ufanikishaji wa kisanii, yakatakasika na kujikalifisha, na yakawa kama alivyoamrishwa na Mwenyezi Mungu: ‘Sema ewe Muhammad, na mimi si miongoni mwa wanaojikalifisha.’

Basi vipi hali Mtume (S.A.W); alikemea utelezi wa maneno na akajitenga na watu wa lugha iliyopotoka[1], akatumia maneno yaliyopanuka katika mahali panapostahiki kupanuka, na yaliyofupishwa katika mahali panapostahiki kufupishwa, akaepuka lugha ya ajabu isiyofahamika, na akachukia lugha ya mtaani isiyo na hadhi, wala hakunena isipokuwa kwa urithi wa hekima, wala hakusema isipokuwa maneno yaliyolindwa na ulinzi wa Mwenyezi Mungu, yakaimarishwa kwa msaada, na yakirahisishwa kwa tawfiq.

Na haya ndiyo maneno ambayo Mwenyezi Mungu alimwekea mapenzi, akayafunika kwa kukubalika, akayakusanyia baina ya utukufu na ladha, pamoja na uzuri wa kueleweka na uchache wa idadi ya maneno, huku yakitosha bila haja ya kurudiwa, na msikilizaji asihitajie kuyasikia tena.”

Hakuwahi kupoteza neno, wala mguu wake haukuteleza, wala hoja yake haikuwahi kudhoofika, wala mpinzani hakuwahi kusimama mbele yake, wala khatibu hakuwahi kumshinda kwa maneno. Bali alikuwa akizidi hotuba ndefu kwa maneno mafupi, wala hakuwa akitafuta kunyamazisha mpinzani isipokuwa kwa kile anachokijua mpinzani, wala hakutegemea hoja ila kwa ukweli, wala hakuwa akitafuta ushindi ila kwa haki, wala hakusaidiana na hila, wala hakutumia udanganyifu, wala hakutusi wala hakudhalilisha, wala hakupendelea kusuasua wala kukurupuka, wala hakuzidisha wala hakupunguza.Kisha watu hawakusikia kamwe maneno yenye manufaa zaidi, wala yaliyonyooka zaidi lafudhi yake, wala yenye usawa zaidi mizani yake, wala yenye njia nzuri zaidi, wala yenye shabaha tukufu zaidi, wala yenye mahali bora zaidi, wala yenye kutoka kwa urahisi zaidi, wala yenye maana fasaha zaidi, wala yenye ufafanuzi wa ndani zaidi kuliko maneno yake (S.A.W).[2]

Na haya aliyoyataja Imamu Al-Jahiz ndiyo aliyoyathibitisha Qadhi ‘Iyadh, ambapo anasema: “Ama ufasaha wa ulimi na ufasaha wa kauli, basi alikuwa (S.A.W) katika daraja ya juu zaidi, na mahali pa wazi pasipo na shaka, akiwa na wepesi wa maumbile, upekee wa mtazamo, ufupi wa maneno, uwazi wa lafudhi, uimara wa kauli, usahihi wa maana, na upungufu wa kujikalifisha. Alitunukiwa muhtasari wa maneno, na akapambwa na hekima za pekee, na akafahamu lahaja za Waarabu, hivyo alikuwa akizungumza na kila kabila kwa lugha yake, na akijadiliana nao kwa lahaja yao, na akiwashindana katika njia ya ufasaha wao, hadi mara nyingi Maswahaba wake walikuwa wakimuuliza katika sehemu tofauti juu ya maelezo ya maneno yake na tafsiri ya kauli yake. Yeyote atakayechunguza hadithi zake na mwenendo wake, atalithibitisha hili na kulielewa.”[3]

Top of Form

Bottom of Form

Hakika anayetafakari maandiko haya mawili ya Maimamu wawili: Al-Jahiz na Qadhi A‘yadh, atasimama juu ya mambo kadhaa yanayowakilisha fasaha katika upeo wake na uzuri wake, na ufasaha wa kauli katika ukamilifu na uzuri wake; kwani wametaja mambo kadhaa yanayofichua ukubwa wa utu wa Mtume (S.A.W)   kupitia mtindo wake wa kifasaha na kauli yake nzuri, nayo ni kupitia mambo haya yafuatayo:

Kwanza: Wingi wa maana na uchache wa idadi ya herufi, na hili linathibitisha kuwa yeye alipewa muhtasari wa maneno; kwani uchache wa maneno pamoja na upana wa maana ni dalili ya hilo. Kutoka katika hadithi ya Abu kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) amesema: “Nimepewa muhtasari wa maneno.” [4]Na muhtasari wa maneno ni kauli fupi zenye hekima, kila kauli ikiwa na maana nyingi huku ikitimiza maana iliyomo, na muhtasari ni miongoni mwa sifa mashuhuri za fasaha ya Kiarabu.[5]

Pili: Licha ya kuzingatia ufupisho, hakuwahi kufupisha kwa kuharibu maana au mbali na lengo; kwa hiyo Al-Rafi’i alihesabu ufupisho kuwa mojawapo ya sifa za kipekee za lugha ya unabii, akisema: “Kusudio, ufupisho, na kuzingatia kile kinachotokana na asili ya maana katika maneno yake, na kutoka kwa asili ya maneno katika maana zake, na kutoka kwa asili ya nafsi katika sehemu yake ya mazungumzo na kwa njia mbili — za maneno na maana — ni jambo lililotambulika katika lugha ya unabii, kiasi kwamba maneno yanakuwa kama harakati za nafsi, na sentensi zinazaliwa kwa njia yake (S.A.W)   kwa uzuri wa hali ya juu, au kama zinavyochukuliwa kutoka nafsi yake kwa uondoaji, jambo hili ni la ajabu, hadi mtu mwenye fikra anaweza kumpa nafsi yake mshangao mkubwa.”[6]

Tatu: Kwamba maneno yake yalikuja yakiwa hayana maneno mageni, machafu, wala ya kejeli. Haikunakiliwa – haikupokewa chochote kuhusu lugha yake ambalo lingekosababisha kutoeleweka kwake au kupotosha maelezo yake. Hii ni kutokana na ule ufasaha wake, ambao haukuwa tu wa maneno na herufi, bali wa lugha kwa ujumla (maneno na maana). Kwa hivyo, maneno yake yalikuwa rahisi, wazi, na yanayokubalika, hayaonyeshi udhaifu, bali hekima, tahadhari, na usahihi; maneno yake yalikuwa thabiti, yenye mfululizo, yasiyo na mchanganyiko, yanayodhibitiwa na akili, Wazo halirukii kwa pupa, bali hudhibitiwa na maoni yenye busara; halikanganyiki kutoka pande zake, wala halikinzani kutoka nyanja zake mbalimbali, bali huonekana likiwa na mlingano mmoja wa uimara, nguvu, mshikamano na uthabiti.[7] Na kwa nini isiwe hivyo?! Ilhali ufasaha wake uliwapita Waarabu wote, hadi akawa ndiye fasaha zaidi kuliko wote. Hili ndilo alilolieleza as-Siddīq (Radhi za Allah ziwe juu yake) aliposema: “Ewe Mtume wa Allah, nimezunguka miongoni mwa Waarabu na kusikia waliofasaha miongoni mwao, lakini sijawahi kusikia mtu mwenye ufasaha zaidi yako. Ni nani aliyekufundisha adabu?” Akasema: “Mola wangu ndiye aliyenilea, nami nimelelewa katika (kabila la) Bani Sa’d.”[8]

Bottom of Form

Nne: Maneno yake yalikuwa mbali na ugumu na utengenezaji wa maneno; Mtume (Rehma na amani zimshukie) alikuwa mbali na ugumu katika maneno na matendo yake. Mwenyezi Mungu alisema: ("Sema (Ewe Mtume): Sikuombeni ujira juu ya haya, wala mimi si katika wadanganyifu." [Surah Saad: 86]. Ugumu ni kutafuta kitu kwa shida kwa sababu ya kutokuwa na ufahamu wa njia rahisi za kuutafuta. Ikiwa maneno yamekusanywa kwa juhudi na kwa tabu, "Na maneno yakikusanya kwa kujikalifisha, basi huyo ni mwenye kujikalifisha.[9] Lakini hakika maneno yake (S.A.W) hayana kujikalifisha wala mashaka." njia yake ilikuwa ni asili ya lugha na ufasaha wake wa asili kama wa wasemaji wa Kiarabu au kwa ufunuo wa Mwenyezi Mungu ambaye alimpa ufafanuzi wa Qur'an[10]. Hii inaoneshwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: "Halafu kwetu ni jukumu letu kufafanua" [Al-Qiyamah: 19].

Yote haya yanaonyesha kwamba lugha aliyotumia, ufafanuzi wake, na ufasaha wake ni sehemu muhimu na inayoonekana katika tabia yake (Rehma na amani zimshukie), na hii inathibitisha kuwa ni mojawapo ya vipengele vya ukuu wake (S.A.W), Hii inathibitishwa na misemo mingi ya Mtume (S.A.W),  inayofichua ufasaha wake na uzuri wa maelezo yake, na kuthibitisha neema ya Mwenyezi Mungu kwake kwa kumpa jozi za maneno yenye maana nyingi (jawami’ Al-Kalim).

Top of Form

Bottom of Form

1- Kutoka kwa Abdullah bin Umar L alisema: Mtume Muhammad (S.A.W)   alisema: «Farasi wana heri katika utosi (vichwa vyao) hadi Siku ya Kiyama» [11]

Hadithi hii, ingawa maneno yake ni machache na mafupi, ila ina maana nyingi na tofauti, kama alivyosema Imam Ibn Hajar: "Iyadh alisema: Katika Hadithi hii, pamoja na maneno mafupi, kuna ufasaha na uzuri usio na kifani, pamoja na mlinganisho rahisi kati ya maneno farasi na heri. Al-Khattabi alisema: Kuna ishara kwamba mali inayopatikana kwa kumiliki farasi ni mojawapo ya mali bora na nzuri zaidi, na Waarabu huitaja mali kama heri, kama ilivyoelezwa katika amri ya Mwenyezi Mungu: (Hakika kuacha heri ni wasia). Ibn Abd al-Barr alisema: Hii inaonyesha upendeleo wa farasi juu ya wanyama wengine kwa sababu hakujakuwepo na hadithi kama hii kutoka kwa Mtume (S.A.W) kuhusu kitu kingine zaidi ya farasi."[12]

2- Na katika hadithi nyingine kutoka kwa Abu Huraira (R.A) alisema: Mtume Muhammad (S.A.W) alisema: «Hakuna maambukizi, wala homa ya manjano wala uharibifu» Kisha mtu wa kijijini (bedui) alimwambia: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, unaonaje ngamia zangu ziko jangwani kama vile swala, ndipo ngamia mgonjwa huingia kati yao na kuwaua? Mtume alisema: “Basi nani aliyeambukiza wa kwanza? »[13]

Anayeangalia hadithi hii huona wazi uzuri wa maneno yake na jibu lake zuri, ukiachilia mbali mtindo wake mzuri. Hili ndilo aliloelezea Hafidh Ibn Hajar anapotafsiri hadithi hii kwa kusema: "Waliamini maambukizi, yaani kuwa mtu mgonjwa anaweza kuambukiza wengine ugonjwa, lakini huu ni upuuzi wa watu wasiojua. Walidhani kuwa mgonjwa akiingia miongoni mwa wenye afya basi huwafanya wawe wagonjwa. Hali hii imethibitishwa na Sheria ya Mwenyezi Mungu kuwa si kweli. Mtume alipokuwa akijibu shaka ya mtu wa kijijini alisema: “Basi nani aliyeambukiza wa kwanza?’ Jibu hili lina uzuri mkubwa na ufasaha, maana yake ni kwamba, kama ugonjwa huo ulishaambukizwa na ngamia mwingine, basi kungekuwa na mfululizo wa maambukizi, na kwa kuwa hakuna mfululizo huo, basi ni wazi kuwa wote waliuguliwa kwa sababu ya Muumba nae ni Mwenyezi Mungu,"[14]

Top of Form

3-Vile vile kauli yake (S.A.W): "Umwabudu Mwenyezi Mungu kana kwamba unamuona; na ikiwa huwezi kumuona, basi Yeye anakuona."

Na huu ni ushahidi wa tatu tunaoupata wa ufasaha wake na ukamilifu wa maelezo yake; kwani hadithi hii ni dalili kuwa alipewa maneno mafupi yenye maana pana. Ushahidi wa hayo ni kauli yake: "Kana kwamba unamuona", maana yake: mja amdhihirishe Mola wake wakati wa kumtii na kumuabudu kwa namna kamili akilini mwake, moyoni mwake, na katika hali ya kuamka kwake, kiasi kwamba hapatiwa na kitu chochote kinachomsahaulisha au kumghafilisha; bali ajitokeze katika ibada yake kwa kujitokeza kamili kabisa, na afikie kiwango katika hali hiyo ya kuhudhuria moyo, unyenyekevu, na kujitokeza kiasi kwamba lau kama Mwenyezi Mungu angetazamwa kwa macho, basi angemtazama katika hali hiyo.

Ama kauli yake (S.A.W): "Na ikiwa huwezi kumuona", yaani: kama hivyo kuona kwa maana hiyo ya kiroho na hali ya moyo, basi uwe katika hali kwamba Yeye anakuona; yaani: uwe mwenye kujua na mwenye kukumbuka, si mwenye kughafilika wala kutojali, na uwe mwenye bidii katika hali ya uja, mwaminifu katika nia yako, kwani yule anayejua kuwa ana Mlinzi na Shahidi anayetazama matendo yake, basi hawezi kukosa adabu hata kwa kupepesa jicho, wala kwa wazo la ghafla, na atasimama daima katika hali inayomridhisha Muumba wake.[15]

Na anasema Imamu al-Ṭībī: "(Kana kwamba wewe)" ni Mafulu Mutlaq, au ni hali ya mtenda. Na ya pili ndiyo yenye nguvu zaidi; kwa sababu kwa hilo mja hupata hali tatu, kama unavyosema: Kana kwamba Zayd kasimama, basi huakisi kwake hali tatu: ya kukaa, ya kusimama nusu, na ya kusimama kamili. Basi hufananishwa hali ya kusimama nusu na hali ya kusimama kamili; kwa sababu kwa kuingiza kana kwamba, huonesha kuwa ana hali nyingine isiyokuwa ya kusimama kamili, ambayo imefananishwa nayo. Kama vile mtu anapomwona mwingine kwa mbali, akawa anashuku baina ya kuwa amekaa au kasimama, kisha katika hadithi ikahisiwa kuwa yuko karibu zaidi na kusimama, akasema: Kana kwamba kasimama, yaani: kusimama kwake kunafanana na kusimama kamili.

Vivyo hivyo katika hadithi hii — mja mbele ya Mola wake ana hali tatu: moja, hali ya kujishughulisha na ibada kwa mujibu wa sharia, kwa kuhifadhi masharti yake, nguzo zake na namna zake; ya pili, hali ya kuweza kutakasika nia, na kujua kwamba yuko mbele ya Mola wake, na kwamba anatazamwa katika harakati na kimya chake; na ya tatu, hali ya kumshuhudia (Mola wake) na kuzama katika bahari za kufunuliwa mambo ya siri. Na kwenye hii ndiyo alivyosema (S.A.W) : "Na furaha ya jicho langu imewekwa katika Swala"[16], na "Ewe Bilal, tuburudishe kwa swala."[17]

Basi kafananisha hali ya pili, ambayo ni ya uangalizi na kujua kwamba unatazamwa, na hali ya kufunuliwa mambo ya siri, ambayo ni maalumu kwa Mtume (S.A.W) hapa duniani. Na sababu ya kufananisha ni upatikanaji wa ladha katika ibada, utulivu katika kumuabudu, na kufungwa kwa njia za kugeuka kwa wengine kwa sababu ya nguvu ya nuru ya kufunuliwa mambo ya siri juu yake. Na hiyo ni matunda ya kujazwa kona zote za moyo kwa mpenzi wake, na siri yake kushughulika naye, na matokeo yake ni kusahau hali za elimu, na kuyeyuka kwa alama na desturi.

Basi, pale alfajiri ilipoanza kuchomoza, mwangaza wake ulizifunika nuru za nyota. Na kauli yake: "(Na ikiwa huwezi kumuona)" — inateremka kutoka katika daraja ya kushuhudia mambo ya siri kwenda kwenye daraja ya uangalizi na kujua kwamba unatazamwa. Basi yapasa kuzingatia maana ya kauli yangu: kwamba Yeye anakuona.[18]

Hakika anayechunguza yale aliyoyasema Imamu al-Ṭībī atasimama juu ya ufasaha wa Mtume (S.A.W) na fasihi ambayo haikanushwi na mwenye haki; na kwa sababu hiyo tumehamisha maandiko haya yote pamoja na urefu wake, ili kuthibitisha upande huu na kuonesha pande zake, na kuelezea ufasaha wake kwa yale yanayolitofautisha na mengine, na kufunua juu yake na upekee wa mwenye nao.

Hakika ufasaha wa Mtume (S.A.W) ni chemchemu tajiri isiyokauka, na kisima kinachobubujika kisichopungua, na ndio kauli iliyo juu zaidi ya kibinadamu; kwani huja kubainisha Qur’ani Tukufu, na juu ya kauli za wanadamu wote, basi yeye ndiye kiumbe fasaha zaidi kwa ulimi na mwenye kauli bora zaidi kwa bayana. Na haya ndiyo aliyoyadokeza Mwalimu Ahmad Hassan Al-Zayyat aliposema: "Hakika ufasaha wa Mtume (S.A.W) ni kazi ya Mwenyezi Mungu, na kilicho kazi ya Mwenyezi Mungu vipimo vya binadamu huwa hafifu kukipima, na mizani yao huwa fupi kufikia kiwango chake; hivyo sisi hatuwezi kufahamu hakika yake, bali tunaweza kufahamu athari yake tu. Na sisi hatujui jinsi kilivyotungwa bali tunajua habari yake. Je, mwanadamu anaweza kuona katika athari za jua zaidi ya mwangaza na joto? Na je, anajua katika siri za bustani zaidi ya harufu nzuri na mbwembwe? Na je, anaweza kupata katika nafsi yake katika vilindi vya bahari zaidi ya hisia ya utukufu na woga? Basi, ufasaha wa Mtume Rehma na amani zimshukie ndio mfano wa juu kabisa wa ufasaha wa Kiarabu. Na ikiwa maneno ya Mwenyezi Mungu ni Kitabu cha bayaai kinachoshinda, basi maneno ya Mtume (S.A.W) ni Suna ya ubayanishi huo. Na ikiwa kufikisha ujumbe ni sifa ya kila Mtume, basi ufasaha ni sifa ya Muhammad (S.A.W)   peke yake."

Na hitimisho la kauli ni kwamba: hakika dalili za ukuu katika nafsi yake (S.A.W) japokuwa ni nyingi, lakini hubaki kuwa yale yanayohusiana na fasihi yake na ufasaha wake ndiyo yaliyo dhahiri zaidi na yaliyo wazi mno; kwani huweza kufikisha mengi kwa maneno machache, na huleta yaliyo mbali kwa mfano rahisi na mwepesi, na hufunga uhusiano kati ya mambo ya kiroho na vielelezo vya kihisia — jambo linaloonyesha upeo wa kuizingatia lugha ya Kiarabu, kuzielewa pande zake na aina zake, na namna ya kuzitumia na mahali pa kuzitumia.

 


[1]  maana yake ni kutoa maneno kutoka chini kabisa ya koo lake, kama ilivyobainishwa katika kitabu Lisan al-‘Arab cha Ibn Manzur, juzuu ya 5, ukurasa wa 108, kilichochapishwa na Dar Ṣadir, Beirut — katika kiingilio cha neno

[2] Al-Bayan wa al-Tabyin, al-Jahiz (aliyefariki mwaka 255 Hijria), (2/13-14), Dar wa Maktabat al-Hilal — Beirut, 1423 Hijria.

[3] Ash-Shifa bi Taʿrif Huquq al-Mustafa, al-Qadhi ʿIyadh, (1/70).

[4] Sahihi Muslim, Kitabu: Al-Masajid wa Mawadiʿ as-Salah, Mlango: Ardhi imenifanywa kuwa msikiti na njia ya kutwaharika, (1/372), Na: (523).

[5] Tazama: Balagha ya Mtume, Dkt. Ali Al-‘Amari, uk. 50

[6]Muujiza wa Qur’ani na Fasaha ya Mtume, Mustafa Sadiq Al-Rafi’i (aliyefariki 1356 H), uk. 246, Taasisi ya Hindawi, 2022.

[7] Angalia: I'jaaz al-Qur'an wal-Balaaghah an-Nabawiyyah, Mustafa Saadiq ar-Rafi'iy, uk. 219

[8] Ad-Durar al-Muntathirah fi al-Ahaadith al-Mushtahirah, Jalaluddin As-Suyuti (aliyefariki 911 H), tahkiki: Dkt. Muhammad bin Lutfi As-Sabbagh, uk. 45, Idara ya Mambo ya Maktaba – Chuo Kikuu cha Mfalme Saud, Riyadh.

[9] Angalia: As-Sinaa‘atayn, Abū Hilāl al-‘Askarī (aliyefariki takriban 395 H), tahkiki: ‘Alī Muhammad al-Bajāwī na Muhammad Abū al-Faḍl Ibrāhīm, uk. 44, Al-Maktabah Al-‘Aṣriyyah – Beirut, 1419 H.

[10] Angalia: As-Sunnah Bayānān lil-Qur'ān, Dkt. Ibrāhīm al-Khūlī, uk. 77.

[11] Ameipokea Al-Sheikhān: Sahīh al-Bukhārī, Kitabu: Al-Jihād na Siyar, Mlango: Farasi wana kheri katika utosi hadi Siku ya Kiyama, (4/28), Hadithi Na. (2849); Sahīh Muslim, Kitabu: Al-Imārah, Mlango: Farasi wana kheri katika utosi mwao  hadi Siku ya Kiyama, (3/1492), Hadithi Na. (1871).

[12] Fathu al-Bari, Sharh Sahih al-Bukhari, Ibn Hajar, Juzuu ya 6, ukurasa wa 56, Dar al-Ma’rifah - Beirut, 1379 H.

[13] Wameipokea Sheikhani: Sahihi ya al-Bukhari, Kitabu: Tiba, Mlango: Hakuna ugonjwa wa manjano, nayo ni maradhi yanayoshambulia tumbo, (7/128), Hadithi Na. (5717), na Sahihi ya Muslim, Kitabu: Salaam, Mlango: Hakuna maambukizi, wala ushirikina wa ndege, wala uharibifu, wala ugonjwa wa manjano (4/1742), Hadithi Na. (2220).

[14] Fathu al-Bari: Ibn Hajar, Juzuu ya 10, Ukurasa wa 241-242

[15] Tazama: Sunnah Bayanan LilQuran, Dkt. Ibrahim al-Khuli, uk. 89.

[16] Musnad Ahmad, (19/305), Hadithi Na. (12292)

[17] Al-Mu’jam al-Kabir, At-Tabarani, (6/277), Hadithi Na. (6215)

[18] Sharh at-Tībī kitabu Mishkāt al-Maṣābīḥ chenye jina al-Kāshif ‘an Ḥaqā’iq as-Sunan, kilichoandikwa na at-Tībī (aliyefariki mwaka 743 Hijria), toleo lililohakikiwa na Dkt. ‘Abd al-Ḥamīd Hindāwī, juzuu ya 2, kurasa 430-431, kimechapishwa na Maktaba ya Nizār Muṣṭafā al-Bāz, toleo la kwanza, mwaka 1417 Hijria (sawa na 1997 Miladia).

Share this:

Related Fatwas