Hukumu ya kuamini taarifa za utabiri wa hali ya hewa
Question
Ni ipi hukumu ya kuamini hali ya hewa inayotarajiwa, kama ile inayotolewa na Mamlaka ya Taifa ya Hali ya Hewa? Je, hali hiyo huhesabiwa kuwa ni miongoni mwa unajimu uliokatazwa kisharia?
Answer
Mamlaka za hali ya hewa huchapisha ripoti na matangazo ya mara kwa mara kuhusu hali ya hewa, yanayojumuisha taarifa zinazohusiana na shughuli za uchunguzi wa hali ya hewa katika eneo maalumu la dunia. Matangazo hayo hayatolewi ila baada ya kufanywa hesabu za kisayansi zilizo sahihi, zinazotegemea nadharia za jumla, sheria za kimaumbile za ulimwengu, na majaribio yaliyorudiwa mara nyingi yaliyofanywa na wanasayansi katika vizazi mbalimbali. Hakuna kizuizi kwa upande wa sharia. Wala hayana uhusiano wowote na unajimu ulioharamishwa, ambao umejengeka juu ya kubahatisha, hisia za kudhania, kudai kujua mambo ya ghaibu, na kuamini kuwa kuna mwenye athari katika ulimwengu kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Maelezo
Mwenyezi Mungu Mtukufu ameufanya ulimwengu na vilivyomo kuwa chini ya matumizi ya mwanadamu ili kumwezesha kutekeleza jukumu aliloumbiwa kwa ajili yake, nalo ni ukhalifa katika ardhi, na ili kukidhi mahitaji yake ya kidini na ya kidunia. Kadiri muda unavyosonga mbele na elimu ya mwanadamu inavyoendelea, ndivyo manufaa yanavyozidi kuongezeka. Mwenyezi Mungu anasema:{Na akalifanya jua na mwezi kwa manufaa yenu daima dawamu, na akaufanya usiku na mchana kwa manufaa yenu.} [Ibrahim: 33].
Maana ya kuvifanya viwe chini ya matumizi ya watu ni kuvifanya viwe na manufaa kwao kulingana na maslahi yao kwa mfumo mmoja unaoendelea bila kukatika, kama mtumwa mtiifu. Kauli hiyo inahusu pia kufanywa jua, mwezi, na nyota ziwe chini ya matumizi ya wanadamu.
Kazi inayofanywa na mamlaka za hali ya hewa ya kuchapisha ripoti na matangazo ya mara kwa mara kuhusu hali ya hewa, yanayojumuisha taarifa zinazohusiana na shughuli za uchunguzi wa hali ya hewa katika eneo maalumu la dunia—hasa shughuli za kimaumbile zinazotokea katika mzunguko wa kila siku kama mabadiliko ya viwango vya joto, uwezekano wa kunyesha kwa mvua, mawingu ya chini, kiwango cha unyevunyevu, kiwango cha shinikizo la hewa, na matukio mengineyo—hufahamika kwa kuzingatia ramani za tabaka za juu za anga zinazoonesha maeneo ya shinikizo la juu na la chini pamoja na mikondo ya hewa, kisha kupimwa juu ya eneo maalumu. Hayo yote hufanywa kwa kutumia nadharia za kisayansi, kanuni za kihesabu, na vifaa vya kisasa ambavyo taasisi husika hutegemea kabla ya kutoa tangazo lake la mara kwa mara kuhusu hali ya hewa kwa kipindi maalumu kama siku moja, mbili, au tatu.
Matangazo hayo hayatolewi ila baada ya kufanywa hesabu za kisayansi zilizo sahihi, zinazojengwa juu ya nadharia za jumla, sheria za ulimwengu, na majaribio yaliyofanywa mara kwa mara na wanasayansi katika vizazi mbalimbali, sambamba na kunufaika kwa kiwango kikubwa na elimu na teknolojia za kisasa ambazo kila siku huleta mambo mapya. Inajulikana kuwa ujuzi huu wa hali ya hewa inayotarajiwa unategemea zaidi dhana yenye uzito kuliko yakini kamili. Imepokewa kutoka kwa Mtume (S.A.W) kutajwa kwa baadhi ya dalili ambazo zinaweza kutumiwa katika kufanya aina hii ya makadirio. Imepokewa kutoka kwa Mama wa Waumini Bi. Aisha (R.A) kuwa Mtume (S.A.W) alisema: “Ikiwa upepo wa baharini utaanzisha mawingu, kisha ukageuka kuelekea Kaskazini, basi hilo ni jicho lenye maji mengi.”
Na katika riwaya ya Al-Bayhaqi katika Ma‘rifat as-Sunan wal-Athar kutoka kwa Imamu Shafii kwa lafudhi: “Iwapo wingu litaanza kwa upepo wa baharini, kisha likageuka kuwa la upande wa Shamu, basi hiyo ndio hali yenye mvua nyingi zaidi.”
Ikimaanisha kwamba ikiwa upepo wa baharini utapiga na kuunda mawingu, kisha upepo wa upande wa Kaskazini ukapiga, basi hilo ni dalili ya mvua kubwa.
Kinachopasa kuaminiwa ni kukata kauli kwamba kutokea kwa baadhi ya matukio pamoja na kuonekana kwa baadhi ya nyota ni jambo la kawaida linalotokea mara nyingi, lakini linaweza pia kutokuwepo, kama ilivyo katika kauli ya Mtume (S.A.W) “Ikiwa mawingu yataanzishwa kwa upepo wa baharini kisha yakageuka kuelekea Kaskazini, basi hilo ni jicho lenye maji mengi,[1]” yaani, ikiwa wingu litachomoza kutoka upande wa Magharibi na kuelekea Shamu, basi wingu hilo huwa na mvua nyingi.
Hili linaungwa mkono na Qur’ani Tukufu katika kuelekeza kunufaika na dalili hizi na kuhimiza kujua elimu hiyo kisheria. Mwenyezi Mungu anasema: {Na Yeye ndiye aliyekujaalia nyota ili muongoke kwazo katika giza la nchi kavu na bahari} [Al-An‘am: 97]. na kauli yake: {Na kwa alama, na kwa nyota wao huongozwa} [An-Nahl: 16. Na aliposema: {Yeye ndiye aliyelijaalia jua kuwa mwanga na mwezi kuwa nuru, na akaipangia awamu ili mjue idadi ya miaka na hesabu” [Yunus: 5). Na kauli yake: {Wanakuuliza kuhusu miezi mipya. Sema: hiyo ni nyakati kwa watu na kwa Hija} [Al-Baqarah: 189]. Jua na mwezi husafiri kwa hesabu iliyo pangwa kwa usahihi, isiyobadilika wala kuyumba. Kila kimoja kina vituo vyake ambavyo hupitia katika majira ya kiangazi na baridi, na kutokana na hilo hutokea tofauti ya urefu na ufupi wa usiku na mchana.
Kutokana na yaliyoelezwa, inabainika kwamba kutabiri hali ya hewa kunakotegemea hisia, uchunguzi wa moja kwa moja, nadharia za kisayansi zilizo sahihi, pamoja na uzoefu na mazoea, ni jambo linalojuzu kisharia, na si katika unajimu ulioharamishwa kisharia. Unajimu ulioharamishwa ni kudai kujua matukio au mambo ya ghaibu, kama kutoa taarifa kuhusu nyakati za furaha na mashaka, uhai na mauti, na mambo mengine yanayofanana nayo, ambayo wanajimu hudai yanaweza kujulikana kupitia mienendo ya sayari, kukutana kwake na kutengana kwake. Hapo huaminiwa kuwa kila nyota ina athari katika matukio ya ardhini. Unajimu kwa maana hii ni aina ya ukuhani unaojumuisha unajimu, uaguzi, ramli, kuchora mistari, na mambo mengineyo yanayoishia katika kudai kujua ghaibu, ambayo Mwenyezi Mungu ameihodhi peke yake. Mambo haya yote ni haramu katika Sharia ya Kiislamu kwa kuwa ni madai ya kujua ghaibu, na ghaibu haijulikani ila kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu peke yake.
Hali ni tofauti na kutoa taarifa za hali ya hewa zinazojengwa juu ya nadharia za kisayansi na sheria za falaki zinazotokana na kufanya Mwenyezi Mungu ulimwengu uwe chini ya matumizi ya wanadamu, na ambazo zinategemea hisia na uchunguzi wa moja kwa moja, na hufanya kazi kwa misingi ya sababu na matokeo ya kisayansi, kama ilivyotajwa.
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
Hakuna kizuizi cha kisharia katika kuamini matarajio yanayotangazwa na kuchapishwa na mamlaka ya hali ya hewa kuhusu hali ya hewa kwa kipindi kijacho, hasa kwa kuwa yanajengwa juu ya misingi na nadharia za kisayansi zilizo maalumu. Taarifa hizo hazizidi kuwa makadirio ya kawaida yanayoweza kutokea tofauti yake, wala hayana uhusiano wowote na unajimu uliokatazwa kisheria, ambao umejengwa juu ya kubahatisha, hisia za kudhania, kudai kujua mambo ya ghaibu, na kuamini kuwa kuna chenye athari katika ulimwengu kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu.
[1] Imepokewa na maimamu: At-Tabarani katika Al-Mu‘jam Al-Awsat, na Malik katika Al-Muwatta’, kupitia riwaya ya Abu Mus‘ab Az-Zuhriy.”
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
