Unyanyasaji wa Kingono

Egypt's Dar Al-Ifta

Unyanyasaji wa Kingono

Question

Nini hukumu ya kisharia kuhusu unyanyasaji? Na je, mavazi ya mwanamke yanahalalisha kitendo cha mnyanyasaji?

Answer

Unyanyasaji wa kingono ni haramu kisharia na ni kosa lenye adhabu kisharia. Kunasibisha kosa hili na vishawishi vya nje pekee ni kisingizio cha bure ambacho hakitolewi isipokuwa na watu wenye nafsi zenye maradhi na matamanio duni. Muislamu ameamrishwa kuinamisha macho dhidi ya mambo ya haramu katika hali na mazingira yote; Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: { Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao. Hili ni takaso bora kwao. Hakika Mwenyezi Mungu anazo khabari za wanayo yafanya} [An-Nur: 30].

Kulinda faragha ya mwanadamu katika mwonekano na sura yake hakukomei tu katika kutovunja sitara iliyowekwa au kutoangalia uchi, bali ni katazo la jumla la kuachia macho kwa wengine bila ya wao kujua na bila dharura. Mnyanyasaji ambaye ameachia matamanio yake akihalalisha kitendo chake, anakuwa amekusanya maovu mawili: kuangalia kwa wizi na kuvunja faragha. Mtume (S.A.W) amesema: «Jiepusheni na kukaa njiani.» Wakasema: "Ewe Mtume wa Mungu, hatuna budi, kwani ni sehemu zetu za mazungumzo." Akasema: «Ikiwa mmekataa na lazima mkae, basi ipeni njia haki yake.» Wakasema: "Na ni nini haki ya njia?" Akasema: «Kuinamisha macho, kuacha udhia, kurudisha salamu, kuamrisha mema, na kukataza maovu» (Imepokelewa kutoka kwa Al-Bukhari na Muslim).

Maelezo

Uislamu umefanya kushambulia heshima za watu[1] kuwa miongoni mwa madhambi makubwa. Imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas (R.A) kwamba Mtume (S.A.W) alihutubia watu siku ya Nahri akasema: ((Enyi watu, ni siku gani hii?)) Wakasema: "Siku takatifu." Akasema: ((Ni mji gani huu?)) Wakasema: "Mji mtakatifu." Akasema: ((Ni mwezi gani huu?)) Wakasema: "Mwezi mtakatifu." Akasema: ((Hakika damu zenu, mali zenu, na heshima zenu ni haramu kwenu[2], kama ilivyo utukufu wa siku yenu hii, katika mji wenu huu, katika mwezi wenu huu)). Alikariri maneno hayo mara kadhaa kisha akainua kichwa chake na kusema: ((Ewe Mwenyezi Mungu, je nimefikisha? Ewe Mwenyezi Mungu, je nimefikisha?)) (Imepokelewa na Al-Bukhari na Muslim).

Kwa sababu mwanamke ndiye sehemu ya thamani na adhimu zaidi ya heshima, Uislamu umeamrisha kumtunza, na ukafunga hata kumtazama kwa matamanio, vilevile ukafunga kumgusa; dalili ya hilo ni kauli ya Mtume (S.A.W): ((Ni bora mmoja wenu achomwe kichwani mwake kwa sindano ya chuma[3], kuliko kumgusa mwanamke asiye halali kwake)) [4]. Maana yake ni kwamba Mtume (S.A.W) alionya dhidi ya mtu kumshambulia mwanamke yeyote asiye halali kwake kwa kumgusa tu, na yeyote anayefanya hivyo anastahili adhabu.

Pia kauli yake (S.A.W): ((...Na ni bora mtu asukumane na nguruwe aliyelowa matope au udongo mweusi unaonuka[5], kuliko bega lake kusukumana na bega la mwanamke asiye halali kwake)) [6]. Hadithi hii inaashiria ubaya wa mtu kukusudia kumgusa mwanamke asiye halali kwake kwa matamanio.

Pia amesema (S.A.W): ((Macho yanazini, ulimi unazini, mikono inazini, na miguu inazini, na tupu inathibitisha hilo au kulikanusha))[7]. Hii inaonesha kuwa viungo hivi vimesifiwa kwa uzinzi kwa sababu ni miongoni mwa vishawishi vyake [8].

Unyanyasaji dhidi ya mwanamke, ukiwa ni uvunjifu wa faragha yake, ni jinai haramu na dhambi kubwa. Mtume (S.A.W) amesema: ((Hakika miongoni mwa riba mbaya zaidi ni kuivunjia heshima ya Muislamu bila ya haki)) [9]. Na katika Hadithi nyingine: ((Hakika miongoni mwa madhambi makubwa zaidi ni mtu kuivunjia heshima ya Muislamu bila ya haki)) [10].

Pia kutoka kwa Ibn Masoud (R.A) kwamba Mtume (S.A.W) amesema: ((Riba ina milango sabini na tatu, mlango wake mwepesi zaidi ni kama mtu kuzini na mama yake, na hakika riba mbaya zaidi ni kuivunja heshima ya Muislamu))[11]. Kadhalika, Bibi Aisha (R.A) amepokea kuwa Mtume (S.A.W) alisema: ((Hakika riba mbaya zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu ni kuhalalisha heshima ya Muislamu)), kisha akasoma: { Na wale wanao waudhi Waumini wanaume na wanawake pasina wao kufanya kosa lolote, bila ya shaka wamebeba dhulma kubwa na dhambi zilio dhaahiri.} [Al-Ahzab: 58] [12].

Wanazuoni wamebainisha kuwa kuivunjia heshima watu ni dhambi kubwa zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko uzina kwa sababu inagusa haki za waja. Pia, wanaowanyanyasa wanawake wanafananishwa na wanafiki; kwani Wanazuoni wamesema kuwa kauli ya Mungu: {Na wale ambao nyoyoni mwao mna maradhi} inahusu wanafiki wasioacha kuwaudhi wanawake [13].

Aidha, unyanyasaji ni jinai [14] katika sheria ya Misri, iwe ni kwa maneno au vitendo.

Tutapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Unyanyasaji ni jinai, dhambi kubwa, na tabia ya kinafiki.

Uislamu umetoa onyo la adhabu kali duniani na akhera kwa mnyanyasaji.

Unyanyasaji wa maneno au vitendo ni kosa la jinai kisheria.

 

[1] E'radh: Utu na heshima ya mwanadamu.

[2] Haramu kwenu: Ina utukufu usiopaswa kukiukwa.

[3] Sindano (Al-Mikhyat): Chombo cha kushonea.

[4] Imepokelewa kutoka kwa Ar-Ruyani (2/323) na At-Tabarani (20/211)

[5] (Al-Ham'ah): Udongo mweusi wenye harufu mbaya.

[6] Imepokelewa kutoka kwa At-Tabarani (8/205)

[7] Imepokelewa kutoka kwa Ahmad (15/192).

[8] Umdat al-Qari Sharh Sahih al-Bukhari, cha al-Ayni (23/157).

[9] Imepokelewa kutoka kwa Ahmad katika "Musnad" yake (3/190), na Abu Dawud katika "Sunan" yake.

[10] Imepokelewa kutoka kwa Abu Dawud katika “Sunan” yake.

[11] Imepokelewa kutoka kwa Al-Hakim katika “Al-Mustadrak” (2/43).

[12] Imepokelewa kutoka kwa Al-Bayhaqi katika “Shu’ab Al-Iman” (9/79).

[13] Funguo za Yasiyoonekana na Al-Razi (25/184), na Tafsiri ya Al-Baydawi (4/238).

[14] "Alilifanya kuwa kosa la jinai": Aliona jambo hilo kuwa kosa linalostahili adhabu.

Share this:

Related Fatwas