Kanuni za Michezo ya Kielektroniki
Question
Nini hukumu ya kucheza michezo ya kielektroniki?
Answer
Kucheza michezo ya kielektroniki kunaruhusiwa kisharia ikiwa kunamletea mtoto faida na hakumsababishii madhara yeye au jamii yake. Ni haramu ikiwa inamdhuru mtoto na kuathiri nafsi yake, afya yake, na akili yake; kwa kupandikiza vurugu, uhasama, na kupenda kutenda uhalifu dhidi ya jamii na nchi yake. Wazazi lazima wakabiliane na hatari ya michezo hii kwa kuchagua inayofaa umri wa mtoto na inayompa faida, kwa sharti isiwe na jambo lolote lililoharamishwa kisharia au kimaadili. Msimamizi anapaswa pia kufuatilia kila wakati tabia na maadili ya mtoto wakati wa kucheza.
Maelezo
Inajulikana kuwa nafsi ya mtoto imeumbwa kwa kupenda mchezo na furaha. Sharia ya Kiislamu imeruhusu michezo yenye faida ya kielimu kwa mtoto; ili awe na mchango chanya katika kutumikia dini na jamii yake. Kutoka kwa Ibn Umar (R.A) kwamba Mtume (S.A.W) alisema: ((Wafundisheni watoto wenu kuogelea, kurusha mishale, na mwanamke kusokota nyuzi)) [1].
Imepokelewa kutoka kwa Anas bin Malik (R.A) amesema: ((Mjume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) alikuwa akiingia kwetu, nami nilikuwa na mdogo wangu wa kiume, naye alikuwa na ndege mdogo (Nughar) akicheza naye, basi (ndege huyo) akafa. Siku moja Mtume (S.A.W) akaingia akamwona ana huzuni, akasema: Kuna nini mbona Abu Umayr ana huzuni? Wakasema: Ndege wake aliyekuwa akicheza naye amekufa, Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Akasema: Ewe Abu Umayr, amefanya nini Nughair? Ewe Abu Umayr, amefanya nini Nughair?)) [2]Na Nughar ni aina ya ndege kama mbulu.
Wanazuoni wamepata faida kutokana na Hadithi hizi kwamba inajuzu kwa wazazi kumwachia mtoto michezo yenye manufaa ikiwa mchezo huo hauna kitu chochote katika mambo yaliyoharamishwa[3].
Na miongoni mwa michezo ya watoto katika zama za sasa ni: Michezo ya kielektroniki au michezo ya video, ambayo imekuwa miongoni mwa aina muhimu zaidi za michezo kwa watoto na vijana katika mazingira mengi; kiasi kwamba madaktari wa magonjwa ya akili wameifanya kuwa sababu kuu katika kugundua baadhi ya magonjwa ya akili kwa watoto, na kipengele cha msingi katika kuainisha mienendo yao.
Baadhi ya tafiti za kisayansi za hivi karibuni zimethibitisha kuwa michezo hii imegawanyika katika aina mbili:
Ya kwanza: Baadhi ya michezo hii ina chanya na faida zinazosaidia katika malezi ya watoto, kuwafundisha, na kuwapa ujuzi wa kupanga, kuratibu, na kutatua matatizo kwa haraka.
Ya pili: Mingine ina athari hasi na madhara makubwa kwa tabia za watoto na mienendo yao, kadhalika kwa afya zao na miili yao; kama michezo ya mapigano (kama "PUBG") na michezo ya kamari inayohusisha picha za utupu (picha za aibu) [4]ambayo humrithisha mtoto vurugu, migogoro, na uhasama.
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
Msimamo wa " Idara ya kutoa Fatwa " ya Misri baada ya ufafanuzi huu, ni kwamba hukumu ya kucheza michezo hii ya kielektroniki inaweza kuwa inajuzu, na inaweza kuwa haijuzu; na hiyo ni kwa namna ifuatayo:
Kwanza: Kucheza michezo hii ya kielektroniki haijuzu ikiwa kutapatikana ndani yake moja ya mambo haya:
Ikiwa itapandikiza katika nafsi ya mtoto vurugu, kupenda kutawala, na uhasama.
Ikiwa itapelekea uraibu; kiasi cha kuchukua nyakati zote za mtoto, hata asipate muda wa kudurusu, kusoma, au kuzungumza na mtu yeyote.
Ikiwa itapelekea msongo wa mawazo, wasiwasi, au kujiua.
Pili: Kucheza michezo hii ya kielektroniki kunajuzu ikiwa masharti haya yote yatatimia:
Michezo hii ya kielektroniki iwe inafaa hatua ya umri wa mtoto.
Iwe inamletea mtoto faida na kumsaidia katika kukuza vipaji au kupanua uwezo wa kiakili.
Iwe inaburudisha nafsi ya mtoto na kutosheleza hamu yake ya kucheza, kwa sharti kusiwe na mchezo wa kamari, mauaji, picha za utupu, au kizuizi chochote cha kisharia na kimaadili.
Isilete athari hasi kwa mtoto kisaikolojia au kimaadili, hivyo achaguliwe michezo inayofaa asili yake na inayompa faida katika kumjenga na kumlea.
Isichukue muda wote wa mtoto, bali iwe katika baadhi ya nyakati zinazofaa; ili mtoto asishughulishwe nayo na kuacha kutimiza wajibu na mahitaji yake, au kuathiri afya yake na akili yake.
Michezo hii iwe chini ya usimamizi wa msimamizi wa mtoto (mzazi/mlezi); ili kufuatilia tabia na maadili ya mtoto.
Michezo hii ya kielektroniki isiwe imepigwa marufuku kisheria nchini; kwa sababu inahamasisha watumiaji wake kutenda uhalifu na ujasusi dhidi ya nchi zao.
[1] Imepokelewa kutoka kwa Al-Bayhaqi katika “Shu’ab Al-Iman” (11/136).
[2] Imepokelewa kutoka kwa Ahmad katika «Musnad» yake (21/ 456)."
[3] Faida za Hadithi ya Abu Umair na Imam Ibn al-Qass al-Shafi’i (uk. 16).
[4] Mambo ya aibu (Picha za utupu)»: Ni picha au matendo ambayo Sharia Tukufu imeharamisha kuyaangalia; kama vile kumtazama mwanamume na mwanamke wakiwa katika tendo la ndoa na mfano wake.
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
