Mipaka ya Kuamiliana Mwanaume na Mwanamke
Question
Ni ipi mipaka ya Kuamiliana na wenzangu (wanawake) kazini au chuoni?
Answer
Mchanganyiko na Kuamiliana baina ya wanaume na wanawake katika shule, vyombo vya usafiri, na maeneo mengine ya umma hauna kizuizi kisharia maadamu uko ndani ya mipaka ya adabu na mafunzo ya Kiislamu, na mwanamke amevaa kwa kusitiri mwili wake, na kwa sharti kuwa mwanamume na mwanamke wajilazimishe kuhifadhi mipaka ya Mwenyezi Mungu katika kutazama, kusikia, na hisia, na waepukane na faragha (khalwa) ya kisheria ambayo hairuhusiwi isipokuwa baina ya maharimu; Mwenyezi Mungu (S.W.) Amesema: {Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao na walinde tupu zao; hili ni takaso zaidi kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye khabari za yale wanayoyafanya} [An-Nur: 30].
Ama kuhusu mazungumzo baina ya mwanaume na mwanamke kwenye mitandao ya kijamii (Internet); pia yanaruhusiwa lakini kwa masharti yaliyowekwa na Wanachuoni, nayo ni kama ifuatavyo:
Mazungumzo baina yao yawe kwa kadiri ya haja na ndani ya mipaka ya dharura; ili yasiwe sababu miongoni mwa sababu za uharibifu na fitina.
Mazungumzo baina yao yasiwe ni sehemu ya kupoteza muda bila faida, yakawa ni mlango miongoni mwa milango ya wasiwasi wa shetani.
Mwanamke asitume picha zake kwa mtu asiyemjua; kwa ajili ya kujilinda nafsi yake na heshima yake ili zisitumike na mmoja wa watu waliohirika kwa namna inayomvunjia heshima.
Maelezo
Mchanganyiko na muamala baina ya wanaume na wanawake katika shule, vyuo vikuu, vyombo vya usafiri, na maeneo mengine ya umma hauna kizuizi Kisharia, maadamu uko ndani ya mipaka ya adabu na mafunzo ya Kiislamu, na mwanamke amevaa kwa kusitiri mwili wake, na kwa sharti kuwa mwanamume na mwanamke wajilazimishe kuhifadhi mipaka ya Mwenyezi Mungu katika kutazama, kusikia, na hisia, na waepukane na faragha (khalwa)[1] ya kisheria ambayo hairuhusiwi isipokuwa baina ya maharimu; Mwenyezi Mungu (S.W.) Amesema: {Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao na walinde tupu zao; hili ni takaso zaidi kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye khabari za yale wanayoyafanya} [An-Nur: 30].
Na wema waliotangulia (Salafus-Saalih) walifuata mkondo huo; kutoka kwa Sahl bin Sa'd (R.A.) amesema: “Wakati Abu Usayd al-Sa'idi alipofanya harusi, alimwalika Mtume (S.A.W.) na maswahaba zake, na hapakuwa na aliyewaandalia chakula wala kuwasogezea isipokuwa mkewe, Umm Usayd...)) Imepokelewa na Bukhari.
Hadithi hii inaashiria kuruhusiwa kwa mchanganyiko wa wanaume na wanawake katika sehemu moja pale kunapokuwa na usalama dhidi ya fitina[2].
Na kutoka kwa Abu Juhayfa (R.A.) amesema: “Mtume (S.A.W) aliunganisha udugu baina ya Salman na Abu Darda; Salman akamtembelea Abu Darda, akamwona Umm Darda akiwa amevaa nguo duni (za kufanyia kazi/asiyejipamba), akamuuliza: Una nini? Akasema: Ndugu yako Abu Darda hana haja na dunia. Abu Darda akaja na kumwandalia chakula, akasema: Kula, kwani mimi nimefunga. (Salman) akasema: Mimi sili mpaka nawe ule. Akala. Ulipofika usiku, Abu Darda alitaka kusimama (kuswali), akasema: Lala. Akalala. Kisha alitaka kusimama tena, akasema: Lala. Ulipofika mwisho wa usiku, Salman akasema: Simama sasa. Wakaswali, kisha Salman akamwambia: Hakika Mola wako ana haki juu yako, na nafsi yako ina haki juu yako, na mkeo ana haki juu yako; mpe kila mwenye haki haki yake. Akamwendea Mtume (S.A.W) na kumtajia hayo, Mtume (S.A.W) akasema: Salman amesema kweli”[3].
Na tunaelewa kutokana na Hadithi hii kwamba: kuruhusiwa kwa mwanaume kuzungumza na mwanamke anayeruhusiwa kuolewa na mtu anayekusudiwa[4], na kumuuliza jambo ambalo lina maslahi ndani yake[5].
Hivyo, kuwepo kwa mwanaume na mwanamke sehemu moja, sawa iwe ni katika ofisi za kazi, kumbi za masomo, au mifano ya hiyo, hakuna kizuizi Kisharia ikiwa shaka itaepukika na faragha (khalwa) haitakuwepo. Kinachokatazwa kisheria ni mwanamume kuwa faragha na mwanamke sehemu ambayo haiwezekani mtu hawezi kuingia sehemu hiyo[6]. Kutoka kwa Anas bin Malik (R.A.) amesema: “Mwanamke mmoja miongoni mwa Ma-Answari alikuja kwa Mtume (S.A.W.), akajitenga naye kando (akazungumza naye faragha), akasema: Wallahi, hakika nyinyi (Ma-Answari) ni katika watu ninaowapenda zaidi”[7].
Hadithi hii inaonyesha kuwa Mtume (S.A.W.) alijitenga na mwanamke huyo pembeni kidogo, lakini watu walikuwa wakiwaona, bali hata walisikia kauli yake (S.A.W.).
Ama kuhusu mazungumzo baina ya mwanamume na mwanamke kwenye mitandao ya kijamii na programu mbalimbali za intaneti, pia yanaruhusiwa lakini kwa masharti yaliyowekwa na wanachuoni, nayo ni kama ifuatavyo:
Mazungumzo baina yao yawe kwa kadiri ya haja na ndani ya mipaka ya dharura; ili yasiwe sababu miongoni mwa sababu za uharibifu na kufungua milango ya fitina. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: {Na saidianeni katika wema na ucha-Mungu, wala msiidiane katika dhambi na uadui. Na mcheni Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu} [Al-Maidah: 2].
2- Mazungumzo baina yao yasiwe ni sehemu ya kupoteza muda na kuutumia bila faida, yakageuka na kuwa mlango miongoni mwa milango ya wasiwasi wa shetani na nafsi yenye kuamrisha maovu; Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: {Na wale ambao wanajitenga na mambo ya upuuzi} [Al-Mu’minun: 3].
3- Mwanamke asitume picha zake kwa mtu asiyemjua; kwa ajili ya kuilinda nafsi yake na kuhifadhi heshima yake ili asitokee mmoja wa watu walipotoka au washenzi akaitumia kwa namna inayomvunjia heshima.
Tunapata faida Kutokana na yaliyotangulia:
Mchanganyiko na kuamiliana baina ya wanaume na wanawake katika Shule, Vyuo Vikuu, Vyombo vya Usafiri, na maeneo mengine ya umma hauna kizuizi Kisharia, maadamu uko ndani ya mipaka ya adabu na mafunzo ya Kiislamu.
Kunatakikana kwa kila mmoja, mwanaume na mwanamke, kujilazimisha katika kuamiliana kwa kuhifadhi mipaka ya Mwenyezi Mungu katika kutazama, kusikia, na hisia, na waepukane na faragha (khalwa) ya kisheria ambayo hairuhusiwi isipokuwa baina ya maharimu.
Mazungumzo baina ya mwanaume na mwanamke kwenye mitandao ya kijamii na programu mbalimbali za intaneti ni jambo linaloruhusiwa kisharia, kwa sharti kuwa mazungumzo hayo yawe ndani ya mipaka ya kazi na manufaa, na yasiwe ni kupoteza muda kunakopelekea kutumbukia katika fitina na mfano wa hayo.
Kunapasa kwa mwanamke kuhakikisha hatumi picha zake kwa mtu asiyemjua; kwa ajili ya kuilinda nafsi yake na kuhifadhi heshima yake ili asitokee mmoja wa watu waliopotoka au washenzi akazitumia kwa namna inayomvunjia heshima.
[1] "Khalwa" (Faragha): Ni mwanamume na mwanamke kuwa sehemu moja ambayo hakuna anayewaona na hakuna mwingine anayeweza kuingia kwao, kama chumba cha kulala na mfano wake. Faragha inaweza kuwa haramu ikiwa mkutano kati ya mwanamume na mwanamke ajinabi (asiye maharimu) utatokea kiasi kwamba kwa kawaida kutiliana shaka hakuwezi kuepukika.
[2] Sharh Swahiyh al-Bukhari cha Ibn Battal (6/53), na Fathul-Baari cha Ibn Hajar (9/251).
[3] Imepokelewa na Bukhari.
[4] "Mwanamke Ajinabi": Yaani si miongoni mwa maharimu wa mwanamume. Na maharimu wa mwanamume ni: Mke, na kila mwanamke ambaye ni haramu kumuoa daima; kama mama, dada, mama mkubwa, mama mdogo, na mfano wa hao.
[5] Fathul-Baari cha Ibn Hajar (4/211).
[6] Ihkamul-Ahkam Sharh 'Umdatil-Ahkam (2/181).
[7] Imepokelewa na Bukhari.
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
