Hukumu ya kununua pipi za Maulidi (Halawat Al-Mawlid) na kupeana zawadi
Question
Je, ni ipi hukumu ya kununua pipi na kupeana zawadi katika Maulidi ya Mtume (S.A.W.)?
Answer
Kuadhimisha Maulidi ya Mtume (S.A.W.) ni jambo linalopendekezwa kisharia, na hilo ndilo walilokubaliana nalo walio wengi miongoni mwa Wanazuoni. Na miongoni mwa vitu alivyokuwa akivipenda Mtume (S.A.W.) ni pipi (vitu vitamu) na asali; hivyo basi, inajuzu kwa watu kupeana zawadi za pipi miongoni mwao katika kumbukumbu ya mazazi yake (S.A.W.).
Wala haisihi kusemwa kuwa: Kununua pipi na kupeana zawadi katika kumbukumbu ya mazazi yake (S.A.W.) ni uzushi (bida’a) na upotevu; kwani maneno hayo ni batili na yanapingana na yale walilokubaliana nalo walio wengi katika Umma.
Maelezo
Kuadhimisha kumbukumbu ya Maulidi ya Mtume (S.A.W.) na kufurahia jambo hilo ni miongoni mwa matendo bora na mambo makuu ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu (S.W.). Walio wengi miongoni mwa wanazuoni wa Umma (Jamhur) wamekubaliana juu ya kupendekezwa kuhuisha kumbukumbu hii kwa namna zote za furaha na bashasha, na kwa kila kheri ya kumtii Mwenyezi Mungu inayomkurubisha mja Kwake.
Ama kuhusu desturi ya watu kununua pipi na kupeana zawadi katika Maulidi ya Mtume (S.A.W.) kwa ajili ya kufurahia mazazi yake na kupenda kile alichokuwa akikipenda: basi ni jambo hilo linapendekezwa kisharia[1]. Kutoka kwa Bibi Aisha (R.A.) amesema: “Mtume (S.A.W.) alikuwa akipenda vitu vitamu (Halwa) na asali” [Imepokewa na Al-Bukhari].
Kitendo hiki cha watu kununua pipi na kupeana zawadi kinahesabika kuwa ni sunna njema; kwani kupeana zawadi ni jambo linalopendekezwa katika Sharia tukufu; Mtume (S.A.W.) amesema: “Peaneni zawadi, mtapendana”[2].
Ama kwa wale wanaosema kuwa kununua pipi na kupeana zawadi katika siku ya Maulidi ni uzushi na upotevu ambao haukuwepo katika Sunna ya Mtume, jibu la maneno haya ni kama ifuatavyo:
Kwanza: Haya ni maneno batili yanayoonyesha ujinga wa wasemaji wake kuhusu Sharia tukufu. Badala yake, wanazuoni wa Umma wa kale na wa sasa wamekuwa wakiadhimisha siku ya mazazi yake (S.A.W.).
Pili: Miongoni mwa namna za maadhimisho ya wanazuoni wa Kiislamu katika kumbukumbu ya Maulidi ilikuwa ni kununua pipi na kupeana zawadi ili kuingiza furaha katika nyoyo za waumini. Kutoka kwa Abdullah bin Umar (R.A.), “Kwamba mtu mmoja alikuja kwa Mtume (S.A.W.) akasema: Ewe Mtume, ni watu gani wanaopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu? Na ni matendo gani yanayopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu? Mtume (S.A.W.) akasema: Watu wanaopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu ni wale wenye manufaa zaidi kwa watu, na tendo linalopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu ni furaha unayoingiza kwa Muislamu”.[3]
Tatu: Imethibiti katika Sunna kuwa Mtume (S.A.W.) alikuwa akipenda vitu vitamu, hivyo basi inapendekezwa kisharia kwa watu kuadhimisha kumbukumbu ya mazazi yake kwa kile alichokuwa akikipenda (S.A.W.) ikiwemo kupeana zawadi za pipi miongoni mwao.
Nne: Imekuja katika baadhi ya habari kuwa Abu Lahab—kafiri aliyekuwa akimuudhi sana Mtume (S.A.W.)—hupunguziwa adhabu Motoni kila usiku wa Jumatatu; kwa sababu mjakazi wake, Thuwaybah, alipombashiria[4] kuhusu mazazi ya Mtume (S.A.W.), alimwacha huru (alimfanya muungwana)[5] kwa ajili ya furaha ya kuzaliwa kwa mtoto wa ndugu yake, Abdullah—baba wa bwana wetu Muhammad (S.A.W.)—[6]. Ikiwa ni hivyo, basi ni bora zaidi kwa Muislamu anayempenda Mtume (S.A.W.) kulipwa thawabu kwa kuadhimisha mazazi yake (S.A.W.) kupitia kuhuisha kumbukumbu hii tukufu kwa kila namna ya utii na kheri, ikiwemo kupeana zawadi miongoni mwa watu kwa kile alichokuwa akikipenda Mtume (S.A.W.) ambacho ni kula pipi na asali.
Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:
1- Kuadhimisha Maulidi ya Mtume (S.A.W.) ni jambo linalopendekezwa kisharia, na hilo ndilo walilokubaliana nalo walio wengi miongoni mwa wanazuoni.
2- Miongoni mwa vitu alivyokuwa akivipenda Mtume (S.A.W.) ni pipi (vitu vitamu) na asali; hivyo basi, inajuzu kwa watu kupeana zawadi za pipi miongoni mwao katika kumbukumbu ya mazazi yake (S.A.W.).
Wala haisihi kusemwa kuwa: Kununua pipi na kupeana zawadi katika kumbukumbu ya mazazi yake (S.A.W.) ni uzushi (bida’a) na upotevu; kwani maneno hayo ni batili na yanapingana na yale waliyoyakubali walio wengi katika Umma.
[1] «Husn al-Maqsid fi 'Amal al-Mawlid» ndani ya kitabu «Al-Hawi lil-Fatawi» cha Al-Suyuti (1/ 230).
[2] Imepokelewa na Malik katika «Al-Muwatta» (2/ 908).
[3] Imepokelewa na Al-Tabarani katika «Al-Mu'jam al-Awsat» (6/ 139).
[4] «Alimbashiria»: Alimpa habari njema.
[5] «Alimfanya muungwana»: Alimpa uhuru wake.
[6] «'Umdat al-Qari Sharh Sahih al-Bukhari» (20/ 93).
Arabic
Englsh
French
Deutsch
Urdu
Pashto
Hausa
