Kupata thawabu kwa kusoma Qur’ani T...

Egypt's Dar Al-Ifta

Kupata thawabu kwa kusoma Qur’ani Tukufu wakati wa Ramadhani kwa wale wasiofunga kwa udhuru.

Question

Je, mwenye kufuturu kwa udhuru anapata thawabu kwa kusoma Qur`ani Tukufu katika mwezi wa Ramadhani?

Answer

Kusoma Qur’ani Tukufu katika mwezi wa Ramadhani kuna thawabu kubwa, na hii ni miongoni mwa matendo mema ambayo anapata thawabu kwa mwenye kuyafanya. Thawabu ya mwenye udhuru ambaye hakuweza kufunga hayapungui kwa thawabu ya mwenye afya anayefunga, na hilo haliathiri matendo yake mengine ya wema.

Maelezo

Kufunga ni miongoni mwa faradhi za Uislamu, na Mwenyezi Mungu Mtukufu ameifanya kuwa ni tegemezi kwa uwezo. Ikiwa Muislamu hawezi kufunga, kwa sababu hawezi kufanya hivyo au inamsababishia shida ambayo hawezi kuibeba, basi ana ruhusa ya kufungua. Mwenyezi Mungu Mtukufu Amesema: {Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya iwezavyo} [Al-Baqarah: 286], na Mwenyezi Mungu Mtukufu kasema khasa kuhusu kufunga na kuondoa ubaya kwa wale wasio na uwezo wa kufanya hivyo: {Mwenyezi Mungu anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito} [Al-Baqarah: 185], imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah (R.A), kwamba Mtume (S.A.W) amesema: “Na nitakapokuamrisheni kufanya jambo, lifanyeni kadiri muwezavyo.” Hadithi hii imekubaliwa. Mwenyezi Mungu Mtukufu Amesema: {Na atakaye kuwa miongoni mwenu mgonjwa au yumo safarini basi atimize hisabu katika siku nyengine. Na wale wasio weza, watoe fidiya kwa kumlisha masikini.}. [Al-Baqarah: 184], maana yake ni kwamba Muislamu ambaye anawajibika na ana maradhi ambayo yanategemewa kupona na ambayo yanamzuia kufunga, na vile vile msafiri, anaruhusiwa kufungua Ramadhani. Kisha ni lazima waifidie baada ya kuondolewa udhuru na wawe na uwezo wa kufunga.

Kusoma Qur’ani Tukufu ni ibada miongoni mwa ibada bora zaidi ambazo mtu hujikurubisha nazo kwa Mola wake. Imesimuliwa kutoka kwa Anas (R.A) kwamba Mtume (S.A.W) amesema: “Ibada bora zaidi ni kusoma Qur’an” (Imesimuliwa na Abu Al-Fadhl Ar-Razi katika “Fadha’il Al-Qur’an”, na Ad-Dailami katika “Musnad Al-Firdaws”, na Imamu As-Suyuti ameitaja katika “Al-Jami’”). Kwa hivyo, kujishughulisha na kusoma Qur’ani Tukufu ni bora kuliko kujishughulisha na adhkari zote isipokuwa zile ambazo zimekuja na mambo ya pekee.

Imepokelewa kutoka kwa Abdullah Ibn Mas’ud (R.A) amesema kwamba Mtume wa Allah (S.A.W) amesema: “Yeyote anayesoma herufi moja kutoka Kitabu cha Allah ana thawabu moja, na thawabu moja ni mara kumi ya mithili yake. Sisemi ‘Alif-Lam-Mim’ ni herufi moja, lakini Alif ni herufi, Lam ni herufi, na Mim ni herufi” (Imesimuliwa na Tirmidhi katika “Sunan” yake).

Imepokelewa kutoka kwa Abu Umamah Al-Bahili (R.A) amesema: “Nilimsikia Mtume wa Allah (S.A.W) akisema: ‘Somani Qur’an, kwa hakika itakuja Siku ya Qiyama ikiwa ni mwombezi kwa wasomaji wake’” (Imesimuliwa na Muslim katika “Sahih” yake).

Mwezi wa Ramadhani ni miongoni mwa misimu ya ibada na wema, na miongoni mwa ibada zinazojulikana zaidi ndani yake ni kufunga, kuswali Swala ya usiku, na kusoma Qur’ani Tukufu. Ikiwa kumaliza kusoma Qur’ani Tukufu ni miongoni mwa mambo yanayopendekezwa, basi katika mwezi wa Ramadhani ni yenye kustahiki zaidi na yenye thawabu kubwa zaidi.

Kufungua katika mchana wa Ramadhani kwa sababu ya udhuru wa kisharia hakuathiri ibada na matendo mema ya Muislamu, na thawabu yake kwa Allah iko thabiti bila ya kupunguzwa. Allah ndiye Mwenye kuwafadhili waja Wake kwa thawabu na malipo.

Mwenye udhuru ambaye hakuweza kufunga ana thawabu yake katika matendo ya wema na mengineyo ambayo Muislamu anapata thawabu kwayo kama thawabu ya mwenye afya anayefunga. Hii ni kwa sababu kuzuiwa kufunga kulikuwa ni jambo lililo nje ya uwezo wake. Fadhila za Mwenyezi Mungu Mtukufu -Naye ndiye Mkarimu kuliko wakarimu wote- ni pana zaidi kiasi kwamba haziwezi kumbana yule mwenye udhuru na kumpunguzia ujira wake au kumhesabu kwa kiwango cha amali yake, bali humhesabu kwa kiwango cha fadhila Zake Yeye (Mwenyezi Mungu) aliyetakasika. Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin ‘Amr bin Al-‘As (R.A) kwamba Mtume wa Allah (S.A.W) amesema: “Hakika mja ikiwa alikuwa kwenye njia nzuri ya ibada, kisha akaugua, ikasemwa kwa malaika aliyemudu: ‘Andika kwake sawa na tendo lake alipokuwa huru, hadi nitakapomudu au nimudu kwangu’” (Imesimuliwa na Imamu Ahmad katika “Musnad” yake).

Pia imesimuliwa kutoka kwa Anas Ibn Malik (R.A) kwamba Mtume wa Allah (S.A.W) amesema: “Ikiwa Allah akimtahini mja Mwislamu kwa balaa katika mwili wake, Allah anasema: ‘Andika kwake matendo yake mema aliyokuwa akiyafanya. Akimponya humwosha na kumtakasa, na akiichukua (nafsi yake) humsamehe na kumrehemu.” (Imesimuliwa na Imamu Ahmad katika “Musnad” yake).

Pia imesimuliwa kutoka kwa Ibrahim Abu Isma’il As-Saksaki kwamba alisikia Abu Burdah akisema: “Yazid Ibn Abi Kabshah na yeye walikuwa wamesafiri pamoja, na Yazid alikuwa akifunga wakati wa safari. Abu Burdah akamwambia: ‘Nilimsikia Abu Musa mara nyingi akisema: Mtume wa Allah (S.A.W) amesema: “Ikiwa mja akaugua au akasafiri, anaandikiwa sawa na alivyokuwa akifanya akiwa mkazi mwenye afya”’” (Imesimuliwa na Bukhari katika “Sahih” yake).

Ikiwa Mwenyezi Mungu Mtukufu amempa mwenye udhuru asiyeweza kufunga ujira wa waliofunga, basi atapata malipo ya matendo mema anayoyafanya, na atapata malipo ya kusoma Qur’ani Tukufu kama malipo ya mfungaji anayesoma Qur’ani Tukufu. Iwapo Muislamu atazuiliwa kufanya matendo mema kwa udhuru kama vile ugonjwa, safari, au sababu nyingine, basi atapata malipo kamili kama alivyokuwa akifanya kabla ya hapo.

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia;

Kusoma Qur’ani Tukufu katika mwezi wa Ramadhani kuna thawabu kubwa, nayo ni miongoni mwa matendo mema ambayo anapata thawabu kwa mwenye kuyafanya.

Thawabu ya mwenye udhuru ambaye hakuweza kufunga haipungui ni kama thawabu ya mwenye afya anayefunga, na hilo haliathiri matendo yake mengine ya wema.

Share this:

Related Fatwas