Hukumu ya Kutumia Vyombo vya Muziki...

Egypt's Dar Al-Ifta

Hukumu ya Kutumia Vyombo vya Muziki.

Question

Ni ipi hukumu ya kutumia vyombo vya muziki kwa ajili ya burudani na kuvisikiliza? 

Answer

Sifa zote njema ni za Allah pekee, na swala na salam ziwe juu ya Bwana wetu Muhammad Mtume wa Mwenyezi Mungu, na pia juu ya aali zake na maswahaba wake, na juu ya wale wanaowafuata kwa wema mpaka Siku ya Malipo.
Uislamu ni dini ya kweli ambayo haina ibara za kubuni, haukulazimisha kwa wanadamu kuwa maneno yao yote yawe ni kumtaja Mwenyezi Mungu, wala ukimya wao wote uwe ni kufikiria utukufu wa Mwenyezi Mungu, wala wote wanayoyasikia ni Qur`ani, lakini Uislamu ulifahamu maumbile yao na silika zao ambazo Mwenyezi Mungu amewaumba nazo, na Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwaumba wafurahi na wacheza. Sisi tunao mfano mwema kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. aliyekuwa akisimama kuswali muda mrefu kutoka usiku hadi miguu yake ikivimba, ingawa hivyo, alikuwa akipenda vizuri, akitabasamu, akicheka, na hakusema chochote isipokuwa kwa ukweli, na vivyo hivyo masahaba walikuwa wakicheka na kudhihaki, wakijua bahati ya nafsi zao ili kujiburudisha, kwa sababu kama mioyo ikitaabika itachoka [252 / Al-Halal wal Haram fi Islam kwa Al-Qaradhawi / Maktabat Wahbah].
Vyombo vya muziki ni kama sauti za kiBin adamu sauti ambazo ni nyimbo, na wimbo ni jambo zuri kwa mtu, uliyoundwa na Mungu siku ambayo Mwenyezi Mungu aliumba, na asili yake ni kwa sababu ya sauti hizi zinazotofautiana kwa nguvu na athari zake kama sauti za radi, mvua, na mshindo wa bahari, na sauti zingine za wanyama na ndege, sauti laini na nyepesi wakati mwingine, na hulia wakati mwingine, kama vile farasi, ngamia, kubweka kwa mbwa, kuimba kwa kore (ndege) na yote ambayo mtu amesikia tangu utoto wake, na hata mtoto hukataa sauti ya honi ya basi na kwayo hujisikia vibaya, na hupenda sauti ya ndege na hutulia na kulala, kwa hivyo mtu wa kwanza aliepuka kile alichokataa kutokana na sauti hizi, na kujaribu kuiga kile ambacho hakukikataa, na kisha akaunga baadhi ya sauti, kwa hivyo akaunda nyimbo ambazo zilielezea furaha au huzuni, kisha hivi karibuni akagundua chombo cha kuutuliza mwili wake kutokana na kuiga sauti, kisha akashirikisha kati ya sauti yake na sauti ya chombo, na huu ulikuwa muingiliano mpya na kazi ya furaha, kwa hivyo kukawa kuimba kunahusishwa na vyombo vya muziki . [7 / Utangulizi wa kitabu Farah Al-Asmaa na Mohamed Al-Rahmouni / Ad-Dar Al-Arabiya Lil Kitab].
Kuimba ni maneno mazuri, ama kwa sauti ile ile au kwa chombo maalumu, na nyimbo ziko aina mbalimbali. Baadhi yake husababisha kulia na kukonda, nayo ni miongoni mwa mashairi ya mapenzi, kutamani kurudi nyumbani na kulia juu ya ujana, maombolezo na kutopenda matamanio, baadhi ya nyimbo hizi zinaburudisha masikio, nazo zinazohusiana na kusifia vinywaji, na kutaja vikao. Na baadhi zake ni zile zinazoburudisha na kuipa raha roho, kama vile kuelezea miti, maua, mbuga na uwindaji, na baadhi yake hufurahisha, na kuhimiza ukarimu, nazo zinazohusiana na kusifu na fahari, na baadhi yake zinazotia moyo, nazo zinazohusiana na vita, na kutaja matukio na uvamizi, wafungwa na kadhalika na hizi zote zinaitwa nyimbo. [4/9 / Al-Mukhasas kwa Ibn Saydah / Dar Ihyaa At-Turath Al-Arabiy]
Lakini ni vizuri kufahamu hukumu ya kusikiliza vyombo vya muziki kwa kusudi la kujiburudisha, kwanza tunaweka wazi ufafanuzi wake, kisha nadharia za wanavyuoni na dalili zao.
Muziki katika lugha ni: vyombo vya kujiburudisha, kama vile kupiga dufu na vyombo vingine vya muziki, na mwanamuziki ni yule anayevipiga vyombo hivi na mwimbaji, na katika Hadithi iliyopokelewa kutoka kwa Al-Bukhari kutoka kwa Aisha R.A., kwamba “Vijakazi wawili walikuwa wakiimba nyimbo za Al-Ansaar katika siku ya Buaath”. [2928, 2929 / 4 / Lisan Al-Arab / Dar Al-Maarif].
Vyombo vya Muziki: ni vyombo ambavyo hupigwa juu yake, kama vile ngoma, difu, oudi na piano, au hupigwa ndani yake, kama vile zumari na tarumbeta, kwa hivyo hutoka sauti ambazo ni sawa na sauti za uimbaji hufanywa na mpigaji au mpulizaji. [28 / Al-Ghinaa wal Musiqa kwa Abdullah Al-Jadeea / Muasastur Rayyan].
Kuhusu maneno ya nyimbo kama yataiendea dhambi basi ni haramu kwa mujibu wa makubaliano ya wanavyuoni, hata kama hayakuimbwa. Abu Hamid Al-Ghazaliy alisema: (Kiwango cha tatu: maneno yenye uzani yenye kufahamika nayo ni mashairi, na hayo hayatoke isipokuwa kwenye koo la mwanadamu tu, kwa hivyo maneno hayo yanaruhusiwa, na inaangaliwa maana ya maneno hayo. Kama yakiwa na uharamu, basi ni haramu kupangwa, na hairuhusiwi kuyatamka, yakiwa kwa kuimba au pasipo na kuimbwa, na haki yake ni kama alivyosema Imamu Shafi – Mwenyezi Mungu amrehemu - wakati aliposema: “Ushairi ni maneno, mazuri yake ni mazuri na mabaya yake ni mabaya.” Kama kwamba ushairi unaruhusiwa kuimbwa bila sauti na vyombo vya muziki, inaruhusiwa vilevile kuimbwa pamoja na vyombo vya muziki, ikiwa vitu vinavyoruhusiwa vikijumuishwa pamoja basi vyote vinaruhusiwa, isipokuwa miongoni mwake ni kitu kilichokatazwa, katika suala letu hili hakuna chochote kilichokatazwa, na namna gani ushairi ukataliwe kuimbwa, na uiliimbwa mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, S.A.W., imepokelewa kutoka kwa Abu Hurairah, kwamba Umar alipita kwa Hassan wakati alipokuwa akiimba shairi msikitini, kwa hivyo akamwangalia, na Hassan akasema: Nilikuwa nikiimba na ambaye aliyekuwepo msikitini ni mbora kuliko wewe [6/1128 / Ihyaa Ulumu Ad-Dini / Dar Ash-Shaab].
Inaruhusiwa kuimba bila ya chombo kulingana na maoni ya wanavyuoni wengi, isipokuwa maneno ya nyimbo hizi ni marufuku kama vile kumsifia mwanamke na kadhalika. Abu Al-Mawahib Al-Shazliy Al-Tunisiy alisema: Imepokewa kutoka kwa kikundi cha Masahaba, R.A., na kutoka kikundi cha wafuasi wa Masahaba, na miongoni mwa Masahaba ni: Omar Bin Al-Khatwab, Othman Bin Affan na Abu Obeida Bin Al-Jarrah, Bilal, Abdullah Bin Omar, Hassan Bin Thabit, Aisha, mama wa Waumini na wengineo, na kati ya wafuasi ni: Said Bin Al-Musayyib, Salim Bin Abdullah Bin Omar Bin Al-Khatwab, na Shuraih Al-Qadi, Said Bin Jabir, Omar Bin Abdul Aziz na wengineo, na wasio wafuasi miongoni mwa wanavyuoni wenye kujitahidi nao ni: Ibn Juraij na Al-Anbariy na imepokewa hivyo kutoka kwa: Malik, Shafiy, Abu Hanifa, Ahmed Bin Hanbal, Sufyan Bin Uyaynah, Abu Bakr Bin Mujahid, na rai hiyo imechaguliwa kutoka Madhehebu ya Shafiy Bw. Abu Mansour Al-Baghdadiy, na Bw. Abu Al-Qasim Al-Qashiriy, na Imam wa Misikiti miwili mitakatifu na Al-Mawardiy, na Al-Ruwianiy. Al-Ghazaliy alitaja makubaliano juu ya rai hiyo, na Al-Qadhi Abu Bakr Bin Al-Arabiy akaichagua kutoka kwa madhehebu ya Malik, na akataja hivyo katika kitabu chake cha Ahkaam Al-Qur`ani. Na ilichaguliwa (rai hiyo) kutoka kwa wanavyuoni wa Madhehebu ya Ahmad Bin Hanbal kutoka kwao ni: Al-Khilal: mwandishi wa kitabu cha Al-Jamii, ambayo ni Madhehbu ya Dhahiriya, iliyotajwa na Ibn Hazm na kuainisha, na Ibn Twahir Al-Maqdisi na alitaja makubaliano ya Masahaba na wale wafuasi juu yake, Ibn Qutaybah na Taj Al-Din Al-Fazari: Mufti wa madhehebu ya Shafiy na mwanachuoni wake katika Damasca, wametaja makubaliano ya wanachuoni wa Miskiti miwili mitakatifu. Na mwandishi wa kitabu cha: [An-Nihayah fi Sharhi Al-Hidaya] kutoka madhehebu ya Hanafiy ametaja hivyo pia, na kwa rai hiyo Imam Al-Sarkhasi alichukua, na ametoa dalili kwamba Ansa: Rafiki yake Mtume wa Mwenyezi Mungu, S.A.W., alikuwa akifanya hivyo, na akaichagua rai hiyo kutoka kwa Maimamu waliokuja baadaye ni, Imam Izz Al-Din Abd Assalam Shafiy [50:49/ Farah Al-Asmaa Birukhas Al-Samaa / Ad-Dar Al-Arabiyah lil Kittab].
Vyombo vya muziki hutoa sauti nzuri ya kuimba, na sauti nzuri bila shaka inaruhusiwa kusikiliza, Mtume wa Mwenyezi Mungu alisema katika Hadithi hiyo iliyopokelewa kutoka kwa Al-Tirmidhiy: “Mwenyezi Mungu Hakutuma Nabii isipokuwa sauti yake ni nzuri.” Na katika Hadithi nyingine iliyopokelewa kutoka kwa Ahmad na Ibn Majah kutoka kwa Mtume S.A.W.: “Allah anasikia mwenye kusoma Qur’ani kwa sauti nzuri zaidi kuliko anayesikia mwimbaji”. Vile vile Mtume S.A.W. alisema akimsifu Abu Mussa Al-Ashaariy, kama ilivyopokelewa kutoka kwa Masheikh wawili (Al-Bukhariy na Muslim): “Hakika umepewa mzumari katika mizumari ya aali Dawud..” Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: {Hakika katika sauti mbaya zote bila ya shaka iliyo zidi ni sauti ya punda}. [LUQMAAN: 19] Aya hii maana yake inaonesha sifa nzuri ya sauti nzuri, na ikiwa inafaa kusema kuwa inaruhusiwa kusikiliza kwa sharti iwe kwenye Qur’ani tu, basi itakuwa ni marufuku kusikiliza sauti ya kinega, kwa sababu si katika sauti nzuri ya Qur'ani, na ikiwa inaruhusiwa kusikiliza sauti isiyo na maana, basi kwa nini isiruhusiwe kusikiliza sauti ambayo hufahamika kwayo hekima, na maana sahihi, na kwamba miongoni mwa maneno ya ushairi ni hekima, basi huzingatiwa sauti kwa kuwa ni nzuri tu [6/11/25 / Ihyaa Ulumu Ad-Dini / Dar Ash-Shaab].
Sauti zilizo na uzani zinafanana na kuiga sauti za wanyama, na sheria haikukataza kusikiliza sauti ya kinega, na vivyo hivyo haikukatazwa kusikiliza sauti hizi kwa uzani wake, lakini ikiwa zikiambatana na kitu kinachokatazwa, basi hukumu yake ni haramu, kana kwamba inahusishwa na vikao vya pombe au vinginevyo, [6/1127 / Ihyaa Ulumu Ad-Dini / Dar Ash-Shaab].
Dalili ya ruhusa yake na matumizi yake – muda wa kuwa haipelekei katika mambo yanayokatazwa kisheria – kutokana na Qur’ani, Mwenyezi Mtukufu amesema: {..na anawahalalishia vizuri, na ana waharimishia viovu, na anawaondolea mizigo yao na minyororo iliyo kuwa juu yao..} [AL AARAF: 157], asili ya vitu vizuri ni kuhalilishwa.
Na kauli yake Mwenyezi Mungu: {Na wanapo iona biashara au pumbao wanayakimbilia hayo na wakakuacha umesimama. Sema: Yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ni bora kuliko pumbao na biashara. Na Mwenyezi Mungu ni Mbora wa watoa riziki}[AL JUMU'AH: 11], kuhusu sababu ya kushuka kwa Aya hii ilitajwa kama msafara wao ukifika na bidhaa watu walikuwa wakiupokea kwa kuimba na kupiga dufu wakifurahia kufika kwake salama kwa upande mmoja, na wakitarajia zile faida na yale mapato yanayoletwa kutokana na msafara huu.
Al-Zamakhshari alisema katika Al-Kashaf: Msafara ulikuwa ukifika watu wanaupokea kwa ngoma na kupiga makofi, hiyo iliyokusudiwa kwa kufurahisha [537/4 / Al-Kashaf kwa Al-Zamakhshari / Dar Al-Kitab Al-Arabi].
Ibn Taher Al-Maqdisi, anayejulikana kwa Ibn Al-Qaysraniy, alisema: vijakazi walikuwa wakipiga madufu na mizumari kwa ajili ya watu ambao wanaoa, hivyo, watu walikuwa wakimwita Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. wakati alipokuwa akisimama katika Swala, kwa hivyo Mwenyezi Mungu Mtukufu akawashutumu na akasema: {Na wanapoiona biashara au pumbao wanayakimbilia hayo na wakakuacha umesimama.} [AL JUMU'AH: 11], [72 / Al-Samaa kwa Ibn Al Qaisrani / Wizara ya Waqfu - Misri] .
Katika Sunna imepokewa kutoka kwa Al-Bukhariy na Muslim kutoka kwa Aisha alisema: Abu Bakr aliingia ndani na Aisha alikuwa na vijakazi wawili katika siku za Mina, walikuwa wakipiga madufu. Na katika mapokezi mengine kwamba vijakazi hawa walikuwa wakiimba nyimbo za Ansaar katika siku ya Buath wakati Mtume (S.A.W.) alipokuwa amejifunika nguo, Abu Bakr akawakaripia vijakazi hawa, basi Mtume (S.A.W.) alifichua uso wake, na akasema: “Ewe Abu Bakr, Waache, kwa maana siku hizi ni siku za Edi”, na katika mapokezi mengine “Ewe Abu Bakr, kila watu wana Edi na hii ni Edi yetu.”
Imepokewa kutoka kwa Al-Bukhariy kutoka kwa Al-Rubai, Bin t Moawidh, alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W. alinijia asubuhi ya siku ya kuolewa kwangu, na akakaa kitandani mwangu, wakati huu vijakazi walikuwa wakipiga madufu na kuimba kuhusu aliyewaua baba zangu siku ya Badr. Mpaka alisema mmoja wa vijakazi hawa: Na miongoni mwetu ni Nabii anayejua ya kesho, basi Mtume S.A.W. akasema: “Acha haya na sema kile ulichokuwa unasema.” Katika mapokezi ya Ibn Majah Mtume S.A.W. alisema: “Kwa habari hii, usiiseme. Hakuna anayejua kitakachotokea kesho isipokuwa Allah tu. Dalili katika Hadithi hizi mbili ni kwamba kuna uimbaji unaambatana na kupiga madufu na ilitokea hivyo kutoka kwa vijakazi ndani ya nyumba ya Mtume na kwamba Aisha alimsikia hivyo na pia Mtume S.A.W. akakataa kukaripia kwa Abu Bakr kwa vijakazi hawa wawili katika Hadithi ya kwanza, baadhi ya wanavyuoni walisema kwamba Hadithi hizi mbili zinaonesha kwamba unaruhusiwa uimbaji kwa ajili ya Edi na harusi, lakini hauruhusiwi kwa kitu kingine, na wanavyuoni hawa wanajibiwa kwamba haviruhusiwi vitu vilivyokatazwa katika Eid na harusi, lakini inapanuka katika mambo mengine yanayoruhusiwa kama mapambo na kula vitu nzuri na vitu mfano wa hivyo, na kwamba inapendekezwa katika Edi na harusi kujifurahisha na kuwafurahisha watu, kwa hivyo watu wanahisi furaha, na inapimwa kwa hali hii kila tukio linalopendeza, likiwa ni kukaa pamoja na marafiki kwa ajili ya kula chakula au mfano wake.
Na imepokewa kutoka kwa Ahmad na Al-Tirmidhiy kutoka kwa Buraidah kuwa: “Mtume wa Mwenyezi Mungu, S.A.W., alitoka katika baadhi ya vita vyake. Alipokwenda, kijakazi mweusi akaja, akasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Hakika mimi nimeweka nadhiri kwa Mwenyezi Mungu ya kupiga madufu na kuimba mbele yako kama ukirudi salama, Mtume S.A.W. akamwambia: “Ikiwa uliweka nadhiri, basi upige, au uache, basi” Kijakazi akapiga madufu, na Abu Bakr akaingia wakati alipokuwa akipiga, kisha Ali akaingia wakati huo huo, kisha Uthman akaingia wakati huo huo pia, kisha akaingia Omar kijakazi akatupa dufu chini kisha akaketi juu yake, na Mtume wa Mwenyezi Mungu, S.A.W. akasema: Ewe Omar, hakika shetani anakuogopa. Nilikuwa nimekaa alipokuwa anapiga dufu. Kisha Abu Bakr akaingia, kisha Ali akaingia, kisha Uthman akaingia wakati huo huo. Lakini wakati Omar alipoingia kijakazi akatupa dufu”.
Abdullah Bin Yusuf Al-Judai alisema: Hadithi hii ni hoja yenye nguvu ya ruhusa ya kucheza na vyombo vya muziki na kuimba pasipo na makatazo, kwa sababu Mtume, S.A.W., alisema kama ilivyopokelewa kutoka kwa Al-Bukhariy na wengineo kutoka kwa Aisha kwamba alisema: “Mwenye kuweka nadhiri ya kumtii Mwenyezi Mungu basi amtii, na ambaye aliweka nadhari ya kutomtii basi asimfanye hivyo”. Na akasema kama ilivyopokelewa kutoka kwa Muslim na Ahmad kutoka kwa Imran Bin Al-Husayn-: “Hakuna kuweka nadhiri ya kutomtii Mwenyezi Mungu.” Na katika mapokezi mengine kuwa: “Hakuna kutimiza nadhiri katika kutomtii Mwenyezi Mungu.” Ikiwa kijakazi huyu angeweka nadhiri ya kufanya haramu, basi Mtume S.A.W. asingemrahisishia kutimiza nadhiri hiyo, lakini Mtume S.A.W. amemruhusu kwani kijakazi aliweka nadhiri ya kufanya jambo la halali [223, 222 / Al-Ghinau Wal-Musiqa fi Mizaan Al-Islam / Muasastur Rayan].
Imepokewa kutoka kwa Al-Bukhariy kutoka kwa Abu Musa, R.A., kwamba Mtume S.A.W. akamwambia Abu Mussa kuwa: “Ewe Abu Musa, hakika umepewa mzumari katika mizumari ya aali Dawud.” Sauti yake inafanana na sauti ya mzumari kwa uzuri wa sauti yake. Kama sauti ya mzumari ni haramu, basi Mtume S.A.W. asingeifananisha sauti yake Abu Mussa kwayo, itakuwa kuaibisha sio kuisifu.
Al-Shawkaniy alisema: Na wanavyuoni wa Madina na wale waliokubaliana nao kutoka kwa wanavyuoni wa Al-Dhahir na kundi la wasufi walisema kuwa inaruhusiwa kusikiliza uimbaji, hata pamoja na udi, na Bw. Abu Mansour Al-Baghdadiy Al-Shafiy alisema katika kitabu chake As-Samaa kwamba Abdullah Bin Jaafa alikuwa hakuona chochote kibaya kuhusu uimbaji na alikuwa akipanga nyimbo kwa vijakazi wake na kuzisikiliza kutoka kwao. Na hiyo ilikuwa wakati wa Amiri wa Waumini Ali, na Bw. huyo aliyetajwa hapo juu pia alitaja kwamba Jaji Shuraih, Said Bin Al-Musayyib, Ata Bin Abi Rabah, Al-Zuhri na Al-Shaabi. Imam wa Misikiti miwili mitakatifu alisema katika kitabu cha An-Nihayah na Ibn Abi Al-Dam kuwa: Wanahistoria wamethibitisha kwamba Abdullah Bin Az-Zubair alikuwa na vijakazi wanapiga udi, na kwamba Ibn Omar aliingia na alikuwa na udi, Ibn Omar alisema: Ewe rafiki wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W.) hii ni nini? akachukua, Ibn Omar akaiangalia na kusema: Hii ni mizani ya Sham, Ibn Al-Zubayr alisema: akili zinapimwa kwayo [5205/5 / Ibtaal Dawah Al-Ijmaa Ala Tahriim Mutlaq As-Samaa kutoka Fatwa ya Al-Shawkaniy / Dar Al-Jiil] na [8/112 / Nail Al-Awtar / Dar Al-Hadith].
Abu Bakr Bin Al-Arabiy alipozungumzia ruhusa ya uimbaji alisema kuwa: Ikiwa mtu alizidisha kile kisichokuwa katika zama za Mtume, S.A.W., udi unaopigwa kwa sauti yenye wimbo ataingia katika kauli yake: Je, mzumari wa Shetani ndani ya nyumba ya Mtume wa Mwenyezi Mungu S.A.W.?! Akasema: Waache kwani siku hii ni siku ya Edi, na kama ikiwepo pamoja kupigwa kwa udi, basi haiathiri katika kuiharimisha kwake, kwa sababu vyombo vyote vya muziki vinahusiana na mioyo ya wanyonge na roho zinaburudishwa kwake, na kutoa uzito wa taabu ambayo kila roho inaibeba. Hiyo hiyo roho ikiihusisha basi sharia imeiruhusu [282/5 / Aredhatul Ahwadhi Sharhu Sunan Al-Tirmidhi / Dar Al-Kutub Al-Alamiyah]
Sheikh Abu Al-Mawahib Al-Tunisi alisema: “Usikilizaji wa kupiga udi ulipokelewa kutoka kwa: Abdullah Bin Omar, Abdullah Bin Jaafar, Abdullah Bin Zubair, Muawiya Bin Abi Sufyan, Omar Bin Al-Aas, na wengineo, na miongoni mwa wale wafuasi ni Kharija Bin Zaid, Abdul Rahman Bin Hassan, na Said. Ibn Al-Musayyib, Ataa Ibn Abi Rabah, Al-Sha`bi, Ibn Abi Atiq, na wengi wa wanavyuoni wa Fiqhi Madinah. Vile vile Al-Marudi alisema inaruhusiwa kutoka kwa baadhi ya wanavyuoni wa Shafiy, na Bw. Abu Mansour Al-Baghdadiy, Sheikh Abi Ishaq Al-Shiraziy walichagua rai hiyo. na kwamba Sheikh Abi Ishaq Al-Shiraziy hakutaja kwamba kuna mwanavyuoni hata mmoja aliyekataa rai hiyo, Ibn Twahir Al-Maqdisi alichagua rai hiyo pia, na Ibrahim Bin Saad: vili vile ni mmoja wa wanavyuoni wa Madinah amesema kwamba inaruhusiwa kupiga udi, na hasemi chochote ila akipiga udi, na alipofika Baghdad na kukutana na Khalifa, akamwambia: Tuambie, nipe udi Ewe Amiri wa Waumini, alisema: Je! Unataka udi wa uvumba au udi ya uimbaji? Akasema: Hapana, nataka udi wa uimbaji, kwa hivyo akamletea kwake, naye akaupiga na kuimba, kisha akamwambia. Na Ibrahim Bin Saad, mmoja wa Masheikh wa Al-Shafiy R.A. na Al-Bukhari, ambaye ni mtu maarufu wa Imamu mwenye kujitahidi, wakati ulipopigwa udi mbele ya Harun Al-Rashid, akamwambia, Ewe Ibrahim, nani aliyesema kuwa hii ni marufuku miongoni mwa wanavyuoni wako? Akasema: Aliyefungwa na Mwenyezi Mungu, Ewe Amiri wa Waumini. Na ametaja Imam Ibn Arafah - katika ufupisho wake wa Fiqhi kutoka kwa Ibrahim Bin Saad – kuruhusiwa kwa uimbaji kwa udi, na Imam Al-Mazari kutoka kwa wenzetu wa Madhehebu ya Maliki kutoka kwa Abdullah Bin Abd Al-Hakam kwamba inaruhusiwa kupiga udi, na imepokelewa kutoka kwa Imam Izz Ad-Din Bin Abdul Al-Salam kuwa inaruhusiwa pia [61:66 / Farahul Asmaa / Ad-Dar Al-Arabia lelkitab].
Ibn Kinana alisema katika Sharhu Al-Khurashiy juu ya Khalil: Inaruhusiwa kupiga mzumari ambao hausaidii pumbao [3/304 / Sharhu Mukhtasar Khalil lil-Kharashi / Dar Al-Fikr].
Imepokelewa kutoka kwa Imam Al-Shawkani kutoka kwa mwanachuoni Al-Fakhani kuwa: Sikujua katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu wala katika Sunna Hadithi moja ambayo ni sahihi juu ya marufuku ya vyombo vya muziki, lakini ni baadhi ya mambo ambayo yametolewa tu, pasipo na dalili dhahiri [117/8 / Nail Al-Awtar Al-Shukani / Dar Al-Hadith].
Na haisemekani kuwa vyombo vya muziki ni haramu kwa mujibu wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: {Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu. Na shirikiana nao katika mali na wana, na waahidi. Na Shet'ani hawapi ahadi ila ya udanganyifu} [AL ISRAA: 64], sauti yake shetani ni kinachoulingania uasi kwa Mwenyezi Mungu, ikiwa vyombo vya muziki ni njia iliyokatazwa basi ni marufuku, vile vile Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: {Na miongoni mwa watu wapo wanao nunua maneno ya upuuzi, ili wawapoteze watu na njia ya Mwenyezi Mungu pasipo kujua, na wanaichukulia ni maskhara. Hao watapata adhabu ya kuwafedhehesha} [LUQMAAN: 6]. Kuharimisha kwa maneno ya upuuzi ni hukumu ya jumla inayojumuisha kila haramu isiyo na maana iliyokusudiwa kupotosha kutoka kwenye njia ya Mwenyezi Mungu, na hii haitegemei uharimisho tu lakini badala yake hupitisha mmiliki wake kwa kufuru, lakini ikiwa maneno hayo ya upuuzi yakichukuliwa kwa nia njema na njia ya jambo jema, basi hakuna kitu kibaya.
Haisemwi kuwa vyombo vya muziki vimepigwa marufuku kwa mujibu wa matini ya Hadithi ya Mtume S.A.W., ambayo imepokewa kutoka kwa Al-Bukhariy kutoka kwa Abu Malik Al-Ashariy kuwa: Alimsikia Mtume, S.A.W., akisema: “Watakuwa kutokana na Umma wangu watu wanaohalalisha uzinifu, nguo za hariri, (kwa mwanaume) pombe na vyombo vya muziki.” Vyombo vya muziki katika Hadithi hii ni haramu kama vikiambatana na makatazo yaliyotangulia, lakini Hadithi nyingine zote ambazo zimetaja kukatazwa kwa vyombo vya muziki, labda ni sahihi lakini sio za moja kwa moja au, sio wazi, au sio sahihi.
Haifahamiki kuwa ni marufuku kwa maneno ya baadhi ya Maimamu, kwa sababu Imamu Abu Hanifa haikuthibitishwa kutoka kwake matini moja kuhusu marufuku ya vyombo vya muziki, na kwamba Al-Qaffaal alisema kwamba Imamu Malik aliruhusu uimbaji na vyombo vya muziki,. Na rai hiyo imepokelewa kutoka kwa Al-Shawkani [8/114 / Nail Al-Awtar / Dar Al-Hadith] Na kwa maneno yake: ni kwamba anayefanya hivyo kwetu ni mafasiki, kauli yake hii inawezekana kwamba wale tunaowafahamu au kuwajua wanasikiliza uimbaji wanasifika kwetu kuwa mafasiki, kauli hii haioneshi kuharamishwa kwa uimbaji.
Kuruhusu uimbaji kunategemea sharti la kutoambatana kwa muziki na makatazo kama vile baraza la mvinyo au wanawake walio uchi. Ikiwa unaambatana na makatazo basi na wenyewe utakuwa umekatazwa pia, na haipaswi kufanya ubadhirifu katika jambo hilo, kwani jambo lolote huwa linaloruhusiwa au huwa linakatazwa kama likipita kiasi. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: {Na kuleni, na kunyweni na wala msifanye ubadhirifu}. [AL AARAF: 31]. Inapaswa kusikiliza uimbaji au matumizi ya vyombo vya muziki sio kupotosha kutoka katika majukumu kama vile Swala na mengine. Ukipotoshwa na majukumu, basi usikilizaji huo utakuwa marufuku kama vitu vingine vikiwa vimepotosha majukumu, basi ni marufuku pia.
Sheikh Jad Al-Haqq alisema katika Fatwa juu ya hukumu ya kusikiliza muziki: tunaona kwamba inaruhisiwa kusikiliza muziki, kuhudhuria mikusanyiko yake, na kujifunza chochote kutokana na vyombo vyake miongoni mwa vyombo vinavyoruhusiwa, isipokuwa kama vyombo hivi vinachochea matamanio, au vinaita kufanya jambo la haramu, au kuambatana na kunywa pombe, densi, uzinzi na unyanyasaji, au kuchukuliwa njia ya kufanya haramu, kuzuia kufanya majukumu, kwa sababu kile kinachoruhusiwa kinaruhusiwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake na kile kinachokatazwa kinakatazwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake [Fatwa Na. 1820 / Mausuatul Fatawa, Dar Al-Iftaa Al-Misriyah].
Kutokana na maelezo yaliyotajwa hapo juu: inaruhusiwa kusikiliza au kutumia vyombo vya muziki, kama haviambatani na mambo yaliyoharamishwa, au yanayozuia kufanya majukumu ambayo ni wajibu.
Na Mungu Mwenyezi Mtukufu ni Mjuzi Zaidi.
Sekretarieti ya Fatwa

 

Share this:

Related Fatwas