Haki za Binadamu Zinazofungamana na...

Egypt's Dar Al-Ifta

Haki za Binadamu Zinazofungamana na Makusudio ya Nafsi.

Question

 Je, Haki nini za binadamu katika Uislamu zinazoendana na makusudio ya nafsi kuhusu makazi na uhuru wa kusafiri na kuishi, kupata kinachomtosha mtu kulinda uhai wake na kuchunga afya yake?

Answer

 Kwa jina la Mwenyezi Mungu, sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, na rehma na amani zimwendee bwana wetu Mtume wa Mwenyezi Mungu, jamaa zake, masahaba wake na wafuasi, na baada ya utangulizo huo:
7- Haki ya Makazi na Uhuru wa Kusafiri na Kuishi popote atakako( ).
Katika haki za binadamu ambazo Uislamu umezipitisha ni haki ya makazi( ), na ambayo Uislamu umeizingatia ni katika mambo ya dharura kwa mwanadamu, pia Uislamu unaiwajibisha dola kuimarisha makazi kwa wananchi wote, kwa wale wenye uwezo miongoni mwao wanaweza kuwa na makazi yao binafsi, na asiye na uwezo serikali inapaswa kumjengea makazi.
Anataja Imamu Ibn Hazmi( ) kuwa matajiri wa kila nchi wanalazimika kusimamia mahitaji ya watu masikini na serikali inawalazimisha katika hilo ikiwa hazina kuu ya nchi haiwezi kufanya hivyo, watu watapatiwa vyakula vya kutosha ambavyo ni lazima kuvipata, na mavazi majira ya baridi au ya joto na mfano wa hivyo, na makazi yatakayo walinda kutokana na hali za mvua, mazingira ya kiangazi, pia na macho ya wapita njia.
Kwa sababu hiyo anasisitiza Ibn Hazmi jukumu la serikali na jamii kwa ujumla kusimamia haki za makazi kwa wahitaji.
Kama ilivyokuja kwenye Fiqh ya Kiislamu( ) kuwa ikiwa kuna mtu ambaye hana makazi wakati ambapo baadhi ya watu wengine wanamiliki makazi zaidi ya mahitaji yao, basi ni jukumu la kiongozi wa nchi kuwatafutia makazi hawa wengine kwa nguvu kwa wale wamiliki.
Ibn Hazmi ameweka sharti katika makazi hayo ikiwa ni pamoja yanayoweza kumlinda mkazi wake na hali ya mvua kipindi cha masika na hali ya joto kipindi cha kiangazi pamoja na macho ya wapita njia, katika kufanya hivyo kunapatikana ulinzi wa heshima ya mtu ndani ya nyumba yake - nayo ni sehemu ya siri zake - hivyo haifai kwa wapita njia kuziona aibu zake kwa macho yao.
1- Miongoni mwa athari za haki ya makazi: Ni kuwa kwenye makazi kuna uharamu, pindi mtu anapopata makazi hivyo haifai kwa mwanadamu yeyote yule kumvamia mwenye makazi haya na kuingia ndani isipokuwa kwa ruhusa yake hata kama atakuwa ni kiongozi mwenyewe, hana haki hiyo bila ya ruhusa, katika hilo Mwenyezi Mungu Anasema: {Enyi mlio amini! Msiingie nyumba zisio nyumba zenu mpaka muombe ruhusa, na muwatolee salamu wenyewe. Hayo ni bora kwenu mpate kukumbuka * Na msipo mkuta mtu humo basi msiingie mpaka mruhusiwe. Na mkiambiwa: Rudini! Basi rudini. Hivi ni usafi zaidi kwenu. Na Mwenyezi Mungu anajua munayoyatenda}( ). Katika Maandiko hayo kuna amri ya wazi ya kutoingia nyumba ya mtu yeyote isipokuwa kwa kupewa ruhusa.
Amri hii ni lazima kwa kila mgeni, awe ni kiongozi au mtu wa kawaida na Uislamu haukuishia hapa tu, bali umeisimamia heshima ya makazi binafsi hata kwa upande wa watoto wadogo wafanya kazi wa ndani pamoja na kuwa wao ni miongoni mwa wakazi wa humo, hilo ni katika mfumo mwema wa adabu, Anasema Mola: {Enyi mlioamini! Nawakutakeni idhini iliyowamiliki mikono yenu ya kulia na walio bado kubaleghe miongoni mwenu mara tatu - kabla ya Sala ya alfajiri, na wakati mnapovua nguo zenu adhuhuri, na baada ya Sala ya isha. Hizi ni nyakati tatu za faragha kwenu. Si vibaya kwenu wala kwao baada ya nyakati hizi, kuzungukiana nyinyi kwa nyinyi. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyo kuelezeni Aya zake, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima}( ).
Mwenyezi Mungu Amechunga kuwa kuna wakati ambao watu hupumzika hivyo hupunguza nguo zao, na wala hawapendi kuonekanwa na yeyote wakiwa katika hali hii hata kama watakuwa watoto wao au wafanya kazi wao wa ndani, bali Mwenyezi Mungu Akawajibisha kuomba ruhusa ndani ya nyakati hizi ili kulinda heshima na kulinda maisha.
Katika heshima ya makazi pia inakusanya kutoyahodhi hayo makazi au kuyavunja kwa nguvu kinyume na ridhaa ya mwenyewe.
Khalifa Umar Ibn Al-Khattab alitoa amri ya kujengwa tena sehemu ya nyumba ya Mmisri mmoja, wakati Amru Ibn Al-Aas alipokuwa anatawala Misri aliichukua hiyo nyumba na kuiingiza kwenye eneo la Msikiti, kama alivyofanya mfano wa hivyo Khalifa Umar Ibn Abdulaziz pindi alipotoa amri ya kujengwa upya nyumba hiyo na kurudishwa kwa mmiliki wake, na kiongozi wa eneo la Sham alikuwa ameichukua nyumba hiyo na kuiingiza kwenye eneo la Msikiti wa Umawiy( ).
2- Miongoni mwa athari za haki ya makazi: Kuzuia uchunguzi na upelelezi wa makazi ya mtu, kwani Uislamu umezuia vitendo vya kuyachunguza makazi ya mtu ili kufuatilia na kujua aibu zake, na Mwenyezi Mungu Anasema: {Wala msipelelezane, wala msisengenyane nyinyi kwa nyinyi}( ).
Itambulike kuwa Sharia ya Kiislamu inauheshimu mno uhuru wa mtu, na Uislamu una shime kubwa ya kuulinda na kuusimamia uhuru huo. Katika Vitabu viwili vya Sahihi, kuna Hadithi inayotoka kwa Abuu Huraira( ) kutoka kwa Mtume S.A.W. amesema: “Mwenye kuangalia nyumbani mwa watu pasi ya ruhusa yao basi wakimng’oa jicho lake mtu huyo hakuna kulipwa fidia”.
Katika kiwango hiki Uislamu unaitukuza heshima ya makazi mpaka wenyewe ukaondosha kisasi na fidia kwa mwenye kuyashambulia makazi ya watu.
Miongoni mwa haki ya kila binadamu, ni mtu kutoka sehemu anayoishi na kurudi tena, na vilevile ana haki ya kusafiri na kuhama kutoka nchini mwake na kisha kurudi nchini humo, pasina kuzuiliwa wala kukwamishwa: {Yeye ndiye aliye idhalilisha ardhi kwa faida yenu, basi tembeeni katika pande zake, na kuleni katika riziki zake. Na kwake Yeye ndio kufufuliwa}( ).
{Kwani ardhi ya Mwenyezi Mungu haikuwa na nafasi mkahamia humo?} [AN NISAA: 97].
Uislamu umehimiza kuhangaika kwenye ardhi na kuijenga pia, nao Uislamu katika hilo unasimamia uhuru wa kusafiri na kuishi.
Wakati huo huo haifai kumlazimisha mtu kuacha nchi yake, na kuwa mbali nayo pasina sababu ya Kisharia: {Wanakuuliza juu ya kupigana vita katika mwezi mtakatifu. Sema: Kupigana vita wakati huo ni dhambi kubwa. Lakini kuzuilia watu wasiende katika Njia ya Mwenyezi Mungu na kumkanusha Yeye, na kuzuilia watu wasiende kwenye Msikiti Mtakatifu na kuwatoa watu wake humo, ni makubwa zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu}.( )
Kutokana na hilo ilikuwa bora kwa wahamiaji miongoni mwa Masahaba kwa kuutanguliza Uislamu wao, na kulazimika kwao kuacha nchi yao, na Mwenyezi Mungu Amewafadhilisha na Akasema: {Basi waliohama, na walio tolewa makwao, na wakateswa katika Njia yangu, na wakapigana, na wakauliwa}( ).
Na Akasema tena: {Wapewe mafakiri Wahamiaji waliotolewa majumbani mwao na mali zao}( ). Kimebainika kwa maelezo hayo kiwango cha uhalifu kwa kumtoa mtu nchini mwake na kumpotezea mali zake.
Na Akasema tena Mwenyezi Mungu: {Wale ambao wametolewa majumbani mwao pasipo haki, ila kwa kuwa wanasema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu!}( ). Ni wazi kuwa haifai kumtoa mtu nchini kwake kinyume na njia za haki.
Uislamu umesimamia uhuru wa mtu wa kusafiri kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kama anavyotaka, kama vile umezuia msongamano barabarani ili kulinda uhuru huu na wala kusipelekee hilo kukwamisha harakati za watu katika kutoka kwao na kurudi kwao.
Vilevile, Uislamu umeruhusu kwa watu kwenda nje ya nchi zao na kurejea nchini kwao pasina vikwazo vyovyote.
Kwa kusisitiza matumizi mazuri ya barabara katika kutoka na kurudi anasema Mtume S.A.W.: “Jihadharini na kukaa barabarani. Masahaba wakauliza ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu hayo maeneo ni vikazi vyetu ni lazima tukae, akasema Mtume S.A.W.: Ikiwa hivyo basi ipeni barabara haki yake, wakauliza Masahaba: Ni ipi haki yake? Akasema Mtume S.A.W. kushusha macho chini, kuondoa kero, kujibu salamu, kuamrisha mema na kukataza maovu”( ).
Katika hilo Mtume S.A.W. amefanyia kazi suala la kutoleta misongamano barabarani kwa watu kukaa ambapo hizo barabara zimeandaliwa kwa waendao na wanaorudi, pindi Masahaba walipoelezea kuwa wao wamezoea vikazi hivi, basi Mtume akawaruhusu kwa sharti la kuepukana kuwakera na kuwafanyia maudhi watu yawe ya wazi au si ya wazi.
Kwani Mtume alikuwa akifanya kazi ya kusimamia haki ya wapita njia akawa haruhusu kwa yeyote kutoka nyumbani kwake au dukani kwake na kwenda barabarani, vilevile ikawa haifai kuleta aina mbalimbali za kero au madhara kwa wapita njia kama vile wakati wa baridi kukojolea kuta mbalimbali na mapito ya wazi ya majitaka kutoka juu kumwagikia katikati ya barabara wakati wa kiangazi, bali anaamrisha watu kuchimba maeneo ya kupitisha maji yatokayo juu, na kila ambaye nyumba yake ina matoleo ya majitaka kuelekea barabarani anamlazimisha kuziba matoleo hayo kipindi cha kiangazi na kuchimba shimo kwenye nyumba yake litakalokusanya majitaka ( ).
Uhuru wa kusafiri huenda ukawa na baadhi ya vikwazo ikiwa hilo linapelekea uwepo wa masilahi ya umma, na hilo ikiwa ni pamoja na sababu za kiafya au usalama au misingi ya adabu za umma.
Amesema Mtume S.A.W.: “Pindi unapoingia ugonjwa nchini na nyinyi mkiwa ndani ya nchi basi msitoke, na mkiusikia huo ugonjwa hali ya kuwa nyinyi mpo nje ya nchi basi msiingie”( ). Kuweka vikwazo kwenye uhuru wa kusafiri kwa maslahi ya umma lengo ni kuzuia kutoeneza ugonjwa.
Imekuja kwenye kitabu cha Samy Al-Hajwy kuwa Omar Ibn Al-Khatwab alizuia Masahaba wakubwa kutoka nadani ya Madinah isipokuwa kwa ruhusa, kwani imepokelewa na Tabary kutoka kwa Shaaby( ) kuwa miongoni mwa yaliyopelekea dini kuwa na ulinzi na Fiqhi kuwa wazi zaidi ni zama za utawala wa Umar ambapo ilikuwa kuzuia Masahaba wahamiaji na Masahaba wengine wakubwa kutoka na kusambaa kwenye miji mbalimbali ambayo ilifunguliwa, alikuwa hawaruhusu kuondoka Madinah isipokuwa kwa ruhusa yake ya muda mfupi kwa jambo la dharura sana, walikuwa washauri wake na kwa sababu hiyo tofauti zilipungua sana na kurahisisha kukutana katika masuala mengi.
Ikawa kikwazo hiki ni miongoni mwa kinachopelekea kwenye masilahi ya umma ikiwa ni pamoja na kukutana Wanachuoni wakubwa na Masahaba kwenye mji mkuu wa utawala na kurahisisha hatua ya kubadilishana mitazamo na kurahisisha mashauriano, na hii dharura iliyopelekea uwepo wa kikwazo hiko.
Baada ya kupanuka kwa dola ya Kiislamu katika zama za utawala wa Uthman R.A. ndipo ilitoka ruhusa ya kusafiri na kusambaa duniani mpaka elimu isambae kwenye miji mbalimbali na kurudi uhuru wa kusafiri kwenye hali yake ya kwanza.
Inafahamika hapa kuwa kikwazo hiki kilikuwa ndani ya kipindi kifupi na kwa watu maalumu wala hakikufanyiwa kazi kwa watu wengine walio baki, na wala hakikutekelezwa ndani ya nyakati zote, dharura - kama wanavyosema watu wa kanuni - hukadiriwa kwa kiwango chake, pindi inapoisha dharura, basi ni lazima kurudi hali ya asili.
Kama vile Uislamu umepitisha utekelezwaji wa adhabu kwa wale wanaopigana vita na Mwenyezi Mungu pamoja na Mtume wake na kufanya uharibifu ardhini na kuendesha vitendo vya wizi na uporaji kwa watu wa amani, anasema Mola Mtukufu: {Basi malipo ya wale wanao mpiga vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wakawania kufanya uchafuzi katika nchi, ni kuuwawa, au kusulubiwa, au kukatwa mikono yao na miguu yao kwa mabadilisho, au kutolewa nchini. Hii ndiyo kufedheheshwa kwao duniani na Akhera watapata adhabu kubwa}( ).
Miongoni mwa vikwazo vya uhuru wa kuishi ni pamoja na yaliyokuja kwenye tahadhari ya kuingia makafiri mji wa Makka na kutoishi kwenye Kisiwa cha Waarabu, Anasema Mola: {Enyi mlioamini! Hakika washirikina ni najisi, kwa hivyo wasiukaribie Msikiti Mtakatifu baada ya mwaka wao huu}( ). Imeteremka Surat At-Tawba baada ya Mtume S.A.W. kurudi kutoka kwenye vita vya Tabuok ambapo Roma ilikuwa imeandaa majeshi yao kwa ajili ya vita hivi na kuwaweka pembezoni mwa Kisiwa cha Kiarabu ambacho kulikuwa uwepo wa washirikina ndani ya eneo hilo ni tishio siku zote dhidi ya Imani ya Kiislamu, na Aya zimebainisha sababu za hatua hii dhidi ya washirikina kutokana na kero walizozifanya dhidi ya Waislamu, na kutokana na kubeba chuki pamoja na shari lakini pia kuvunja ahadi yao na kiapo chao na Mtume S.A.W.( ), anasema Mola: {Je, hamtapigana na watu walio vunja viapo vyao na wakawa na hamu ya kumfukuza Mtume, nao ndio waliokuanzeni mara ya kwanza?}( ).
Lengo la kuondolewa kwao kwenye Kisiwa cha Kiarabu ni kulinda kambi ya Kiislamu kwa wale wenye kufanya vitimbi pamoja na kufanya usaliti wa ahadi mpaka iwezekane kupambana na maadui wa Uislamu nje ya Kisiwa hali ya kuwa Mtume akiwa ni mwenye utulivu mpaka mwisho wa vita, katika kutekeleza hilo amesema Mtume S.A.W. katika Hadithi iliyopokelewa na Bibi Aisha R.A.: “Zisiachwe kwenye Kisiwa cha Kiarabu dini mbili”( ).
Kama vile Umar aliwatoa wasiokuwa Waislamu kutoka Madina na baadhi yao alikutana nao huko Sham na baadhi yao alikutana nao huko Kufah, pia Abubakari aliwahamisha watu na kukutana nao huko Khaibar( ).
Baadhi ya Wanachuoni wanaona kuwa kutokubalika washirikina kubakia Bara Arabu kinachokusudiwa kuwepo kwao kama kundi kwa sababu kukusanyika kwao ndiyo sababu ya kutolewa kwao. Ama uwepo wao kama mtu mmoja mmoja hakuna zuio lolote, anaona Imamu Abu Hanifa( ) kuwa maamuzi yao kubakia Madina ni kufaa moja kwa moja isipokuwa kuwepo Msikitini, na kwa upande wa Imamu Malik anaona kuwa inafaa kuingia Makka kwa shughuri za kibiashara au wasafiri( ).
Amesema Imamu Shafiy: Hawaruhusiwi kuingia eneo la Msikiti wa Makkah isipokuwa kwa ruhusa ya Imamu kwa ajili ya masilahi ya Waislamu( ), na kuangalia yale yanayorudi kwao miongoni mwa manufaa( ), vilevile inafaa kuingia ili kutekeleza ujumbe au kutaka usuluhishi au hali ya utulivu au kufanya malipo au mfano wa hayo miongoni mwa sababu ambazo kiongozi atawapa usalama madamu tu watakuwa wakienda mara kwa mara kwenye dola ya Kiislamu mpaka warudi nchini kwao( ), vilevile wakitakiwa kusikiliza Maneno ya Mwenyezi Mungu, Anasema Mola: {Na ikiwa mmoja wapo katika washirikina akikuomba ulinzi, basi mpe ulinzi apate kusikia maneno ya Mwenyezi Mungu. Kisha mfikishe pahala pake pa amani. Haya ni kwa kuwa hao ni watu wasiojua kitu}( ).
Na kama hivyo mfumo wa Uislamu unatambua mfumo wa uhuru wa mtu kwa maana za wazi madamu tu katika mipaka ya haki uadilifu na kheri, pindi uhuru unapogongana na haki au uadilifu au kheri, basi husimama kuangaliwa kwake.
8- Haki ya Binadamu Kupata Kinachotosha Kulinda Uhai wake( ).
Ni haki ya kila binadamu kupata kinachomtosha katika viimarishaji vya uhai na vya umuhimu wake, ikiwa ni pamoja na chakula mavazi na makazi, na yanayolazimu kwa ajili ya afya ya mwili wake ikiwa usimamizi na yanayolazimu afya ya roho yake na akili yake ikiwa ni pamoja na elimu maarifa na tamaduni katika wigo unaoruhusu mali ya serikali, na inaongezewa katika hilo kuwa kila anachoweza mtu kujitosheleza yeye mwenyewe basi umma ni juu yake kumtoshelezea.
Sharia ya Kiislamu imepitisha kuwa kuna vitu vya dharura ni lazima kuvilinda, na imeharamisha kabisa kufanya uadui kwenye hivyo, navyo hufahamika kama mambo matano ya dharura, nayo ni kulinda dini, kulinda nafsi, kulinda akili, kulinda kizazi, na kulinda mali.
Umuhimu wa kulinda nafsi na akili ni jambo lilinalotakiwa kufikiwa na kila binadamu aweze kupata kile kinachotosha kulinda uhai wake.
Dola ya Kiislamu husimamia wajibu kwa sura nzuri ili kulinda haki za watu na kusimamia maisha yao, kwani Uislamu umemzingatia mtu kwenye kusimamia jamii kwa ngazi zote.
Ikiwa ni pamoja na kusimamia familia yake ambapo Sharia imemuamrisha kumgharamia ndugu wa karibu ambaye masikini kama vile inavyoamrisha katika kuunga undugu.
Katika kusimamia jamii ndani ya kijiji pindi inapokuwa na mahitaji sana au kupatwa na mitihani na changamoto za umasikini, anasema Mtume S.A.W. “Watu wowote wa eneo husika mtu mmoja miongoni mwao amelala na njaa, basi watakuwa wamejitoa kwenye jukumu waliloamrishwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake”( ). Na anasema tena Mtume S.A.W.: “Bado hana Imani mtu ambaye amelala hali ameshiba na jirani yake akiwa na njaa”( ).
Uislamu umeinua haki ya usimamizi wa kijamii kwa watu kwa kuifanya kuwa ni sababu ya ukaribu kwa Mwenyezi Mungu.
Kwani Uislamu umeusia jirani kukirimiwa na kufanyiwa mashirikiano mema kwa kiwango kikubwa mno, Anasema Mola: {Mwabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na chochote. Na wafanyieni wema wazazi wawili na jamaa na mayatima na masikini na jirani wa karibu na jirani wa mbali, na rafiki wa ubavuni na mpita njia, na waliomilikiwa na mikono yenu ya kulia. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wenye kiburi wanaojifaharisha}( ).
Hivyo Uislamu umefanya kwa mtu kuwa na haki katika kusimamia maisha yake kwa upande wa familia yake na upande wa jamii yake ndogo miongoni mwa jirani zake na watu wa kijijini kwake, kisha haki yake kwa upande wa serikali, na usimamizi huu huwajibika serikali ni sawa sawa huyo mtu akiwa ni Mwislamu au si Mwislamu, imepokelewa na Abu Yussuf ( ) kuwa “Umari Ibn Al-Khattab siku moja alimwona mtu mzima wa Kiyahudi akiwa anawaombaomba watu, Umar akamwuliza sababu ya kufanya hivyo yule mzee akajibu: Ninaomba kwa ajili ya Jiziya /malipo mahitaji na umri, akasema: Hatujakufanyia haki, tumekula ujana wako na tukakuacha wakati wa uzee wako, akampa malipo yake na kuamrisha kupewa mali kwenye hazina ya fedha za Waislamu kwake yeye mzee na kwa watoto wake”. Haki ya mtu kutoka upande wa serikali ni kumtoshelezea kupitia vyanzo vyote vya mali ya serikali.
Hivyo tunakuta jamii ya Kiislamu yote inajukumu la kusimamia wenye mahitaji na jukumu hili limepitishwa na Qur`ani pamoja na Sunna, Anasema Mola: {Na saidianeni katika wema na ucha-Mungu}( ), na akasema: {Na ambao katika mali zao ziko haki maalumu * Kwa mwenye kuomba na anaye jizuilia na kuomba}( ).
Na kwa kupitisha Uislamu usimamizi wa haki ya kuishi maisha mazuri kwa watu unasimamia mifumo mitatu nayo ni: Zaka Sadaka na Waqfu.
- Haki ya Uduma ya Afya( ):
Uislamu umetoa umuhimu mkubwa suala la afya ya mtu kwa kuizingatia humsaidia mtu kutekeleza wajibu wake wa kidini na kimaisha ambapo kwa hiyo afya anaweza mtu kunufaika na kufikia matarajio yake, anasema Mtume S.A.W.: “Muumini mwenye nguvu ni bora na anapendwa zaidi na Mwenyezi Mungu kuliko Muumini dhaifu katika kila jambo la kheri” ( ).
Kwa kutambua haki ya mtu katika huduma ya afya Uislamu umeweka hilo kuwa ni jukumu la mtu kwa kuzingatia kuwa ni wajibu wake, kama vile umezingatia kuwa wajibu wa serikali kwani ni haki ya mtu.
1- Katika kuzingatia huduma ya afya ni wajibu wa mtu. Uislamu umeamrisha watu wote kujiweka mbali na kila chenye kuleta madhara ya afya yao, kwani umeharamisha pombe na uzinifu ikiwa lengo ni kulinda afya na kuwaamrisha kuwa mbali na yale yanayopelekea kuumiza afya zao na kumaliza nguvu zao, Anasema Mola: {wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamizi}( ).
Na anasema Mtume S.A.W.: “Hakuna kudhuru wala kujidhuru”( ).
Kama vile Uislamu umehimiza watu kufanya usafi ili kulinda afya, ukaamrisha watu kutawadha kabla ya kusali na kuoga baada ya mtu kupatwa na janaba, na kuchunga sana lishe na kinywaji safi, na umekataza kunywea kwenye mdomo wa chupa lengo ni kuzuia magonjwa ya kuambukiza, kama ulivyopendezesha kufanya mazoezi ili kuimarisha mwili, na katika hilo anasema Mtume S.A.W.: “Hakika mwili wako una haki juu yako”.
Kama vile Uislamu umeamrisha watu kufanya haraka kupata matibabu wakati wa kuumwa, miongoni mwa kauli zake Mtume S.A.W.: “Mwenyezi Mungu hakuteremsha ugonjwa isipokuwa ameuteremshia tiba yake”( ).
Misingi yote hii imekuja katika sura ya amri hivyo hupata thawabu mtekelezaji wake na kupata dhambi mwenye kwenda kinyume nayo, kama vile Uislamu umetoa umuhimu mkubwa huduma za afya bali umefanya ni katika vipaombele vya mambo ya ibada, kwa sababu hiyo amesamehewa mgonjwa kutekeleza mambo ya lazima ya kidini ambayo yanawawia uzito kwao. Uislamu ukampa ruhusa mgonjwa kula chakula wakati wa mchana wa Ramadhani kwa kuhofia kuongezeka au kuzidi ugonjwa wake au kuchelewa kupona badala yake atalipia funga hiyo baada ya kupona kwake, na ukahalalisha kwa yule inayompa taabu ibada ya funga kwa kumruhusu kula mchana na kulipa fidia ya kulisha chakula masikini.
Kama vile umempa ruhusa msafiri kula mchana wa Ramadhani ili kumwondolea matatizo ambayo yataweza kuathiri afya yake. Anasema Mola: {Basi atayekuwa mjini katika mwezi huu na afunge. Na mwenye kuwa mgonjwa au safarini, basi atimize hesabu katika siku nyingine}( ).
Na anasema tena Mwenyezi Mungu: {Na wale wasioweza, watoe fidiya kwa kumlisha masikini}( ). {Mwenyezi Mungu anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito}( ).
2- Ama huduma ya afya kwa kuizingatia ni haki ya watu kwa serikali hivyo Uislamu umepitisha haki hiyo kwa sura tofauti, ambapo Mtume S.A.W. alikuwa wagonjwa akiwaandalia sehemu ya kupatia matibabu, kwani siku moja alifikiwa na watu kutoka Arinah - walikuwa wanane - na walisilimu na walifika Madina wakawa wanalalamika maumivu katika bandama, na Mtume S.A.W. akaamrisha kupatiwa chanjo, na walikuwa karibu na maeneo ya Qubaa na walikaa huko mpaka wakapona na walitaka ruhusa ya kunywa maziwa na Mtume akawaruhusu.
Hivyo ndivyo tunakuta dola ya Kiislamu imezisimamia huduma za afya kwa wananchi wake( ).
Marejeo: Kitengo cha tafiti za Kisharia Ofisi kuu ya Mufti wa Misri.

 

Share this:

Related Fatwas