Maswali Mbalmbali katika Jarida ya ...

Egypt's Dar Al-Ifta

Maswali Mbalmbali katika Jarida ya Dauwa

Question

 Ni ipi hukumu ya wanawake wanaofanya kazi katika uwanja wa mashauriano ya jamii? Ni ipi hukumu ya kazi yake katika uwanja wa masuala ya umma ya serikali, pamoja na uwanja wa kisiasa? Ni ipi hukumu ya wanawake wanaofanya kazi kama mjumbe wa mabaraza la Ushauri au Bunge? Je! Mnasemaje kuhusu wale wanaopinga kuingia kwa wanawake katika mabaraza ya Ushauri au Mabunge na kujaribu kuwatenga na jukumu lao la kweli katika kujenga jamii?

Answer

 Sifa zote njema ni za Allah pekee, na swala na salaam ziwe juu ya Bwana wetu Muhammad Mtume wa Mwenyezi Mungu, na pia juu ya jamaa zake na maswahaba zake, na juu ya wale wanaowafuata kwa wema mpaka Siku ya Malipo
Kazi ya mwanamke, kama ilivyo, haipingwi na sheria ya Kiislamu; asili yake inaruhusiwa maadamu kazi yenyewe ni halali, kulingana na maumbile ya mwanamke, haina athari mbaya kwa maisha ya familia yake. Hivyo ni pamoja na kuthibitisha kwa kufuata mwanamke yule dini na maadili, usalama wa nafsi yake, heshima yake na dini yake wakati anapoifanya kazi hiyo.
Kazi ni moja ya haki za watu binafsi, na kila mmoja ana haki ya kushiriki katika aina yoyote ya biashara halali kama anavyotaka. Kupata riziki yake na kuweza kuishi kwa heshima. Sheria ya Kiislamu haikutofautisha kati ya wanawake na wanaume katika haki hii; Mwenyezi Mungu amesema: “Si vibaya kwenu kuitafuta fadhila ya Mola wenu Mlezi” [Al-Baqarah: 198], na imepokelewa kutoka kwa Imamu Muslim kutoka kwa Jabir Ibn Abdullah, R.A., kwamba alisema: shangazi yangu ametalikiwa, kwa hivyo alitaka kukata tende zake. Mtu mmoja akamkaripia ili aende nje, kwa hivyo mwanamke huyo alikwenda kwa Mtume wa Allah, S.A.W, akamwambia: “Ndio, ukate tende zako, kwani labda utatoa sadaka au utafanya tendo jema.”
Kuhusu ushiriki wa wanawake katika maisha ya kijamii, hali hii ni aina ya marekebisho ambayo yanahitajika kwa sheria, na Mwenyezi Mungu anasema: “Na Waumini wanaume na Waumini wanawake wao kwa wao ni marafiki walinzi. Huamrisha mema na hukataza maovu” At-Tawba [71] Kwa hivyo, wanawake wanaweza kufanya kazi katika uwanja wa mashauriano ya jamii na kuchukua nafasi katika vituo, taasisi, jamii za misaada, na vyombo vingine vinavyohusika katika jambo hili. Wanawake katika enzi za Mtume, S.A.W., walikuwa wakitimiza majukumu mengi ya kijamii, kwa hivyo walikuwa wakitoka na wanaume katika vita, na kuwauguza, kuwanywesha, na kadhalika, na walikuwa wakihudhuria Swala na Sikukuu.
Kuhusiana na kazi ya wanawake katika uwanja wa kisiasa na masuala ya serikali, hali hii inaingia katika hukumu ambayo imetangulia hapo awali, na inathibitishwa na: Kile ambacho Uislamu unasisitizia kuhusu msingi wa ushauri bila ubaguzi kati ya jinsia na jambo lingine; Mwenyezi Mungu anasema: “na shauriana nao katika mambo.” [Al I’mran: 159], na imepokelewa kutoka kwa Al-Bukhari kwamba Mtume, S.A.W., alimuuliza mkewe Ummu Salamah, R.A., kuhusu Mkataba wa Al-Hudaybiyah baada ya kuandika mkataba wa amani na washirikina, na baada ya kuwaamuru Waislamu watoe kafara zao na kunyoa nywele zao; Hawaendi Makka mwaka huu, na hakuna hata mmoja wao aliyeinuka. Omar Ibn Al-Khattab, R.A, anasema: Alipomaliza suala la kitabu, Mtume wa Allah, S.A.W., aliwaambia wenzie: “Simameni, chinjeni kisha nyoeni.” Alisema: Wallahi, hakuna hata mmoja wao aliyesimama mpaka aliposema hayo mara tatu. Wakati hakuna hata mmoja wao aliyesimama, aliingia kwa Ummu Salamah na kumweleza kile alichokutana na watu. Ummu Salamah akasema: Ewe Nabii wa Allah, je! Ungependa hivyo, nenda nje, halafu usiongee na yeyote kati yao mpaka unachinja ngamia na ng'ombe wako na umwite kinyozi wako ili akunyoe. Kwa hivyo alitoka nje na hakuongea na yeyote kati yao mpaka alipofanya hivyo, alichinja ngamia na ng'ombe wake na kumwita kinyozi wake, naye akamnyoa. Walipoona hivyo, walisimama na kuchinja, na wengine wao wakinyoana.
Miongoni mwa misimamo inayothibitisha haki ya wanawake ya kushiriki kisiasa ni msimamo wa Mama wa Waumini, Aisha, R.A, kuhusu mzozo kati ya Imamu Ali, Mwenyezi Mungu Amrehemu, na Sahaba mkubwa Muawiyah Ibn Abi Sufyan, R.A., Mama wa Waumini, Aisha R.A., alisema maoni yake kuhusu mzozo huu, na yeye mwenyewe alienda kuwapatanisha kwenye uwanja wa vita, lakini Mwenyezi Mungu aliajaalia mapigano hayo [Rejea: Morouj Adh-Dhahab na Masoudi 2/357, Dar Al-Hijrah, na Al-Kamel fi Al-Tarikh na Ibn Al-Atheer 3/119, Dar Al-Kutub Al-Ilmiyyah, na Tariikh At-Tabari 4/462, Dar Al-Maarif].
Ama kutawala kwa wanawake nafasi za kisiasa katika serikali au taasisi za serikali; Baadhi ya Hadithi zilipokelewa katika hali ya kufanya kazi ya wanawake katika nafasi ya mamlaka ya utendaji, au polisi, au kile kinachoitwa katika urithi wa fiqhi ya Kiislamu kama "Hesba", pamoja na: ile iliyopokelewa kutoka kwa Al-Tabaraniy katika kamusi yake kuu kutoka kwa Abi Balj Yahya Ibn Abi Salim, alisema: Nilimuona Samra binti Nahik, naye alikuwa amewahi kumuona Mtume wa Allah, S.A.W., Samra alikuwa amevaa ngao nene na kitambaa kizito, akiwa na mjeledi mkononi mwake. anawaadhibu watu, anaamrisha mema na anakataza mabaya. Kwa hivyo, baadhi ya wanavyuoni wa Kiislamu wameruhusu wanawake kushikilia cheo hicho nyeti.
Imetolewa Fatwa kutoka Dar Al-Iftaa la Misri Na. 701 mwaka wa 2008 kwamba mwanamke anaruhusiwa kufanya kazi kama wakala wa mashtaka ya kiutawala, sharti tu awe na uwezo wa kupatanisha kati ya majukumu yake ya kijamii na kifamilia, na kufuata kwake maadili na maadili ya kisheria katika sura na tabia, na kwamba tabia ya kazi hii labda wakati mwingine inahitaji kufunga mlango wa chumba pamoja na kuruhusiwa kuingia mtu yeyote wakati wowote, hali hiyo sio marufuku ikiwa tu hakuna shaka yeyote, na hali hii haizingatiwi kuwa ni kujitenga ambako kulikatazwa. Na kazi yake katika suala hili ni kutokana na suala la kuamrisha mema na kukataza yaliyo mabaya, kutafuta kuweka utulivu wa umma, na kuzuia ufisadi na wafisadi.
Inaruhusiwa pia kwa mwanamke kutawala mahakama pia, kulingana na mtazamo wa baadhi ya wanavyuoni. Hii ndiyo kauli ya Al-Tabari, ambapo aliruhusu utawala wake kwa mahakama bila kipingamizi. Kwa sababu inajuzu kwake kuwa Mufti, basi inajuzu kwake kuwa jaji, kwa hivyo uanaume sio sharti katika hilo, nayo imepokelewa kutoka kwa Imamu Malik, na hivyo ndivyo maoni ya Ibn Hazm kutoka kwa Zahiriyya. [Rejea: Al-Mughni na Ibn Qudamah 10/92, Dar Ihyaa At-Turaath Al-Arabi, Al-Qawanin Al-Fiqhiyah na Ibn Juzay 1/253, Dar Al-Fikr, Fath Al-Bari na Ibn Hajar 8/128, Dar Al-Maarifa, Al-Muhalla na Ibn Hazm 8/527, 528, Al-Muniriyah]
Katika madhehebu ya Imamu Abu Hanifa ni kwamba ikiwa mwanamke ameteuliwa kama jaji, inajuzu hukumu yake katika suala ambalo ushahidi wake unakubalika. Wakasema: Kwa sababu ujaji ni sehemu ya utawala, kama ushahidi, na mwanamke huyo ni mmoja wa watu walioweza kutoa ushahidi, kwa hivyo yeye ni mmoja wa watu wanaoweza kutawala [Rejea: Fath Al-Qadeer na Ibn Al-Hamam 6 391, Dar Ihyaa At-Turaath Al-Arabiy].
Na wanachuoni wa Fiqhi wa Imamu Shafi, ingawaje ni miongoni mwa wale wanaosema kuwa hairuhusiwi kwa mwanamke kutawala ujaji, lakini wameweka kanuni kwamba ikiwa mtawala atamteua kwa ujaji, basi ujaji wake utatekelezwa; kwa dharura tu [Rejea: Nihayat Al-Muhtaj na Al-Ramli 8/240, Mustafa Al-Halabi].
Vivyo hivyo, inajuzu kwake kushiriki katika uchaguzi wa uanachama katika Baraza la Ushauri na Bunge, maadamu anaweza kupatanisha kati ya kufanya kazi katika mabaraza haya na haki za mumewe, watoto, na wamiliki wa haki, ikiwa zipo, sharti tu hali hii iko katika mfumo wa hukumu za maadili ya Uislamu mbali na kujipamba na hali ya kujitenga isiyo ya kisheria. Kuchagua wanawake wengine katika hali hii ni suala la kutekeleza maslahi ya umma.
Imetolewa Fatwa kutoka Dar Al-Iftaa nchini Misri hapo awali Na. 852 mwaka wa 1997 kuhusu hukumu ya mwanamke kuwa mwanachama wa Baraza la Wawakilishi au Wananchi, Fatwa hii ilihitimishwa kuwa: kisheria hakuna pingamizi lolote kwa mwanamke kuwa mwanachama wa Baraza la Wawakilishi au watu, ikiwa watu wamekubali kuwa wanawake wanawawakilisha katika mabaraza hayo, ilimradi maelezo ya mabaraza haya yanalingana na maumbile ambayo Allah amewapambanua nayo, na kwamba wanawake ndani yao wamefungwa na mipaka na sheria ya Allah, kama alivyoeleza Allah na kuamuru katika Sheria ya Uislamu.
Ama kupinga kwa ushiriki wa wanawake katika kazi za kijamii na kisiasa, ikiwa nia ni kudhalilisha wanawake na kuweka kando mchango wao katika kujenga jamii, basi hii ni kinyume na kanuni ya usawa kati ya jinsia kwa haki na wajibu, na pia inapingana kanuni ya usawa kati ya jinsia katika uwezo wa halali; Na Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Nao wanawake wanayo haki kwa Sharia kama ile haki iliyo juu yao” [Al-Baqarah: 228].
Na ushiriki huu sasa umekuwa ukweli usiopingika; Wanawake hushiriki na wanaume katika nchi nyingi za Kiislamu na Kiarabu katika shughuli zote za serikali na katika maisha ya kisiasa na kisayansi; Wanawake wamekuwa Mabalozi, Mawaziri, Maprofesa wa Vyuo Vikuu na Majaji kwa miaka mingi, nao wanawake ni sawa na wanaume kwa malipo na vyeo vya kazi katika kazi hizi zote. Kinachotakiwa ni kuweka ushiriki huu – uwe na mipaka kwake mwenyewe- ndani ya mfumo wa maamuzi ya kisheria na maadili ambayo huhifadhi hadhi ya wanawake, kuhifadhi heshima yake, kujenga nyumba yake, na kumridhisha Mungu wake.
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu Ni Mjuzi Zaidi
Amana ya Fatwa

Share this:

Related Fatwas