Hukumu ya Uimamu wa Mwanamke

Egypt's Dar Al-Ifta

Hukumu ya Uimamu wa Mwanamke

Question

Je, mwanamke anaweza kuwa Imamu wa wanaume katika Swala ya faradhi? Na je, inajuzu kwa mwanamke kuwaswalisha wanawake wenzake katika Swala ya faradhi? Na ni wapi atasimama kama Imamu iwapo ataswalisha wanawake?

Answer

Uimamu wa Swala katika Uislamu una hadhi kubwa na nafasi ya juu; kwa kuwa kwa uimamu ndipo jamaa ya Waislamu inasimama. Kwa ukubwa wa hadhi ya uimamu, sharia tukufu imeweka masharti kwa ajili yake. Miongoni mwa masharti yaliyowekwa katika uimamu wa jamaa ya wanaume katika Swala za faradhi: ni kuwa mwanaume. Hivyo, haijuzu mwanamke kuwa Imamu wa wanaume katika Swala ya faradhi, tarawehe, au Sunna nyingine zote. Akiwaswalisha, Swala zao zinabatilika kwa makubaliano ya wanazuoni.

Lakini mwanamke anaweza kuwaswalisha wanawake wenzake katika Swala ya faradhi, na atasimama pamoja nao katikati ya safu. Iwapo atasimama mbele yao, Swala zao itakuwa sahihi lakini pamoja na kuchukiza.

Maelezo

Uimamu wa Swala katika Uislamu una hadhi kubwa na nafasi ya juu; kwa kuwa kwa uimamu ndipo jamaa ya Waislamu inasimama, hivyo Swala yao hupata fadhila na daraja zaidi kuliko wakiswali peke yao. Kutoka kwa Abdullahi bin Umar (R.A) amesema: Nilimsikia Mtume (S.A.W) akisema: “Swala ya jamaa ni bora kuliko Swala ya mtu mmoja kwa daraja ishirini na saba.” (Ameitoa Bukhari na Muslim).

Kwa ukubwa wa hadhi ya uimamu, Sharia imeweka sharti la kumtanguliza mbele alie bora zaidi miongoni mwa waliopo katika kusoma Kitabu cha Allah, elimu ya Sunna, uzee katika umri, na mengineyo. Hivyo, Mtume  (S.A.W)  alikuwa ndiye Imamu wa Waislamu katika Swala zao alipokuwepo, na wakafuata mfano huo bora wa umma wa Maswahaba, waliowafuata, na waliokuja baada yao katika karne bora, na hii ndiyo kazi ya Waislamu tangu zamani hadi leo.

Hili ndilo alilolibainisha Mtume  (S.A.W)  aliposema: “Atawaongoza watu katika Swala yule aliye bora zaidi kwa kusoma Kitabu cha Allah. Wakilingana katika usomaji, basi yule aliye na elimu zaidi ya Sunna. Wakilingana katika Sunna, basi yule aliye tangulia kuhama. Wakilingana katika kuhama, basi yule aliye tangulia  kusilimu. Na asimame mwanaume kumswalisha mwanaume katika mamlaka yake, wala asikae nyumba yake juu ya sehemu ya heshima yake ila kwa ruhusa yake.” (Ameitoa Muslim katika Sahih yake kutoka kwa Abu Mas‘ud al-Ansari).

Miongoni mwa masharti yaliyowekwa katika uimamu wa jamaa ya wanaume katika Swala za faradhi: ni kuwa mwanaume. Hivyo, haijuzu mwanamke kuwa Imamu wa wanaume katika Swala ya faradhi, tarawehe, na Sunna zote. Akiwaswalisha, Swala zao zinabatilika kwa makubaliano ya wanazuoni. Na hili ndilo lililotajwa na wafuasi wa Madhehebu yanayofuatwa.

Ama ikiwa wanaomswalisha ni wanawake, basi inajuzu uimamu wake kwao katika Swala ya faradhi, na atasimama pamoja nao katikati ya safu wakati anaswalisha. Akisimama mbele yao, inajuzu pia kwa kuchukiza; kwa sababu kusimama katikati ni stara zaidi kwake, na ni bora kuliko kusimama mbele.

Na jambo hili limeelezwa na Wanazuoni wengi wa Imamu Hanafi kuwa linajuzu kujuzu pamoja na kuchukiza, na baadhi ya Wanazuoni wa Imamu Maliki, na limewekewa sharti na Imamu Al-Lakhmi kuwa kama hapana mwanaume wa kuwaongoza, vinginevyo itakuwa ni Makruh. Pia wamesema hivyo Wanazuoni wa Shafi na Hanbali, na limeripotiwa kutoka kwa baadhi ya Maswahaba na waliowafuata miongoni mwa Maimamu wa ijtihadi. Imepokelewa kutoka kwa Mama wa Waumini Aisha, Mama wa Waumini Ummu Salama, Ibn Abbas, Ibn Umar (R.A) na kundi la waliotangulia.

Kutoka kwa ‘Ata kutoka kwa Mama wa Waumini Aisha (R.A): “Alikuwa akiwaswalisha wanawake, akiswali pamoja nao ndani ya safu.”

(Ameitoa Ibn Abi Shaybah katika al-Musannaf).

 

Na kutoka kwa Hujayra binti Husayn (R.A) amesema:
“Ummu Salama alituswalisha Swala ya Alasiri, akasimama katikati yetu.”

(Ameitoa Abdurrazzaq katika al-Musannaf).

Na kutoka kwa Ummu Waraqah (R.A) kwamba Mtume wa Allah (S.A.W) :“Alimruhusu kuadhini, kuqimu, na kuwaswalisha wanawake wake.” (Ameitoa al-Daraqutni katika Sunan).

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Uimamu wa Swala katika Uislamu una hadhi kubwa na nafasi ya juu; kwani kwa uimamu ndipo jamaa ya Waislamu inasimama, hivyo Swala yao hupata fadhila na daraja zaidi kuliko wakiswali peke yao.

Hukumu ya uimamu wa mwanamke katika Swala inatofautiana kulingana na anaomswalisha. Ikiwa ni wanaume, basi hakuna khilafu kuwa haijuzu kuwaswalisha, na wakiswali nyuma yake Swala zao huharibika, na inawabidi kurudia.

Ikiwa anaowaswalisha ni wanawake, basi inajuzu kuwaswalisha katika faradhi, na atasimama pamoja nao katikati ya safu wakati wa uimamu wake. Akisimama mbele yao inajuzu pamoja na  kuchukiza, kwani kusimama katikati kuna stara zaidi kwake.

Share this:

Related Fatwas