Hukumu ya Swala kwa Mgonjwa wa ‘Alz...

Egypt's Dar Al-Ifta

Hukumu ya Swala kwa Mgonjwa wa ‘Alzheimer

Question

“Je, hukumu ya Swala kwa mgonjwa wa Alzheimer (ugonjwa unaoathiri ubongo) ni ipi: je, huondolewa kwake? Na je, anatakiwa kuzilipa Swala alizoziacha pale anapopata fahamu tena?”

Answer

“Mgonjwa wa Alzheimer hupitia hatua tatu kuu ambazo dalili zake hujitokeza hatua kwa hatua. Ingawa zote hushirikiana katika maana ya kusahau, kuchanganyikiwa na kupungua kwa uelewa, kila hatua hutofautiana kwa kiwango cha ugonjwa, daraja la ufahamu na uwezo wa kujidhibiti.”

“Hatua ya kwanza ya ugonjwa huu ndiyo inayohusiana moja kwa moja na hukumu ya kisharia kuhusu utekelezaji wa Swala. Hata hivyo, hukumu hiyo inafungamana na uwezo na kadiri ya kuweza kufanya, kwa mujibu wa kanuni isemayo: ‘Kinachowezekana hakiondolewi kwa sababu ya kisichowezekana.’ Katika hatua hii, mgonjwa anaweza kusaidiwa na baadhi ya vifaa vya kisasa vinavyomkumbusha au kumsaidia kukamilisha ibada, kama vile vifaa vya kielektroniki au miswala yenye teknolojia maalumu.

Ama hatua ya pili na ya tatu: huingia katika kundi la maradhi ya akili yaliyotajwa wazi na wanazuoni kuwa hupoteza uwezo wa akili na kuondoa matendo yake. Wataalamu wa Fiqhi wamekubaliana kwamba mgonjwa katika hali hizi mbili halazimiki kuswali. Hata hivyo, endapo atapona na akili ikarejea, basi hukumu inamhusu tena, na analazimika kuswali Swala za wakati uliopo. Kuhusu Swala alizoziacha wakati wa ugonjwa: Wanazuoni wengi wanasema hazilipiwi, iwe ni chache au nyingi. Ingawa maandiko yamekuja kuhusu wazimu na waliopoteza akili, hukumu hiyo imepanuliwa kwa kila anayepoteza akili yake kwa sababu inayosameheka.”

Maelezo

Swala ni Faradhi ya lazima kwa kila mtu aliyebaleghe na mwenye akili timamu, awe mwanaume au mwanamke. Wajibu huu umetajwa wazi katika Qur’ani Tukufu, Sunna na kwa makubaliano ya Waislamu wote. Mwenyezi Mungu anasema: ‘Na shikeni Swala’ (Al-Baqara: 110), na tena: {Hifadhi Swala, na hasa Swala ya katikati} [Al-Baqara: 238], na pia: {Simamisha Swala katika ncha mbili za mchana na nyakati za usiku} [Hud: 114].

Ibn Abbas (R.A) amepokea kwamba Mtume Muhammad (S.A.W), alipomtuma Mu‘adh (R.A) Yemen, alimwambia: ‘Utakuja kwa watu wa Kitabu, basi jambo la kwanza unalotakiwa kuwalingania ni ibada ya Mwenyezi Mungu. Watakapomkubali Mwenyezi Mungu, wambie kuwa Amefaradhisha juu yao Swala tano katika mchana na usiku wao. Watakapozitekeleza, wambie kuwa Mwenyezi Mungu Amefaradhisha juu yao kutoa Zaka katika mali zao, zitakazorejeshwa kwa masikini wao. Watakapokubali, chukua kutoka kwao, lakini usichukue mali bora zaidi za watu.’ (Imepokewa kwa makubaliano ya Bukhari na Muslim).

Aidha, Waislamu wote wameafikiana kwamba Swala tano ni Faradhi ya lazima.

Mtu anayehesabika kuwa amekalifishwa (aliyechukuliwa hatua ya kisharia) ni yule anayekidhi masharti ya uhalali: Uislamu, kubaleghe na kuwa na akili timamu. Iwapo sharti lolote kati ya haya litakosekana, basi mtu huyo atapoteza sifa ya kuwajibika kwa Swala.

Uhalali kamili unaomfanya mtu awajibike kwa ibada unatokana na akili, kwa kuwa akili ndiyo chombo cha kufahamu na njia ya kuelewa. Ndiyo maana Wanazuoni wa Fiqhi wamekubaliana kwamba mgonjwa wa akili halazimiki kuswali katika hali ya ugonjwa wake. Aidha, Wanazuoni wengi wanasema pia halazimiki kulipa Swala alizoziacha baada ya kupona, kwa sababu uwezo wa kutekeleza ibada hupotea pale akili inapozimwa. Bila ya akili hakuna uwajibu wa kisharia, hivyo basi Swala zilizopita katika kipindi cha ugonjwa hazilazimiki kulipwa. Hoja yao ni kwamba sharia imeondoa jukumu na taklifu kwa mgonjwa wa akili na haimhutubii kwa amri hiyo.

Imepokewa kutoka kwa Ali bin Abi Talib (R.A) kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) amesema: ‘Qalam imeondolewa kwa watu watatu: kwa mwendawazimu aliyeondokewa na akili yake, kwa aliyelala hadi aamke, na kwa mtoto hadi abaleghe.’ Imepokelewa na Abu Dawud, Al-Nasa’i na Al-Daraqutni katika vitabu vyao vya Sunan, na pia Ibn Khuzaymah na Ibn Hibban katika vitabu vyao vya Sahih, pamoja na Al-Hakim katika Al-Mustadrak, naye akaihukumu kuwa sahihi.

Abu Dawud amesema: Ibn Jurayj amepokea kutoka kwa Al-Qasim bin Yazid, kutoka kwa Ali (R.A), na ameongeza ndani yake: ‘na mzee aliyepoteza kumbukumbu (Al-Kharif).’

Katika riwaya nyingine: ‘Na kwa mwendawazimu mpaka apone.’ Imepokelewa na Abu Dawud katika Al-Sunan, na pia Al-Tayalisi, Ahmad, Abu Ya‘la na Al-Shashi katika vitabu vyao vya Musnad, kutoka kwa Ali bin Abi Talib na Aisha (R.A).

Katika riwaya nyingine:‘Na kwa mwendawazimu mpaka arejee akili au apate fahamu.’ Imepokelewa na Ibn Al-Jarud katika Al-Muntaqa, na Ibn Majah na Al-Bayhaqi katika Al-Sunan, na Al-Hakim katika Al-Mustadrak, kutoka kwa Aisha (R.A).

Na katika riwaya nyingine: ‘Na kwa aliyeugua mpaka uponywe.’ Imepokelewa na Ahmad katika Al-Musnad, kutoka kwa Ali bin Abi Talib (R.A), na Ibn Al-Jazari katika Manaqib Al-Asad Al-Ghalib amehukumu isnadi yake kuwa sahihi.

Sifa zilizotajwa katika Hadithi, ingawa zimekuja kwa sura tofauti, zote zinarejea kwenye maelezo matatu yenye uhusiano wa karibu au yaliyo sawa. Kutokana nazo, zinapatikana hali tano: mtoto, mtu anayelala, aliyezimia, mwendawazimu, na mzee aliyechanganyikiwa. Kwa maana halisi, wote hawa hukusanyika katika makundi matatu, na hawahusishwi na taklifu ya kisharia.

Kwa sababu hiyo, Wanazuoni wametaja wazi kwamba hali nyingine pia huingia katika maana hii; kama vile kuzimia kuhusishwa na usingizi, na udhaifu wa uzee (kuchanganyikiwa) pamoja na upotevu wa akili kuhusishwa na wazimu. Hata zaidi, kila mtu ambaye akili yake imepotea kwa sababu inayosameheka, iwe kwa muda mfupi au mrefu.

“Ugonjwa wa Alzheimer ni jina linalokusanya ndani yake viwango mbalimbali vya maendeleo ya maradhi. Kimsingi, ni hali ya kudhoofika kwa seli za ubongo inayopelekea kupungua kwa kumbukumbu na uwezo wa akili, na hatimaye kushuka kwa kasi kwa fikra, ujuzi wa kitabia na kijamii. Ugonjwa huu ndio chanzo kikuu cha ugonjwa wa kusahau (dementia), ambapo unasababisha takribani kati ya asilimia 60 hadi 70 ya visa vyote.

Dementia kwa ujumla hutokea kutokana na magonjwa na majeraha mbalimbali ya ubongo, ikiwemo Alzheimer, kiharusi, dementia ya mishipa ya damu, dementia ya sehemu ya mbele au ya upande wa ubongo (frontal au temporal), na dementia yenye miili ya Lewy (Lewy bodies). Tofauti kati ya aina hizi hutambulika kupitia vipimo vya kazi za ubongo, kama vile vipimo vya uwezo wa kiakili, picha za uchunguzi wa ubongo na mbinu nyingine. Mara nyingine, mtu anaweza kuathirika na mchanganyiko wa aina zaidi ya moja kwa wakati mmoja.

Shirika la Afya Duniani (WHO), kupitia tovuti yake rasmi, limeeleza pia kwamba ugonjwa wa Alzheimer hupitia hatua tatu kuu, ambazo dalili zake hujitokeza taratibu hatua kwa hatua.

Hatua ya kwanza: Katika hatua hii mgonjwa hupungua nguvu zake na kumbukumbu hudhoofika. Dalili za kusahau huanza kujitokeza, ufahamu wa muda hupungua, na mara nyingi hupatwa na hali ya kuchanganyikiwa na kutokuwa na msisimko kwa mambo yanayotokea kumzunguka.

Hatua ya kati: Hapa mgonjwa husahau kwa kiwango kikubwa matukio mapya na majina, hupotea hata katika maeneo aliyoyazoea, ikiwemo nyumbani kwake. Tabia hubadilika, uwezo wa kuelewa hupungua, jambo linalosababisha ugumu wa kuwasiliana na wengine. Huuliza maswali mara kwa mara, husimama katikati ya sentensi na kushindwa kukamilisha maneno. Katika hatua hii, mgonjwa huhitaji msaada na uangalizi mkubwa.

Hatua ya mwisho: Katika hatua hii, mgonjwa hutegemea kikamilifu msaada wa wengine. Hupoteza kabisa shughuli zake, ufahamu wa muda na mahali huvurugika sana, na anakumbwa na ugumu mkubwa wa kuwatambua ndugu na marafiki. Anahitaji msaada wa karibu katika kujihudumia, hukabiliwa na ugumu wa kutembea, na mabadiliko ya tabia ambayo mara nyingine huongezeka na kuwa ya ukali au hata ya uhasama.

kiwango kikubwa na huwanyang’anya uhuru wao wa kujitegemea, hauchukuliwi kuwa sehemu ya kawaida ya uzee au kuishi maisha marefu.

Na japokuwa hatua tatu za ugonjwa huu hufanana katika dalili kuu za kusahau, kuchanganyikiwa na kupungua kwa ufahamu, bado zinatofautiana kati ya hatua moja na nyingine kwa kiwango cha maradhi, daraja la uelewa na uwezo wa kujidhibiti.

Katika hatua ya kwanza, mgonjwa bado anaweza kutekeleza majukumu yake mengi na mahitaji yake ya kila siku, ikiwemo ibada za kimwili kama Swala na saumu. Ikiwa mgonjwa ana uwezo wa kutekeleza ibada, basi analazimika kuitekeleza, kwa mujibu wa kanuni ya kisheria isemayo: ‘Kinachowezekana hakiondolewi kwa sababu ya kisichowezekana.’ Kanuni hii inatokana na kauli ya Mtume (S.A.W): ‘Ninapokuamrisheni jambo, fanyeni kadiri mnavyoweza.’ Katika hatua hii, mgonjwa anaweza pia kutumia vifaa vya kisasa vinavyomsaidia kukumbuka na kukamilisha ibada pamoja na tiba na dawa.

Ama katika hatua ya pili na ya tatu, ugonjwa hushinda akili ya mgonjwa, ufahamu wake hubadilika na matendo yake huchanganyikiwa. Hali hizi zinahesabiwa kuwa ni sehemu ya kupotea kwa akili, na hivyo mgonjwa huingia katika sifa zilizotajwa katika hadithi, ambazo zinamaanisha kuondolewa jukumu la kisheria kwa mwenye kuzipata. Wanazuoni wametaja wazi kuwa kila hali inayomnyima mtu uwezo wa kuelewa ujumbe wa sharia, inaleta maana ya kutotekelezeka kwa jukumu, kwa kuwa mojawapo ya masharti ya jukumu ni uwezekano wa kuelewa ujumbe huo.

Tunapata faida kutokana na yaliyotangulia:

Hukumu ya kisharia kuhusu utekelezaji wa Swala inahusiana moja kwa moja na uwezo na kadiri ya mtu kuweza kufanya.

Wanazuoni wa Fiqhi wameafikiana kwamba mgonjwa wa akili halazimiki kuswali katika hali ya ugonjwa.

Wengi wao pia wanasema haimlazimu kulipa Swala alizoziacha baada ya kupona, kwa kuwa uwezo wa utekelezaji hupotea pamoja na kupotea kwa akili. Bila akili, hakuna uwajibu wa kisheria, hivyo basi swala zilizopita katika kipindi cha ugonjwa hazilazimiki kulipwa.

Share this:

Related Fatwas